Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Singida, ACP Lucas Mwakatundu, akiteta jambo na wasaidizi wake wakati akizungumzia tukiohilo la mauaji. |
Na Dotto Mwaibale, Singida.
ANTHONY Thomas Lugulu (41) mkazi wa Kijiji cha Ng'anguli Kata ya Maluga
Wilaya ya Iramba mkoani Singida amemuua mke wake kwa kumgiga na kitu
kizito kichwani na kukipasua na kisha
kujiua kwa kujinyonga kwa kutumia waya.
Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Singida, ACP Lucas Mwakatundu, akizungumza
na waandishi wa habari jana alisema tukio hilo lilitokea Oktoba 18, mwaka huu
ambapo uchunguzi wa Jeshi la Polisi umebaini kuwa chanzo cha mauaji hayo ni
wivu wa kimapenzi kati ya wanandoa hao.
Mwakatundu akielezea tukio hilo alisema Oktoba 18, 2022 saa 2:30 usiku
zilitokea taarifa za mauaji katika kituo kikuu cha polisi wilayani Singida
kutoka kwa raia mwema katika mtaa wa Bima-Unyankindi kata ya Mitunduruni.
Alisema baada ya polisi kufika eneo la tukio alikutwa mwanamke aitwaye Tatu
Rashid (38) akiwa amefariki ndani ya chumba chake huku mwili wake ukiwa na
majeruhi yaliyotokana na kupigwa na kitu kizito kichwani.
"Timu ya wapelelezi kutoka Jeshi la Polisi ilipofika eneo la tukio na kufanya
uchunguzi wa awali na kubaini kuwa mwili wa marehemu ulikuwa na jeraha kubwa
kichwani lililotokana na kupigwa na kitu kizito huku mwili huo ukiwa umelala
chali chini na kufunikwa kwa shuka na blanketi," alisema.
Alisema Oktoba 18, mwaka huu saa 12:56 asubuhi mume wa marehemu (Tatu),
Antoni Thomas Lugulu naye alikutwa akiwa amejiua kwa kujinyonga kwa kutumia
waya uliofungwa kwenye mti nje ya nyumba yake.
Mwakatundu alisema katika eneo la tukio kulikutwa simu ya marehemu pamoja
na ujumbe unaosema asibugudhiwe mtu yeyote kwa maamuzi aliyoyachukua.
"Jeshi la Polisi Mkoa wa Singida linatoa wito kwa wananchi kuachana na vitendo vya kikatili na kujichukulia sheria mkononi,wananchi wanatakiwa kuishirikisha jamii inayowazunguka,viongozi wa dini pamoja na wa serikali za mitaa kutatua migogoro yao ili itatuliwe kwa amani," alisema.








No comments:
Post a Comment