Mwenyekiti wa Jumuhiya ya Maridhiano na Amani Tanzania ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati ya Siasa wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Kata ya Mtoni, Sikujua Mziray, akizungumza na waandishi wa habari Aprili 7, 2025 (hawapo pichani) kuhusu madai ya Wananchi wa Kijiji cha Kazole Kusini Mji Mpya Kata ya Vikindu Wilaya ya Mkuranga Mkoa wa Pwani kupigwa, kujeruhiwa na kubambikiwa kesi na anayesaiwa mwekezaji.
...........................................
Na Dotto Mwaibale, Mkuranga
BAADHI ya Wananchi wa Kijiji cha Kazole Kusini Mji
Mpya Kata ya Vikindu Wilaya ya Mkuranga Mkoa wa Pwani wanalalamikia kupigwa, kujeruhiwa
na kubambikiwa kesi huku wenzao wakitumikia vifungo gerezani kwa madai ya
kung’oa bikoni kwenye shamba la mtu anayedaiwa kuwa ni Mwekezaji.
Wakizungumza na waandishi wa habari Aprili 7, 2025 wananchi
hao wamedai kuwa waliruhusiwa kuendeleza shamba hilo kwa shughuli za kilimo
baada ya Rais wa Awamu ya tano Hayati John Pombe Magufuli kudaiwa kufuta hati
ya umiliki wa shamba hilo kufuatia aliyekuwa mwekezaji kushindwa kuliendeleza tangu apewe na kijiji
hicho mwaka 1988 ili kuanzisha kiwanda badala yake linadaiwa kuwa na mifugo isiyozidi 100 wakiwemo mbuzi, ng’ombe
na kondoo.
Muwekezaji aliyefutiwa hati hiyo ametajwa kuwa ni
Antinyazi Gulamali (maarufu kama Hamidu Barani) ambaye alikuwa akimiliki hekta 1750
ambazo hajaziendeleza hadi leo.
Hamidu ametajwa pia kumiliki Kiwanda cha Soap and
Allied Industry kilichopo jijini Dar es Salaam na kuwa tangu amiliki eneo hilo
wananchi hawakuwahi kumuona hadi siku
aliyohudhuria mkutano ulioitishwa na aliyekuwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na
Maendeleo ya Makazi, Mhe.William Lukuvi lakini zaidi ya hapo ni kuendelea kuwepo
na matukio ya kukamatwa na walinzi wa
shamba hilo huku viongozi wa Mkoa wa Pwani wakidaiwa kutozungumza chochote
kuhusu jambo hilo.
Wananchi hao wamedai kuwa kesi kubwa wanayofunguliwa
ni kuingia kwenye shamba hilo na kutoa bikoni na siyo ya kuliendeleza baada ya
mwekezaji huyo kuondolewa umiliki wake.
Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari
ambao walifika katika eneo hilo kusikiliza malalamiko ya wananchi hao, mkazi wa Kijiji hicho Omari
Kilumbi alisema wanateseka kutokana na wanaodaiwa kuwa ni walinzi wa shamba
hilo kuharibu mazao yao waliyopanda (mihogo na mboga mboga) kwa kuyafyeka na
kulisha mifugo jambo lililowafanya wakose chakula (futari) wakati wa Mwezi
Mtukufu wa Ramadhani.
“ Shamba hili limetuletea misukosuko mingi mno ikiwemo
ya kupigwa na kujeruhiwa na walinzi hawa, kufyekewa mazao yetu na kufunguliwa
kesi ya kung’oa bikoni halali na kuwekwa
haramu wakati siyo kweli kwani zinazoondolewa zipo kwenye shamba hilo zaidi ya
miaka mitano ,” alisema Kilumbi.
Kilumbi alisema kwa nyakati tofauti wamewahi kutumikia
vifungo gerezani na kuwataja baadhi ya walio jeruhiwa na walinzi hao baada ya
kupigwa kuwa ni Mzee Omari Mtibila,
Eliud Ibrahim na Esal Omary.
Aliwataja wanaotumikia kifungo gerezani kuwa ni
Aminiel Mshana, Ramadhani Gogi, Haruni Makanjila na Beatrice Kivamba aliyekuwa
mjamzito ambaye anatumikia kifungo cha nje baada ya kuwa na mtoto mchanga aliyemzaa
wakati akiendelea kutumikia kifungo hicho.
Kikongwe Mwanahamisi Binti Hassan (80) anasema
anasikitika kwa vitendo ambavyo
wanafanyiwa na walinzi wa kampuni hiyo hasa cha kuharibu mazao yao na kubomoa
vibanda vyao walivyo vijenga katika shamba hilo na kueleza kuwa kulipata shamba
hilo hawakubeti ambapo ana muomba Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.
Samia Suluhu Hassan awasaidie.
Kwa upande wake Bibi Nuru Mbonde (64) alisema hali
siyo shwari katika eneo hilo wanaharibiwa mazao yao waliyolima na kubomolewa
nyumba zao na kibaya zaidi walinzi hao walichana bendera ya Chama Cha Mapinduzi
(CCM) iliyosimikwa katika masikani ya chama hicho waliyoianzisha ndani ya
shamba hilo.
“Mama Samia Rais wetu wanawake wenzako na uzee wetu
huu tunanyanyaswa utafikiri Tanzania siyo nchi yetu tunaomba tusaidie tunapita
katika wakati mgumu kwani polisi wanatukamata na kutufungulia kesi na kibaya
zaidi wanaokamatwa ni wale wanaotoa taarifa za kunyanyaswa kwetu tukimbilie
wapi sisi jameni ? ” alisema bibi huyo huku akiangua kilio.
Mwenyekiti wa Jumuhiya ya Maridhiano na Amani Tanzania
ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati ya Siasa
wa CCM Kata ya Mtoni, Sikujua Mziray alisema chokochoko hizo zilianza
baada ya Magufuli kufuta hati hiyo
aliposimamishwa na wananchi Mkuranga na kuzungumza nao alipokuwa akitokea
kwenye mazishi ya Rais wa Awamu ya Tatu, Hayati Benjamin Mkapa Lupaso mkoani
Mtwara.
Alisema mara baada ya Magufuli kueleza nia ya kufuta hati
ya umiliki wa shamba hilo, William Lukuvi alifika katika kijiji hicho na
kuwaambia wananchi wajiunge katika vikundi vya watu watano ili waanze kufanya
kilimo kwenye maeneo ya mabondeni wakati
wakisubiri kurasimishiwa rasmi.
“Hii ni neema ya Wilaya ya Mkuranga na vitongoji vyake
ambavyo ni vinufaika wa eneo hilo,” walimnukuu Lukuvi alivyo sema.
Alisema baada ya hapo haukufanyika utaratibu wowote wa
Serikali Mkoa wa Pwani kuhusu maagizo yaliyotolewa na Lukuvi ambapo wananchi
waliendelea kulitumia shamba hilo kwa kilimo na mwaka jana mwishoni ndipo
walipoanza kupata madhira hayo.
Alisema jambo la kushangaza ni pale wanapoona shamba
hilo likipimwa viwanja vidogo vidogo na anayedaiwa kuwa mwekezaji ambavyo
vinadaiwa vitauzwa kwa madalali wakati hati ya umiliki ilisitishwa.
“Tumekuwa katika sintofahamu kwa mambo yanayofanyika
katika shamba hili kwani hati ya umiliki
ilifutwa inakuwaje tena aanze kupima viwanja kwa lengo la kuviuza na
hakuna kiongozi yeyote aliyefika kuzungumza na wananchi kuhusu jambo hilo huyu
ni mwekezaji kweli au mlanguzi wa ardhi yetu ? ,” alihoji Mziray.
Mziray alisema mara nyingi kila wanapohoji kuhusu
shamba hilo viongozi wa wilaya hiyo wamedaiwa kutoa madai ya kuwepo kesi
mahakama kuu wakidai ilifunguliwa na wananchi dhidi ya mwekezaji huyo kesi
ambayo hata namba yake na tarehe iliyofunguliwa hawaitaji.
Alisema kesi iliyopo mahakama kuu ni ile iliyofunguliwa
na Kampuni ya NCG Chemical Industries
Limited Company dhidi ya wananchi ambayo inasimamiwa na William Mlacha Meneja
wa kampuni hiyo huku kwa upande wa wananchi ikisimamiwa na Mwanasheria
waliyemtaja kwa jina la Alex Enock na wala
haihusu shamba hilo.
“ Sisi hatujawahi kuwa na kesi yoyote na mwekezaji huyu
zaidi ya ile iliyofunguliwa na kampuni ya Chemical Industries Limited Company shauri
namba 209/ 2022 dhidi ya Amiri Malombola na wenzake 60 iliyokuwa mbele ya Jaji
Mhina ambayo itupiliwa mbali na Machi
22, 2024 walifungua kesi nyingine namba 55/130
ya ardhi namba 28132 iliyopo mbele ya Jaji Msafiri ambayo imepangwa
kusikilizwa Mei 15, 2025 na kama kulikuwepo kesi iliyofunguliwa na mwekezaji
huyo labda ilikuwa baina yake dhidi ya Serikali na siyo wananchi wa hapa ,”
alisema Mziray.
Mziray alisema
kisiasa jambo hilo haliposawa kwani lisipofanyiwa kazi kwa wakati upo uwezekano
mkubwa wa kuwafanya wananchi kuwa na hasira na
kupunguza kura za Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan katika uchaguzi mkuu utakaofanyika
mwezi oktoba mwaka huu ukizingatia kuwa katika kijiji hicho kuna wananchi zaidi
ya 600 kitu ambacho akitakuwa siyo
kizuri kumnyima kura Rais Samia aliye
wafanyia maendeleo makubwa watanzania kwa sababu tu ya baadhi ya watu kutaka
kupoka ardhi hiyo kiujanja.
Afisa Usalama Mkuu wa Kampuni inayodaiwa kusimamia
shamba hilo, Joseph Mwenga aliyefika
kwenye eneo ambalo waandishi wa habari walikuwa wakipata maelezo kutoka kwa
wananchi kuhusu jambo hilo huku akiwa ameongozana na walinzi wa jamii ya kimasai
waliokuwa wamebeba silaha za jadi alisema kwa kifupi kuwa wao wapo kisheria
katika shamba hilo.
Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhe. Abubakar Kunenge hakuweza
kupatikana ili kuzungumzia suala hilo baada ya waandishi wa habari kufika
ofisini kwake na kuambiwa na katibu wake kuwa alikuwa kwenye mbio za mwenge.
Hata hivyo Katibu Tawala wa Wilaya ya Mkuranga Omary
Mwanga akizungumza kwa niaba ya mkuu wa wilaya hiyo alikiri kulifahamu suala hilo
na kueleza kuwa ni la muda wa miaka mitano sasa na kuwa wananchi hao walimfungulia
kesi mwekezaji huyo ambaye alishinda.
“Ninachokijua kama munachouliza kinahusu shamba la
Hamidu Barani, wananchi walifungua kesi dhidi ya mwekezaji huyo na mahakama kuu
ilimpa ushindi na sisi kama Serikali tunasimamia hukumu na maamuzi ya mahakama
na si vinginevyo,” alisema Mwanga.
Alisema umiliki wa hati ya ardhi inapositishwa
kunataratibu nyingi zinazofanywa ikiwa ni pamoja na kutangazwa kwenye gazeti la
Serikali.
Alisema hivi sasa mwekezaji huyo anaendelea na zoezi la kufufua mipaka ya shamba hilo kwa kuweka bikoni mpya.
Bibi Nuru Mbonde (64) akionesha bendera ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) inayodaiwa kuchanwa na walinzi wa kampuni inayolinda shamba la mwekezaji huyo.
Katibu wa wa Jumuhiya ya Maridhiano na Amani Tanzania, Mashauri Musa akichangia jambo kwenye mkutano huo.
Wakazi wa Kazole wakiwa kwenye mabaki ya matofali baada ya moja ya nyumba iliyokuwa kwenye shamba hilo kubomolewa na walinzi wa shamba hilo.
Mzee Ahmadi Mpate akizungumzia misukosuko wanayo kumbana nayo kwenye shamba hilo.
Wananchi wakionesha shamba la mihogo iliyoharibiwa na walinzi hao.
Wananchi wa Kijiji cha Kazole wakipita kwenye mpaka wa shamba hilo iliyowekwa hivi karibuni na mwekezaji huyo.
Bikoni mpya zikiwa kwenye shamba hilo tayari kwa kuwekwa.
Bikoni mpya zinazodaiwa kuwekwa na mwekezaji huyo katika shamba hilo baada ya kuzitoa za zamani

Muonekano wa bikoni za zamani zikiwa kwenye shamba hilo.
Wananchi wakiwa kwenye shamba hilo wakiwaonesha waandishi wa habari uharibifu wa mazao yao yanayodaiwa kuharibiwa na walinzi wa shamba hilo.Muonekano wa shamba la mihogo iliyolimwa na wananchi katika shamba hilo.













No comments:
Post a Comment