BIDII ya kazi na uzalendo inatajwa
kuwa ni moja ya nguzo inayomfanya mtu kusonga mbele katika hatua ya maendeleo
yake binafsi na Taifa kwa ujumla hali ambayo tunaiona katika baadhi ya mataifa
makubwa kama China ilivyofanya mapinduzi makubwa ya kiuchumi kutokana na watu
wake kuwa wazalendo na kufanya kazi kwa bidii.
Ili kurahisisha utendaji wa kazi,
Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeunda Taasisi mbalimbali na
kuweka wasimamizi lengo likiwa ni kuharakisha maendeleo ya nchi hususani
yanayowahusu wananchi katika sekta mbalimbali kama vile elimu, ardhi, maji,
umeme, afya na nyinginezo.
Wakuu wa taasisi hizo wengi wao
wamekuwa wakipatikana kutokana na elimu zao, uzoefu wa kazi ambazo
wamewahi kuzifanya aidha wakiwa chini ya viongozi wengine au kwa kuteuliwa moja
kwa moja na mamlaka za juu.
Leo katika safu hii napenda
kumzungumzia Dkt. Erasmus Kipesha, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Elimu
Tanzania (TEA). Binafsi namuita mzalendo ambaye anawiwa kuipeleka mbele
elimu ya Tanzania kutokana na maboresho makubwa anayoyafanya kupitia
mamlaka hiyo iliyoanzishwa kwa Sheria ya Bunge Na. 8 ya Mfuko wa Elimu ya
mwaka 2001 kifungu cha 5(1) ikiwa na jukumu la kusimamia na kuratibu Mfuko
wa Elimu wa Taifa. TEA ni taasisi ya Serikali chini ya Wizara ya Elimu, Sayansi
na Teknolojia.
Niseme tu kuwa Dkt. Kipesha na timu
yake wapo kazini na wamejipanga vilivyo kuhakikisha wana msaidia Mhe. Rais Dkt.
Samia Suluhu Hassan kuboresha miundombinu ya elimu nchini kupitia Mfuko wa
Elimu wa Taifa.
Dkt.Kipesha si mkuu wa taasisi hiyo
aliyetoka nje bali alikuwa ndani ya taasisi hiyo akihudumu kama Mkurugenzi wa
Huduma za Taasisi hivyo anaijua vizuri na ndio maana kuteuliwa kwake kuwa
Mkurugenzi imekuwa rahisi kwake kuwa na mikakati endelevu na kuchukua hatua za
haraka kuitekeleza ili kuinua ubora wa elimu sambamba na uboreshaji wa
miundombinu.
Kila mwenye macho anaweza kuwa
shuhuda wa haya ninayosema hivi sasa kupitia TEA chini ya Serikali inayoongozwa
na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan tunaona maboresha makubwa ya miundombinu ya
shule zetu hapa nchini kuanzia madarasa, matundu ya vyoo, wingi wa maabara za
sayansi, mabweni ya wasichana na wavulana, nyumba za walimu hali ambayo
imeongeza ufaulu wa wanafunzi kwenye shule nufaika.
Kazi hii kubwa inayofanywa na TEA
chini ya Dkt. Kipesha na timu yake inapaswa kuungwa mkono na kila mpenda
maendeleo hasa katika sekta ya elimu ambayo ni msingi mkubwa wa maisha ya
mwanadamu. Kutokana na maboresho haya
makubwa yanayofanyika kwenye miundombinu ya elimu, ni vigumu kutofautisha
mabweni ya wanafunzi wa shule za watu binafsi na Serikali. Hakika kazi kubwa
imefanyika na inaendelea kufanyika. Pongezi nyingi kwa TEA na shukrani nyingi
kwa Rais Samia kwa kutoa fedha za miradi hii.
Tabia ya Dkt. Kipesha ya kukutana na
watendaji wenzake na kupokea maoni yao na kuyafanyia kazi ni moja ya jambo
kubwa linalochochea ufanisi wa kazi na utekelezaji wa miradi mbalimbali ya
elimu.
Kufanya ziara za kwenda kushiriki maadhimisho mbalimbali kama yale ya Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu yaliyofanyika Mei 26, 2024 katika viwanja vya Shule ya Sekondari Popatlal Jijini Tanga yamekuwa yakichochea utendaji kazi wa mamlaka hiyo na wananchi kujua shughuli zinazofanywa na TEA.
Kutoa nafasi kwa maafisa wa TEA
kwenda kushiriki shughuli mbalimbali za nje kama walivyo kwenda baadhi yao
kwenye Maadhimisho ya Kitaifa ya Juma la Elimu ya Watu Wazima yaliyofanyika
Viwanja vya Chipukizi mkoani Tabora pia ina leta afya ya uwajibikaji kwa
maofisa wa mamlaka hiyo.
Kushiriki kwake katika mafunzo elekezi kwa Watendaji Wakuu wa Taasisi za umma ambayo yalifanyika Oktoba 7, 2024 katika Chuo cha Uongozi cha Mwalimu Nyerere Kibaha, mkoani Pwani yana muongezea uelewa zaidi na usimamizi mzuri wa taasisi yake na kutekeleza kwa umahiri majukumu yake kwa kuzingatia Sheria, Kanuni na Miongozo ya Serikali.
Dkt. Kipesha katika kujua
umuhimu wa vyombo vya habari kupitia uratibu wa Ofisi ya Msajili wa
Hazina alikutana na wajumbe wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF)
kwa lengo la kuelezea utekelezaji wa majukumu na mipango ya TEA katika kutoa
huduma kwa umma kupitia ufadhili wa miundombinu ya elimu.
Akizugumza katika mkutano huo, Dkt. Kipesha alisema moja ya majukumu ya TEA ni
utafutaji rasilimali kwa ajili ya Mfuko wa Elimu wa Taifa na kwamba njia
mojawapo inayotumika katika jitihada hizo ni uandaaji wa maandiko ya miradi
yatakayowezesha kupata fedha kutoka taasisi za ndani na nje ya nchi ili
kusaidia uendelezaji wa miundombinu ya elimu.
Katika kipindi cha miaka mitano kuanzia mwaka 2019/2020 hadi 2022/2023 jumla ya
michango na ufadhili wa Sh.1.4 ilikusanywa na TEA kutoka kwa wadau mbali mbali
ikiwa ni pamoja na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Mamlaka ya Hifadhi za
Taifa (TANAPA), Taasisi ya Asilia Giving inayojihusisha na shuguli za utalii
Jijini Arusha pamoja na Taasisi ya Flaviana Matata.
Tunaiona kazi kubwa inayofanywa na TEA chini ya Dkt. Kipesha na timu yake kwenye sekta ya elimu na kuthibitisha haya, Oktoba 21 na 22, 2024 Menejimenti ya TEA chini yake imekutana kwa siku mbili kwa lengo la kutathmini utekelezaji wa majukumu yake kama yalivyoainishwa kwenye Mpango Mkakati wa Mamlaka hiyo wa miaka mitano (2021/2022 – 2025/2026). Tathmini inayolenga kubaini maeneo ya kuboresha na kuweka mikakati madhubuti ya kuimarisha ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yake hasa utafutaji wa rasilimali fedha kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya elimu na kuzifikia shule nyingi zaidi.
Katika kikao hicho cha kufanya tathmini, Dkt. Kipesha, alisisitiza umuhimu wa kuhakikisha majukumu ya TEA yanaenda sanjari na utekelezaji wa Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014, ambayo inalenga kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia kuwa bora, salama, na endelevu katika shule na vyuo.
Nitakuwa mchoyo wa fadhira kama
sitamtaja aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka hiyo Bi. Bahati Geuzye ambaye
ameaminiwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan baada ya kuona kazi kubwa
aliyoifanya akiwa TEA na kumteua kwenda kuwa Katibu Tawala wa Mkoa wa Mtwara
ambaye kwa kiasi kikubwa amechangia maboresho makubwa katika sekta ya elimu
hasa miundombinu na kuacha alama katika taasisi hiyo.
Bi. Geuzye akiwa Mkurugenzi Mkuu wa
TEA, Dkt. Kipesha alikuwa Mkurugenzi wa Huduma za Taasisi ambapo chini ya
uongozi wake mwaka jana, TEA ilipanga kutumia Sh. Bilioni 8 kwa ajili
ya kufadhili miradi ya kuboresha miundombinu ya elimu Nchini.
TEA ambayo ni miongoni mwa Taasisi za
muungano kupitia Mfuko wa Elimu imetoa ufadhili wa Sh. Milioni 500 kwa ajili ya
mradi wa ukarabati wa miundombinu pamoja na ununuzi wa vifaa vya kufuindishia
na kujifunzia katika vyuo viwili vya elimu ya juu vilivyopo Tanzania Zanzibar.
Katika ufadhili huoTaasisi ya Karume
ya Sayansi na Teknolojia (KIST) ilipokea ufadhili wa Sh. Milioni 200 na Chuo
Kikuu cha Zanzibar (SUZA) kampasi ya Benjamin Mkapa iliyopo Pemba ilipokea
ufadhili wa Sh. Milioni 300, ufadhili huo umenufaisha wanafunzi 700 katika vyuo
hivyo viwili.
Katika kuunga mkono serikali kuhamia
Dodoma, TEA kupitia Mfuko wa Elimu ilifadhili miradi mikubwa miwili ikiwa ni
pamoja na ujenzi wa shule mpya ya msingi inayofundisha kwa lugha ya kiingereza
ya Msangalele kwa thamani ya Sh. Milioni 750 katika mwaka wa fedha 2021/2022.
Aidha mfuko ulifadhili ujenzi na ukarabati
wa miundombinu ya elimu katika shule nne za msingi za Jijini Dodoma ambazo ni
Kisasa, Kizota, Medelin A, Mlimwa C kwa thamani ya Sh bilioni 1.9
Hayo ni baadhi ya mafanikio makubwa
ya TEA kupitia Mfuko wa Elimu wa Taifa lakini makubwa zaidi ya hayo yana kuja
baada ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan hivi karibuni kumteua Dkt. Leonard
Akwilapo kuwa Mwenyekiti Bodi ya TEA.
Dkt. Akwilapo tuna mjua kuwa ni
mchapakazi, mbunifu na mpenda maendeleo. Tunaamini TEA sasa ina kwenda kufanya
vizuri zaidi kwa usimamizi wa Mwenyekiti huyo wa Bodi na wajumbe ushirikiano wa
Menejimenti na watumishi wote kwa ujumla.
Mafanikio na kazi yote hii kubwa inatekelezwa na TEA chini ya Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambacho ni Chama Tawala.
Imeandaliwa na Dotto Mwaibale, (0754-36 2990)
Shule ya Serikali ya Mchepuo wa Kiingereza Msangalalee iliyojengwa na Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) kupitia Mfuko wa Elimu wa Taifa Jijini Dodoma.
Muonekano wa vyumba vya madarasa Shule ya Msingi Urughu wilayani Iramba mkoani Singida vilivyojengwa na Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) kupitia Mfuko wa Elimu wa Taifa.
Matundu 24 ya vyoo Shule ya Msingi Umwe iliyopo Wilayani Rufiji mkoani Pwani yaliyojengwa na Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) kupitia Mfuko wa Elimu wa Taifa.
Maabara ya Sayansi iliyojengwa na Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) kupitia Mfuko wa Elimu wa Taifa Shule ya Sekondari William Lukuvi iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Iringa mkoani Iringa.
Bweni lililojengwa na Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) kupitia Mfuko wa Elimu wa Taifa Shule ya Sekondari Mbomai iliyopo halmashauri ya Wilaya ya Rombo mkoani Kilimanjaro.
Muonekano wa bweni lililojengwa na Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) kupitia Mfuko wa Elimu wa Taifa Shule ya Sekondari Mbomai iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Rombo mkoani Kilimanjaro.













No comments:
Post a Comment