SERIKALI KUSHIRIKIANA NA KAMPUNI KUTOKA JORDAN KUPATA MAJI ARDHINI - SINGIDANIBLOG

Habari za Hivi Punde

Post Top Ad

Monday, 29 July 2024

SERIKALI KUSHIRIKIANA NA KAMPUNI KUTOKA JORDAN KUPATA MAJI ARDHINI

Waziri wa Maji, Jumaa Aweso (kushoto) akipata maelezo kutoka kwa Mkurugenzi wa Kampuni ya Al- Firdaws Investment Co Ltd kutoka nchini Jordan, Ahmed Al Khatib (katikati mwenye shati jeupe) jinsi kifaa cha kisasa cha kutafutia maji ardhini kinavyofanya kazi wakati wa ziara yake ya siku moja ya kikazi alipotembelea kwenye eneo la uwekezaji la kampuni hiyo lililopo Kijiji cha Choda Wilaya ya Ikungi mkoani Singida, Julai 28, 2024.

........................... 

Na Dotto Mwaibale, Singida 

SERIKALI kushirikiana na Kampuni ya Al- Firdaws Investment Co Ltd kutoka nchini Jordan kwa ajili ya kupata maji kutoka ardhini yatakayotumika kwa shughuli mbalimbali za maendeleo nchini. 

Hayo yamebainishwa na Waziri wa Maji, Jumaa Aweso wakati akizungumza na wataalamu kutoka Sekta ya maji alipokuwa katika ziara ya kikazi ya siku moja katika Kijiji cha Choda kilichopo wilayani Ikungi mkoani Singida baada ya kupata maelezo ya upatikanaji wa maji kutoka ardhini kwa kutumia teknolojia ya kisasa inayofanywa na kampuni hiyo.  

Waziri Aweso alifika katika kijijini hicho kuona uanzishwaji wa shamba la umwagiliaji linalomilikiwa na kampuni hiyo walilopatiwa na Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi. 

Aidha, Aweso alisema kuwa changamoto kubwa tuliyonayo hapa nchini ambayo inasababisha kukosekana kwa maji ni kuwa na teknolojia duni hivyo kupitia kampuni hiyo chini ya mwekezaji huyo wanakwenda kufanya mapinduzi makubwa ya upatikana wa maji na kupata suluhisho. 

" Kuwa na watu wa aina ya Firdaws  ni neema kubwa” alisema Aweso. 

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa  Wizara hiyo, Mwajuma Waziri alisema kuwa Tanzania ina changamoto nyingi za maji hivyo ni vizuri kuiga mafanikio makubwa yaliyopatikana nchini Jordan kwa kutumia teknolojia hiyo mpya ya upatikanaji wa maji kutoka ardhini. 

Mkurugenzi wa Kampuni ya Al-firdaws, Ahmed Al Khatib alisema wao wana uzoefu wa kutosha na kuwa kama wataaminiwa na kupewa kazi hiyo wataona matunda yatokanayo na kazi hiyo kutokana na huduma bora watakayoipata kutoka kwa mwekezaji huyo.  

Akimzungumzia Mwekezaji huyo Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi, Justice Kijazi alisema kuwa tayari halmashauri hiyo imempatia  Mwekezaji huyo  ekari 11,700. 

Katibu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Ikungi, Shabani Muhimbani alisema uwekezaji mkubwa unaofanywa na kampuni hiyo ni utekelezaji wa ilani ya chama hicho chini ya Rais Samia Suluhu Hassan na kuwa una kwenda kutoa ajira kwa makundi mbalimbali hasa vijana.

Waziri wa Maji, Jumaa Aweso, akipeana mkono na Mkurugenzi wa Kampuni ya Al- Firdaws Investment Co Ltd kutoka nchini Jordan, Ahmed Al Khatib baada ya kupatiwa taarifa ya mradi huo wa kutafuta maji ardhini.
Mkurugenzi wa Rasilimali za Maji, Dkt. George Lugomela, akizungumza wakati wa ziara hiyo.
 Katibu Mkuu Wizara ya Maji, Mwajuma Waziri akichangia jambo kwenye wizara hiyo.
 Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi, Justice Kijazi akimueleza jambo Waziri wa Maji Jumaa Aweso wakati wa ziara hiyo. Kulia ni Katibu Mkuu Wizara ya Maji, Mwajuma Waziri.
Kaimu Katibu Tawala Wilaya ya Ikungi, Joseph Ghati Kibasa, akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya ya Ikungi, wakati akitoa salamu za mkuu wa wilaya kwa Waziri wa Maji Jumaa Aweso.
Muonekano wa sehemu ya shamba hilo la ekari 11,700 alilopewa muwekezaji huyo na Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi kwa ajili ya mradi huo.
Baadhi ya vifaa na mabomba vikiwa nje ya ofisi za Kampuni ya ya Al- Firdaws Investment Co Ltd kutoka nchini Jordan iliyopo Kijiji cha Choda Wilaya ya Ikungi.
Matrekta ya kazi yakiwa tayari kwa kazi.
 

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad