" />

HABARI ZA HIVI PUNDE

CHADEMA YAWATAKA WANANCHI SINGIDA KUPAZA SAUTI DHIDI YA SERIKALI KUKITHIRI VITENDO VYA UTEKAJI WATU



Makamo Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Taifa, Tundu Lisu (wa tatu kutoka kushoto( akiongoza maandamano ya amani yaliyoandaliwa na chama hicho yaliyoanzia Mandewa Manispaa ya Singida na kupita katika baadhi ya mitaa hadi Stendi ya Zamani ulipofanyika mkutano wa hadhara Aprili 27, 2024.

Makamo Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Taifa, Tundu Lisu akiwahutubia Wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika Stendi ya Mabasi ya Zamani Mkoa wa Singida mwishoni mwa wiki. Aprili 27, 2024

................................

Na Dotto Mwaibale, (Singidani Blog)

WANANCHI Mkoa wa Singida wametakiwa kupaza sauti kwa Serikali ili kukomesha kukithiri kwa vitendo vya utekaji wa watu vilivyoshamiri mkoani hapa.

Kauli hiyo ilitolewa na Makamo Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Taifa, Tundu Lisu wakati akiwahutubia mwishoni mwa wiki  wananchi wa Mkoa wa Singida kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika Stendi ya Mabasi ya Zamani ulioandaliwa na chama hicho baada ya kufanyika kwa maandamano ya amani yaliyopita katika maeneo kadhaa ya mji wa Singida.

Lisu alitoa ombi kwa wananchi hao huku akiinyoshea  kidole Serikali kwa kuwa kimya dhidi ya vitendo vya utekaji na upoteaji wa watu wakiwemo wafanyabiashara wawili wa Mkoa wa  Singida ambao alidai walipotea mwishoni mwa mwaka jana na kuwa walichukuliwa na maafisa wa Jeshi la Misitu (TFS)

"Hawa wasiojulikana hatuwajui majina lakini tunajua ni kinani na tunajua wanatokea wapi, ni wao na askari polisi wao na usalama wa taifa wao"

Lisu alisema chama hicho kinafanya maandamano nchi nzima baada ya Serikali kuwa kimya kufuatia kupanda kwa gharama za maisha, kutaka katiba mpya, kukithiri kwa tozo na kuwekwa kwa kikotoo.

Alisema wanafanya maandamano baada ya kuona ardhi ya watanzania ikiuzwa kwa watu wanaoitwa wawekezaji kutoka nje ya nchi, kukithiri kwa kuuza rasilimali za nchi kama bandari na ubadhirifu mkubwa unaofanyika akitolea mfano kuwa kila mwaka ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) imekuwa ikibaini kupotea kwa zaidi ya Sh.Trilioni 2,  lakini hakuna hatua yoyote inayochukuliwa dhidi ya wahusika.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Singida,  Jackson Jingu aalisema katika muendelezo wa wimbi hilo la utekwaji na ushambuliaji wa watu wiki  iliyopita chama hicho kimempoteza mwanachama wao Peter Mtinangi ambaye aliuawa na watu wanaoitwa wasiojulikana na kumuhusisha mmoja wa wanasiasa katika wilaya hiyo ya Ikungi.

"Hakuna watu wasiojulikana, tulimsikia Mwenyekiti wa UVCCM Mkoa wa Bukoba akisema watu wanaomtukuna Rais watawapoteza na polisi wasiwatafute," alisema Jingu.

Naye Mwenyekiti wa Kamati ya Sera Chadema Kanda ya Kati,  David Djombe alisema wanaandama kuishinikiza Serikali kubadili mfumo na kuacha kuleta wakuu wa mikoa, wilaya na wakurugenzi wa halmashauri kwa kuteuliwa badala yake wanataka viongozi wanaowataka wenyewe.

"Nchi hii ina mambo ya ajabu sana, mkuu wa mkoa analetwa, mkuu wa wilaya analetwa, mkurugenzi, tunaandamana kudai katiba mpya ambayo itatuletea wakuu wa mikoa, wilaya na wakurugenzi tunaowataka sisi" alisema

Kwa upande wake Wakili Msomi wa kujitegemea kutoka Mkoa wa Mbeya, Boniface Mwambukusi alisema watu wanapotea nchini lakini mtu akihoji juu ya hilo anaambiwa anashusha hadhi ya jeshi la polisi.

Mwabukusi alisema kuwa Mkoa wa Singida unaweza kuendelea bila ya kuwepo kwa wakuu wa wilaya mkoa kutokana na waliopo majukumu yao kutoeleweka.

"Tunataka katiba mpya ambayo italinda maslahi ya kila mwananchi, sio watu wanapotea ukihoji unaambiwa unashusha hadhi ya jeshi la polisi, hawa askari wakijengewa mazingira bora ya maisha yao hizi kesi za kusingizia zitatoka wapi?, " alihoji Mwabumkusi huku akishangiliwa.

Katika mkutano huo baadhi ya wananchi akiwemo Juma Mwiru ni miongoni mwa waliojitokeza kutoa kero zao na kueleza kutekwa kwa ndugu zake wawili walitekwa tangu Desemba 28, 2023 na mpaka leo hawajapatikana wala hawana taarifa yoyote ya mahali walipo na kama wapo hai au wamekufa na kuwa wamekuwa changamoto kubwa wanapozitembelea familia za ndugu zake hao kutokana na watoto kuishi maisha magumu na kuuliza maswali kila wakati wakiuliza walipo baba zao na siku watakayorudi.

"Tunaomba msaada jamani, familia inateseka mno, ndugu zangu wamepotea tokea mwezi wa 12 mpaka sasa hakuna taarifa yoyote kuhusu walipo" alisema.

Wananchi walioudhuria maandamano na mkutano huo walijitokeza kwa wingi huku wakiwa na mabango yaliobeba jumbe mbalimbali huku asilimia kubwa yakidai katiba mpya pamoja na kupungua kwa gharama za maisha.

Maandamano ya namna hiyo ni ya kwanza kufanyika katika Mkoa wa Singida na nimuendelezo wa maandamano mengine  kwani tayari yamekwisha fanyika kwenye mikoa mingine ikiwa ni ajenda ya chama hicho ya  kudai mambo ya msingi ya wananchi wa Tanzania.

Wakili Msomi wa kujitegemea kutoka Mkoa wa Mbeya, Boniface Mwambukusi, akizungumza kwenye mkutano huo.
Mjumbe wa Kamati Kuu Chadema Taifa, ambaye pia ni Mbunge wa Bunge la Wananchi kupitia Jimbo la Isimani mkoani Iringa, Patrick Ole Sosopi akizungumza kwenye mkutano huo.
Mbunge Mstaafu wa Chadema Jimbo la Mlimba ambaye pia ni Mbunge wa Bunge la Wananchi kupitia jimbo hilo mkoani Morogoro Suzana Kiwanga akizungumza kwenye mkutano huo. 
Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Singida, Jackson Jingu akiunguruma kwenye mkutano huo.
Mwakilishi wa Katibu wa Chadema Kanda ya Kati, David Jumbe, akizungumza kwenye mkutano huo.

Katibu wa Chadema Jimbo la Singida Mjini, Mutta Adrian akiongoza itifaki ya kupokea maandamano hayo kabla ya kuanza mkutano huo wa hadhara.

Mwenyekiti wa Baraza la Wazee Chadema Mkoa wa Singida, Wilson Lutha akizungumza.
Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Morogoro, Jackson Malisa akizungumza.
Katibu wa Baraza la Wanawake Chadema (BAWACHA) Mkoa wa Singida, Beatrice Asikey akichangia jambo kwenye mkutano huo.
Wakili Deogratius Mahainyila, akizungumza kwenye mkutano huo..
Viongozi mbalimbali wakiwa meza kuu wakati wa mkutano huo.
Aliyekuwa Spika wa Bunge la Wananchi kupitia chama hicho, Celestine Simba akizungumza.
Mwenyekiti wa Kamati ya Mafunzo wa Chadema Kanda ya Kati, Imelda Malley akishusha nondo kwenye mkutano huo.
Mbunge wa Bunge la Wananchi wa Chadema Mkoa wa Tabora Martin Mussa  akizungumza kwenye mkutano huo.
Makamo Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Taifa, Tundu Lisu akifurahia jambo na Wakili Msomi, Boniface Mwambukusi wakati wa mkutano huo.
Katibu wa Chadema Mkoa wa Singida, Samwel Maro, akiongoza mkutano huo.
Wananchi wakionesha mabango yenye jumbe mbalimbali wakati wa mkutano huo huku askari polisi wakiimarisha ulinzi.
Wananchi wakiwa kwenye mkutano huo huku askari polisi wakionekana wakiimarisha ulinzi.
Mkutano huo ukiendelea.
Mabango yakioneshwa wakati wa mkutano huo.
Wananchi wakipunga mkono kuonesha ishara ya kukikataa Chama Cha Mapinduzi (CCM)
Mkutano ukiendelea.
Wananchi wakiwa kwenye maandamano hayo.
Maandamano yakiendelee kwenye baadhi ya mitaa ya mji wa Sindida.
Mabango yenye ujumbe mbalimba yakioneshwa wakati wa maandamano hayo.
Maandamano yakichanja mbuga katika ya Mji wa Singida huku Jeshi la Polisi likiimarisha ulinzi wa kutosha.
Taswira ya halisi ya mkutano huo.


 

No comments