DC IRAMBA: UMILIKAJI WA ARDHI KIHOLELA NDIO CHANZO CHA MIGOGORO - SINGIDANIBLOG

Habari za Hivi Punde

Post Top Ad

Friday, 28 October 2022

DC IRAMBA: UMILIKAJI WA ARDHI KIHOLELA NDIO CHANZO CHA MIGOGORO

Mkuu wa Wilaya ya Iramba, Suleiman Mwenda akimkabidhi hati ya kumiliki ardhi Mariam Msengi Mkumbo wakati wa zoezi la kutoa hati katika eneo la Lulumba, Kiomboi wilaya humo mkoani Singida jana. 
Kamishna Msaidizi wa Ardhi Mkoa wa Singida, Shamim Hoza akizungumza katika hafla hiyo.
Mkuu wa  Wilaya ya Iramba, Suleiman Mwenda akisisitiza jambo kwenye hafla hiyo.
Maafisa Ardhi Mkoa wa Singida wakiendelea na zoezi la umilikishaji wa ardhi kwa Wananchi wa Shelui wilayani Iramba mkoani hapa jana. Kulia ni Kamishna Msaidizi wa Ardhi Mkoa wa Singida, Shamim Hoza.
Zoezi la umilikisha ardhi Shelui wilayani Iramba likiendelea.
Wakina mama wakisubiri kupatiwa hati zao eneo la Lulumba Kiomboi, wilayani Iramba.
Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa, Kijiji cha Lulumba, Yohana Lyanga, akizungumza kwenye hafla hiyo.
Diwani wa Kata ya Kiomboi, Omary H. Omary akizungumza kwenye hafla hiyo.
Hafla ikiendelea.
Msajili wa Hati Msaidizi Mkoa wa Singida, Palmon Rwegashora akizungumza katika hafla hiyo.
Mkuu wa Wilaya ya Iramba, Suleiman Mwenda akiwa katika picha ya pamoja na wananchi waliokabidhiwa Hati za kumiliki ardhi wakati wa zoezi la kutoa hati katika eneo la Lulumba, Kiomboi wilaya humo mkoani Singida jana.

....................................... 

Na Dotto Mwaibale, Iramba

MKUU wa Wilaya ya Iramba, Suleiman Mwenda amesema umilikaji wa ardhi kiholela ndio chanzo kikubwa cha migogro ya ardhi nchini.

Mwenda ambaye alikuwa mgeni rasmi katika hafla ya kukabidhi hati za ardhi 100 kwa wananchi wa Lulumba Kiomboi wilayani humo ambao wamekamilisha zoezi zima la kuzilipia na kupata mafunzo ya umuhimu wa kupima ardhi zao yaliyotolewa na Ofisi ya Ardhi Mkoa wa Singida alisema jambo hilo limekuwa ni changamoto kubwa wilayani humo.

Alisema ardhi ni rasilimali muhimu sana kwani kila kitu kinachofanyika hapa duniani kinafanyika juu ya ardhi na kuwa masuala  yanayohusu  ardhi  ni  nyeti  sana.   

Mwenda alisema kuwa vita vingi vilivyopo duniani chanzo chake ni ardhi ikiwepo ile inayoendelea kule ukreni na kutingisha uchumi wa dunia.

“Mimi katika kesi ninazokumbuna nazo ofisini kwangu nyingi ni za migogoro ya ardhi ambazo ni kati ya asilimia 80 hadi 90 na sababu kubwa inayosababisha hali hiyo ni watu wengi kumiliki ardhi kienyeji bila ya kufuata utaratibu unaotambulika na Serikali” alisema Mwenda.

Mwenda aliomba idara ya ardhi wilayani humo kuhakikisha inaharakisha kupima ardhi ya wananchi wote jambo litakalosaidia kuleta maeendeleo na kupunguza migogoro hiyo ambayo imekithiri.

Kamishna Msaidizi wa Ardhi Mkoa wa Singida, Shamim Hoza akizungumza katika hafla hiyo aliomba ajenda ya ardhi iwe namba moja kwenye vikao vya baraza la madiwani la halmashauri ya Wilaya ya Iramba kwa tukizingatia kuwa ardhi ni sekta wezeshi kwa kuwa kila kitu kinafanyika juu yake.

“Ardhi hii ni lazima tuithamini, tuilinde na kuitunza kwa nguvu zetu zote na ili tufanikiwe tunapaswa tuwe na ajenda hiyo ya kudumu” alisema Hoza. 

Hoza alitaja faida kadhaa za kuwa na hati ya kumiliki ardhi ni kuwa na uhakika wa usalama wa ardhi ya muhusika anayomiliki, nyumba au maendeleo yoyote aliyoyafanya katika ardhi hiyo, hati hiyo kutumika katika kuomba mkopo benki ikitumika kama rehani na kutumika kama dhamana mahakamani na polisi na hati hiyo inaweza kusaidia kuhamisha umiliki wa ardhi kiuhalali na kwa uhakika.

Hoza alisema mchakato huo wa kutoa hati kwa wananchi mkoani hapa unaendelea katika wilaya tatu za Iramba, Manyoni na Ikungi ambapo maofisa wa ardhi Mkoa wa Singida wakishirikiana na wenzao katika wilaya hizo wamekuwa wakitoa elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu wa kuwa na hati za umiliki wa ardhi huku muitikio ukiwa mkubwa.

Alisema ofisi yake imejipanga  kuhakikisha zoezi hilo litaendelea vizuri katika wilaya zote mkoani hapa na kuwa la mafanikio.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad