..................................................
Na Dotto Mwaibale, Singida
SHIRIKA la Umeme Tanzania (TANESCO) kupitia kwa Mkurugenzi wake Mtendaji , Gissima Nyamo-Hanga limekuja kivingine baada ya shirika hilo Mkoa wa Singida kutoa matofali 300 kwa ajili
ya kusaidia ujenzi wa madarasa katika Shule ya Msingi Mnung'una iliyopo Wilaya ya
Singida mkoani hapa.
Akikabidhi matofali hayo Disemba 2, 2023 kwa uongozi wa shule hiyo kwa
niaba ya Meneja wa Shirika hilo Mkoa wa Singida, Afisa wa Tanesco, Juma Omari
alisema wametoa matofali hayo ikiwa ni kuunga mkono jitihada za Serikali
inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan za kuhakikisha wanafunzi wanapata
mazingira bora ya kusomea kwa kujengewa miundombinu mizuri.
"Hatua hii ya utoaji wa matofali haya ni agizo la Mkurugenzi
wetu Mtendaji wa Tanesco Gissima Nyamo-Hanga alilolitoa kupitia Meneja wetu kuja kutoa msaada huu ambao
umelenga kuwasaidia wanafunzi kupata mazingira bora ya kusomea," alisema
Omari.
Omari alisema utoaji wa msaada wa namna hiyo utakuwa endelevu na utafanyika katika shule zingine za msingi mkoani hapa
ambapo alitumia nafasi hiyo kuyaomba mashirika mengine nayo kujitoa kwa ajili
ya kusaidia ujenzi wa miundombinu ya shule zetu.
Mwalimu Mkuu wa Shule hiyo, Bahati Ramadhani akipokea msaada huo
alilishukuru shirika hilo kwa kutekeleza ahadi yao waliyoitoa katika mahafali
ya darasa la saba ya mwaka huu baada ya kuwaomba kuchangia chochote katika
ujenzi wa madarasa.
"Leo tunafuraha kubwa ya kupokea matofali haya ikiwa ni ahadi
iliyotolewa na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) Mkoa wa Singida ahadi yao
wameitimiza kikamilifu tunawashukuru sana na tunawaomba waendelee kuwa na moyo
huo huo wa kusaidia ujenzi wa shule mbalimbali mkoani hapa," alisema
Ramadhani.
Mwalimu Mkuu huyo alitumia nafasi hiyo kumshukuru Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha nyingi kwa ajili
ya kujenga miundombinu katika shule mbalimbali na kuwa na katika shule hiyo ya
Mnung'una amewapa fedha kwa ajili ya kujenga vyoo na kuondoa kabisa changamoto
iliyokuwepo ya ukosefu wa vyoo.
Aidha, aliwaomba wadau wengine yakiwemo mashirika ya umma kuiga mfano
wa shirika hilo kwa kujitoa kusaidia shughuli za maendeleo ya kijamii badala ya
kusubiri kazi hizo kufanywa na Serikali.Wafanyakazi wa TANESCO wakishusha matofali hayo wakati wa kuyakabidhi kwa uongozi wa shule hiyo.







No comments:
Post a Comment