Mwalimu Helena Nyahuru Mahamba wa Shule ya Msingi ya Unyakhae katika Manispaa ya Singida akiwadhoofu kutokana na maradhi ya kisukari yanayomsumbua kwa miaka 17.
.........................
Na Dotto
Mwaibale, Singida
Kutokuwepo
kwa kipengele ndani ya Katiba ya Chama
cha Walimu Tanzania (CWT) cha kutotoa msaada kwa wanachama wake wanapokuwa na
changamoto mbalimbali ikiwemo kuumwa imewavuruga walimu wa Mkoa wa Singida.
Hali hiyo imewafanya
baadhi yao kujitoa kwenye chama hicho na kujiunga na vyama vingine vikiwepo Chama cha Kutetea Haki na Maslahi ya Walimu
Tanzania (CHAKAMWATA) na Chama cha Kulinda na Kutetea Walimu Tanzania (CHAKUHAWATA).
Akizungumza
na mwandishi wa habari hii mwanzoni mwa wiki Katibu wa CWT Manispaa ya Singida, Jones Madale alisema
kwenye katiba ya chama hicho hakuna kipengele kinachoeleza kumsaidia mwalimu
zaidi ya kutetea maslahi yao kwa mwajiri wao.
Kauli ya
katibu huyo imekuja kufuatia mwanachama wa chama hicho Mwalimu Helena Nyahuru Mahamba
wa Shule ya Msingi ya Unyakhae katika manispaa hiyo kuumwa ugonjwa wa kisukari
kwa miaka 17 ambapo chama hicho kimempa Sh.100.000 tu ndani ya kipindi hicho.
“ Mwalimu huyo ni mtumishi wa Serikali mwajiri
ndiye anayewajibika sisi kama wanachama jukumu letu ni kumsukuma atoe huduma
kwa mtumishi wake. Sisi huwa tunakwenda kumuangalia na kumpa pole pamoja na misaada
midogo midogo kama kumpa matunda lakini ndani ya katiba yetu hakuna kipengele
kinachoelezea kumsaidia,’ alisema
Madale.
Kutokana na
hali hiyo baadhi ya walimu wa Manispaa hiyo wamekiri wenzao kuhamia katika
vyama hivyo kwa ajili ya kufuata maslahi mazuri ambapo walitoa maoni yao kama
ifuatavyo.
Mwalimu wa
Shule ya Msingi Unyanga ambaye hakupenda jina lake liandikwe alidai kuwa licha
ya kutokuwepo kwa kipengele hicho watumishi wengine wa idara zingine wanapoumwa
wamekuwa wakipatiwa fedha za matibabu nje ya bima zao lakini siyo wa idara ya
elimu.
Mwalimu huyo
alisema kuwa walimu wamekuwa wakifanya kazi kubwa ya kuwatengeneza watumishi wa
ngazi tofauti wakiwepo viongozi hivyo maslahi
yao yanapaswa kuboreshwa.
“Kuna
mwalimu mkuu wa Shule ya Msingi Somoko Leonard Bundara Februari 23, 2026 alivunjika
mguu na kujeruhiwa kichwani baada ya kupata ajali ya pikipiki, na kupoteza
fahamu.
Alipopelekwa
Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Singida alipewa rufaa kwenda Hospitali ya
Benjamin Mkapa Dodoma ambapo mwajiri wake alitoa gari na majeruhi aligharamia mwenyewe
mafuta kwa kutoa Sh. 300,000,” alisema mwalimu huyo.
Hata hivyo mke
wa majeruhi huyo Mwalimu Mwajuma Faustine amethibitisha mme wake kutoa kiasi
hicho cha fedha na kudai kuwa tangu wafike hospitali hapo hakuna kiongozi
yeyote wa CWT wala mwajiri aliyefika
kumjulia hali zaidi ya baadhi ya walimu ambao ni rafiki zake.
Mwalimu
Helena Mahamba baada ya kushindwa kumudu gharama za matibabu alilazimika kubaki
nyumbani akijiuguza huku hali yake ikiendelea kudhoofu kila siku.
Taarifa zake zilipotolewa kwenye mitandao ya
kijamii wiki liyopita akiomba msaada wa matibabu na kwa jitihada za Naibu
Waziri wa Afya Dkt. Florence Samizi alipoisoma taarifa hiyo aliagiza mgojwa
huyo apelekwe Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Singida kuanza matibabu upya mara
moja.
Pamoja na
kuanza matibabu hali yake iliendelea kuwa mbaya na Machi 14, alipata rufaa ya
kuhamishiwa Hospitali ya Benjamin Mkapa jijini Dodoma kwa ajili ya kupata
matibabu kwa kusafirishwa na mwajiri wake.
Mwajiri wake
alitoa fedha za kununua mafuta na Hospitali ya Rufaa Mkoa wa Singida ilitoa
gari la wagonjwa.
Ombi kubwa
la walimu hao ni katika katiba yao kuwepo kipengele cha kuwasaidia walimu
wanapo kuwa na changamoto mbalimbali ikiwemo ya magonjwa kutokana na michango yao
wanayoichangia kila mwezi.
“Walimu Manispaa ya Singida tupo zaidi ya 800 ambapo kwa mwezi kila mwalimu hukatwa siyo chini ya Sh. 33,000 na wale ambao wapo daraja la juu hukatwa zaidi ya kiwango hicho. Ni fedha nyingi zinazokusanywa ukipiga mahesabu hiyo ni kwa manispaa pekee, tunaomba ziwe zinatumika kutusaidia tunapokuwa na changamoto badala ya kusubiri kusaidiwa jeneza na kusafirishwa kwenda makwetu tukifa,” alisema Mwalimu Robert Mtinga.
Kwa upande
wake Mwalimu Helman Magoti alisema ni vema kuipitia katiba yao vizuri ili
kuielewa kama hakuna kipengele cha kutambuliwa wanapokuwa na changamoto ya maradhi
ili wapiganie kiwekwe kwa maslahi mapana ya walimu.
“Walimu wengi ni wagonjwa lakini wanajipambania wenyewe kupata matibabu, licha ya kuwa na bima dawa zingine zenye gharama kubwa hushindwa kuzipata na kulazimika kwenda kuzinunua. Katiba ya chama chetu ikiwekwa kipengele cha kututambua itatupunguzia mzigo wa kujigharamia matibabu ukizingatia mishahara yetu siyo mikubwa,” alisema Mwalimu Gregory Michael wa Shule ya Msingi Uhamaka.
Baada ya
habari hiyo kuandikwa kwenye mitandao ya kijamii viongozi wakuu wa CWT Manispaa
ya Singida Machi 8, 2026 wakiongozwa na Mwenyekiti wa chama hicho, James Msai
walikwenda kumjuali hali Mwalimu Mahamba.
Viongozi hao
mara baada ya kuwasili kwa mgonjwa huyo ajenda
yao kubwa ilikuwa ni kuona namna ya Mwalimu Mahamba kurudishwa nyumbani kwao
baada ya kushauriana na ndugu zake huku wakiahidi kufuatilia kwa mwajiri wake
barua aliyoandika kuomba kusaidiwa matibabu.
Hatua hiyo
ilijiri baada ya kuona hana mtu wa uhakika wa kumuuguza katika eneo hilo
analoishi, ambapo walitoa pole yao kwa kumpa sabuni, mipira ya kuvaa mikononi
(Groves) na Pempasi.
Viongozi
wengine waliokuwepo katika msafara wa kwenda kumjulia hali mwalimu mwenzao huyo
ni pamoja na Katibu wa chama hicho Manispaa ya Singida, Jones Madale na
Wawakilishi, Yasinta Makaya na Innosanta Shayo.
Baadhi ya
walimu wamepongeza hatua zilizochukuliwa na mwajiri wake Mkurugenzi Mtendaji wa
Manispaa ya Singida na uongozi wa Hospitali ya Rufaa ya Singida kwa kufanikisha
kumpeleka mgonjwa huyo Hospitali ya Benjamin Mkapa kwa ajili ya kuendelea
kupata matibabu zaidi ambapo amelazwa wodi namba mbili ghorofa ya pili.
Pamoja na
kuanza kupata matibabu Mwalimu Mahamba anahitaji msaada wa mahitaji ya
kibinadamu kama chakula, maji, sabuni na mengine mengi ambayo yanahitaji fedha
kwa atakaye guswa kumsaidia anaweza kumtumia kiasi chochote kupitia namba 0787820053
au 0759521565 na Mungu atakubariki kwa utoaji wako kwani kutoa siyo utajiri
bali ni moyo wa mtu.
Uongozi wa Singidani Blog unatoa shukrani na pongezi nyingi kwa Naibu Waziri wa Afya Dkt. Florence Samizi kwa kuchukua hatua za haraka na kufanikisha Mwalimu Helena Nyahuru Mahamba kuanza kupata matibabu baada ya kusoma habari hiyo.
Mwalimu Helena Nyahuru Mahamba akifanya mazoezi ya kutembea nyumbani kwake Unyakhae Manispaa ya Singida.
Mwalimu Helena Nyahuru Mahamba alivyokuwa kabla ya kuanza kuumwa.
Taarifa hii imeandikwa na Dotto Mwaibale namba 0754362990.








No comments:
Post a Comment