Wanufaika wa TASAF wa Kikundi cha Pain for Succes wakiwa katika picha ya pamoja
Na Dotto Mwaibale, Chalinze, Pwani.
WALENGWA 2517 wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) katika Halmashauri ya
Wilaya ya Chalinze mkoani Pwani wamekithi vigezo vya kupata ruzuku ya
uzalishaji ambayo mpango wake mahususi ni kuwatoa kwenye mpango wa TASAF ili waweze
kujitegemea.
Hayo yabainishwa na Afisa Ufuatiliaji wa Miradi TASAF, Janeth Mtelelah wakati
akizungumza na waandishi wa habari baada ya kuwatembelea walengwa kadhaa wa TASAF na
kukagua miradi yao mbalimbali ya ufugaji wa kuku, mbuzi na biashara ndogondogo.
Alisema walengwa hao 2517 ni kati ya walengwa 6,011 ambao walikithi vigezo
vya kusoma na kupata shughuli za kufanya kama zilivyotajwa hapo juu kikiwemo
kilimo ambapo waliomba fedha kuanzia Sh.100,000 hadi 500,000.
“Fedha hizi tunawapa kwa awamu ambapo awamu ya kwanza tunawapa aslimia 50
kwa wafanyabiashara, asilimia 70 kwa wale wa mifugo na asilimia 60 kwa ajili ya wale wa
kilimo na tumekuwa tukitoa kwa awamu ili kuweka uwajibikaji na kuweza kuwapima ambapo jambo la kushukuru
kwa awamu ya kwanza walengwa 1960 miradi yao imefanya vizuri kutokana na timu yetu ya ufuatiliaji ambayo ilikuwa ikiwatembelea mara kwa mara” alisema Mtelelah.
Alisema kuwa utaratibu uliotumika
kutoa ruzuku hizo ni kwa kila mnufaika kuandika andiko lake la mradi na
kisha kuomba fedha ambapo alipatiwa kulingana na vigezo vilivyobainishwa.
Mtelelah alisema hayo yote yanafanyika kwa uwezeshaji mkubwa anaoufanya
Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuwajali wananchi wa hali ya chini kwani kabla ya
kuwawezesha walengwa hao baadhi yao walikuwa hawawezi kupata milo mitatu ambayo
wanaipata hivi sasa ambapo pia wameweza kuwapeleka watoto wao shuleni hakika ni kazi kubwa iliyofanywa
na Mama Samia.
Alisema licha ya Rais kuelekeza fedha nyingi kwenye shughuli mbalimbali za
kijamii, ameona ni vema kutenga kiasi kikubwa cha fedha ikiwa ni pamoja na kutoa magari
kwa TASAF nchi nzima kwa ajili ya
utekelezaji wa mpango wa kuzinusuru kaya za walengwa ambao kwa kiasi kikubwa
unazisaidia kaya maskini kujikwamua kutoka kwenye umaskini.
Mratibu wa TASAF katika halmashauri hiyo Michael Mwakanjuki alisema
kazi kubwa ambayo wanaifanya ni kwa walengwa hao ambao wanapata fedha hizo
kuhakikisha wanashirikiana na wataalamu ili miradi yao iende vizuri na kuinua
uchumi wa kaya zao.
Alisema wataalam au wawezeshaji waliopewa mafunzo wamekuwa wakipita kwenye
maeneo yao kutoa ushauri ili kukuza miradi yao.
Mwezeshaji wa shughuli za TASAF katika halmashauri hiyo Flora Balakana
alisema katika shughuli za uzalishaji wamekuwa wakishirikiana na maafisa ugani
katika vijiji 84 na kuhakikisha walengwa wao wote wanafikiwa na kupewa huduma
stahiki ili waweze kutekeleza miradi yao.
Alisema mafanikio ya walengwa hao hayaji hivi hivi bali yanatokana na kazi
kubwa wanayoifanya maafisa ugani kwa kushirikiana nao ambapo alitumia nafasi
hiyo kuishukuru Serikali kwa kuwezesha kuwapeleka maafisa ugani kila kijiji ili
kuwasaidia wananchi wakiwemo walengwa hao wa TASAF.
Baadhi ya walengwa waliotembelewa na miradi yao kukaguliwa ni Mwajuma
Rajabu na Prisca Felix wakazi wa Msoga ambao wanafuga kuku, Veronica Kumpite
(42) na Maria Msigala (60) ambao wanajishughulisha na ufugaji wa mbuzi katika Kijiji cha Mindutulieni.
Wanufaika wengine waliotembelewa ni Kikundi cha Wanawake cha Pain for Succes ambao
wanaendesha miradi ya kilimo, ufugaji wa bata na sasa wanafyatua matofali kwa
ajili ya kujenga banda la kuku ili waweze kuanzisha ufugaji wa kuku.
Wanakikundi hao ambao wanamoto wa maendeleo waliweza kutoa burudani ya nyimbo mbalimbali za kumshuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuwajali wanawake kupitia TASAF na shairi lililoimbwa kwa umahiri mkubwa na Msanii Chozi Lukanga.












No comments:
Post a Comment