.............................
Na Dotto Mwaibale, Mkalama
HALMASHAURI ya Wilaya ya Mkalama mkoani Singida imeibuka kidedea kwa kuwa
na hoja 14 za Mdhibiti na
Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), na kuzishinda halmashauri zingine sita za mkoa huo.
Hoja hizo
katika kila wilaya ni kama ifuatavyo, Wilaya ya Itigi ilikuwa na hoja 45 na
sasa zimebaki 15, Wilaya ya Ikungi hoja 28 na zilizobaki ni 17, Iramba hoja 75
ambazo zimebaki ni 22, Manyoni hoja 59,na ambazo zimebaki kwa hatua mbalimbali za
utekelezaji ni 17, Singida Manispaa zilikuwa hoja 64 na Wilaya ya Singida
zilikuwa 54 na zilizobaki ni 16.
Kufuaatia
ushindi huo mnono Mkurugenzi Mtendaji wa halmashauri hiyo, Asia Mesos,
Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo James Mkwega pamoja na timu yao ya wataalamu
wamepongezwa kwa nyakati tofauti wakati wa kikao maalumu cha Baraza la madiwani
kilichoketi jana kwa ajili ya kupitia hoja za CAG.
Akizungumza Juni 28, 2024 katika kikao hicho Mkuu wa Mkoa wa
Singida, Halima Dendego alitoa miezi mitatu kwa halmashauri hizo kuhakikisha
ndani ya kipindi hicho ziwe zimezimaliza hoja zote ambazo zinatia dosari.
“Leo nipo
halmashauri ya sita na sisi kama mkoa tunasubiriana hadi Septemba 30, 2024 hoja
zote ziwe zimemalizika kuendelea kuwa nazo ni kuyakumbatia mapungufu yale
aliyoyaona CAG,” alisema Dendego.
Dendego
aliziomba halmashauri hizo kupitia kamati zao za fedha zifanye kila
linalowezekana kuhakikisha ndani ya miezi hiyo hoja zote ziwe zimefungwa ambapo
pia alitoa angalizo kwa wakuu wa idara kuwa mtu yeyeyote atakayebainika
kuzaliza hoja atawajibika mwenyewe kuzijibu kwani yeye na viongozi wengine
hawataitisha kikao kuzijibu.
“Kutengeneza
hoja binafsi nachukulia kama kula bila kunawa, sitegemei katika ustaarabu huo
tulionao wa 2024 kwamba kunawatanzania bado wanakula bila ya kunawa,”
alisisitiza Dendego.
Dendego
aliwataka madiwani wa halmashauri hiyo kutokuwa sehemu ya watu ambao
wanalalamika kutokukamilika kwa miradi badala yake wachukue hatua kama sheria
inavyoelekeza ya kumshughulikia mtu yeyeyote ambaye watamuona anataka
kuwarudisha nyuma.
Aidha Dendego
alisema Rais Samia, Mama wa Taifa na Chifu Hangaya amekuwa akitoa fedha nyingi
za kutekeleza miradi katika mikoa yote lakini atashangaa kuona mikoa iliyopo
pembezoni mwa nchi yetu kama Katavi na mingine ikikamilisha miradi yao kwa
wakati na Mkoa wa Singida ukishindwa kwa madai eti fedha hazitoshi. Jambo hilo
na mazoea ya namna hiyo kwake hayana nafasi.
“Singida
mnamchanga wa kutosha, maji, mawe na viwanda tena mpo jirani na Mkoa wa Dodoma
eti mnasema miradi inashindwa kukamilika kwa sababu hela hazitoshi acheni tabia
hiyo mimi nataka kuona miradi inakamilika na chenji inabaki,” alisema Dendego.
Mkuu huyo wa
Mkoa wa Singida aliwataka wataalamu na maofisa watendaji mkoani humo kuwa
wabunifu wa kutengeneza programu mbalimbali za kuinua uchumi na
kuachakulalamikia na kuungana na makundi mengine ambayo yanamtukana Rais Samia
Suluhu Hassan kwenye mitandao.
“Ninyi
wataalamu mnapaswa kuwa wabunifu tumieni elimu yenu kwa kuibua mipango yenye
tija ambayo itaibua mambo mbalimbali ya kufanya na kutengeneza ajira kwenye
maeneo yenu bada la ya kumtukana Rais ambaye anawapa mshahara jitokezeni bila
ya kuona aibu kuyasema mambo yote ya maendeleo anayofanya Rais wetu,”
alisisitiza Dendego.
Alisema katika
suala la kufanya kazi za kuwaletea maendeleo wananchi yupo tayari kufanya kazi
usiku na mchana na hata kulala ndani ya gari lakini ahakikishe kazi zinafanyika
pasipo kukwama.
Katika hatua
nyingine Dendegu alizitaka halmashauri za wilaya nazo zifanye utaratibu wa
kukopa fedha zinazotolewa na Serikali kwa ajiri ya kuwakopesha wananchi ili
wazitumie kuanzisha miradi kama ya uchimbaji wa madini na kazi zingine ikiwa ni
moja ya njia ya kuongeza kipato katika halmshauri hizo badala ya kuitegemea
Serikali pekee.
“Nikija kwenye
maeneo yenu ya kazi sitaki kusomewa taarifa kwenye karatasi nataka itoke katika
kiganja chako cha mkono Rais akija hapa akiuliza nina watu wangapi mkoani hapa mnataka nimjibu
kuwa sijui, mifugo mingapi sijui , kila nitakacho ulizwa nijibu sijui nitakuwa
mkuu wa mkoa wa namna gani, mimi naweza nataka na nyinyi muweze na mtume salamu
kwa wengine waambieni moto umewaka,” alisema Dendego.
Kwa heshima
kubwa aliyompa Rais Samia Suluhu Hassan kuna watanzania zaidi ya milioni 60 kati
ya hao 26 wameteuliwa kuwa wakuu wa mikoa nayeye akiwepo hivyo hawezi kulala
usingizi atafanya kazi katika mazingira yoyole yale hata kulala ndani ya gari ili kazi
hiyo ifanyike kwa ufanisi na ubora.
Dendego kwake
suala la elimu alisema ni la kufa na kupona atalisimamia na kuhakikisha watoto wanapata
elimu kwani wakiachwa mitaani ndio hao wanaoenda kuishambulia serikali mitandaaoni.
Katibu Tawala
wa Mkoa wa Singida, Dkt. Fatma Mganga akichangia kuhusu ukamalishaji wa miradi
kwa wakati alitoa ushauri kwa halmashauri hizo kuwatumia mafundi na wahandisi waliopo maeneo inapotekelezwa miradi hiyo kwa kuwapa mikataba ya muda mfupi ili utaalamu wao utumike kuongeza
kasi ya kazi huku akiwataka wakurugenzi na watu wa idara ya manunuzi kuzunguka
madukani kuona bei za vifaa vinavyouzwa na vile vifaa vitakavyouzwa kwa bei ya
chini vinunuliwe badala kuachia mwanya wa kununua vifaa hivyo kwa bei ya juu.
Kwa upande
wake Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama, James Mkwega naye aliungana na viongozi
wengine ambao wametaka ufungwaji wa hoja zote za CAG ndani ya muda uliopangwa
ambapo alitumia kikao hicho kumshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha
nyingi za utekelezaji wa miradi mbalimbali wilayani humo ukiwepo wa Kituo cha
Afya cha Kata ya Gumanga.
Mkuu wa Wilaya
ya Mkalama Moses Machali alisema wana Mkalama wasibweteke kwa ushindi huo
waliopata wa kuwa na hoja chache za CAG kuliko halmashauri zingine ambapo
aliwataka kuzipunguza hoja hizo ikiwezekana ziishe kabisa kwani huenda kuna
halmashauri zingine hazi hoja hizo kabisa.
Naye Katibu wa
Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Mkalama, Agness Chuwa akitoa salamu za
chama katika kikao hicho cha baraza la madiwani naye aliungana na viongozi
wengine kuhakikisha hoja zote za CAG zinafungwa kwa wakati uliopangwa na wakati
wa utekelezaji wa miradi hiyo ifanyike kwa thamani ya fedha zilizotolewa na
Serikali.
Mkaguzi Mkuu
Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) Mkoa wa Singida,
Othman Jumbe aliwaeleza madiwani hao kuwa miradi hiyo inapokamilishwa
ikamilishwe si kwa kuangalia majengo yalivyo bali majengo hayo yawe na ubora na
thamani ya fedha zilizotolewa.
Akizungumzia
ukamilishaji wa miradi hiyo yenye hoja alisema ni jukumu la halmashauri husika
ya kuona namna ya kutafuta hela za kuimalizia na vingine miradi hiyo itaingizwa
kwenye hoja ya mwaka mwingine wa fedha jambo ambalo sio zuri.
Katika baraza hilo madiwani walipata fursa ya kuchangia hoja mbalimbali huku hoja iliyohusu matengezo ya magari ambayo yamechukua muda mrefu tangu yaharibike yakiwa kwenye gereji mbalimbali ikichukua nafasi kubwa kujadiliwa.
Diwani wa Kata ya Miganga, Omari Mpinga Nzia akichangia jambo kwenye kikao hicho.
Diwani wa Viti Maalum, Zainabu Kihara kutoka Kata ya Kinyagiri kulia na Diwani mwenzake Wankembeta Timotheo kutoka Kata ya Ibaga wakiwa kwenye kikao hicho.
Diwani wa Kata ya Ilunda, Mohamed Imbele akichangia wakati wa kujibu hoja.








No comments:
Post a Comment