RC MALIMA ' AWAFUNDA ' JUKWAA LA USHIRIKA - SINGIDANIBLOG

Habari za Hivi Punde

Post Top Ad

Friday, 16 May 2025

RC MALIMA ' AWAFUNDA ' JUKWAA LA USHIRIKA

Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Adam Malima akiwa kwenye picha ya pamoja na viongozi, wadau  na wanachana wa Jukwaa hilo
.............................................

Na Godwin Myovela, Morogoro

MKUU wa Mkoa Adam Kighoma Malima amewataka wana-ushirika wote mkoani hapa kutambua kuwa ushirika sio msaada, bali ni nguvu ya pamoja ya kujisaidia – na njia bora ya kuondoa umaskini kwa heshima na mshikamano.

Alisema mafanikio ya vyama hivi hayawezi kupatikana bila uwajibikaji wa kweli ambao ndio msingi wa uaminifu. Bila uaminifu, hakuna ushirikiano wa kweli. Na bila ushirikiano, hakuna maendeleo.

Malima aliyasema hayo jana wakati akizindua Jukwaa la 5 la Maendeleo ya Ushirika mkoa wa Morogoro, lenye kauli mbiu isemayo ‘Ushirika hujenga ulimwengu ulio bora.’

Ushirika ni nguzo ya jamii jumuishi na chombo thabiti cha kujenga ulimwengu ulio bora kuanzia vijijini, sote tunaweza kuondoa kabisa umasikini kupitia ushirika sababu kila kitu kimerahisishwa, ikiwemo upatikanaji wa huduma za kifedha, masoko ya bidhaa, pembejeo za kilimo kwa bei nafuu,” alisema

Akihamasisha takribani vyama 226 vinavyounda jukwaa hilo mkoani hapa, mathalani, namna kilimo pekee kinavyoweza kuleta mabadiliko ya kiuchumi, alieleza namna ya kufunga mkanda na kukikabili kama biashara kubwa, kwa kutumia mbegu bora, zana za kisasa, umwagiliaji wa uhakika, na kuongeza thamani ya mazao kabla ya kuyauza.

Alisema kilimo huajiri watu wengi, hasa vijijini, huongeza kipato cha wakulima na kuchochea matumizi, huzalisha chakula cha ndani na kupunguza utegemezi wa uagizaji, pia mazao yake ni malighafi kwa viwanda, huongeza mauzo ya bidhaa ndani na nje ya nchi, zaidi mahitaji ya kilimo huchochea maendeleo ya barabara, teknolojia, fedha, masoko, na maghala.

Pia kwa wafugaji na wachakataji wa mazao ya mifugo, alihimiza kuacha tabia za uchakachuaji hasa maziwa ambayo baadhi ya wafugaji hudiriki kuweka sukari, maji na ugoro ili kuongeza uzito, jambo ambalo siyo tu ni udanganyifu, bali ni hatari kubwa kwa afya za walaji.

“Leo nimeshtuka kusikia kiwango cha utoaji maziwa kwa ngombe mmoja hapa ni chini ya lita 3! na pia kuna viashiria vya udanganyifu kwenye biashara hii. Natoa maelekezo kwa Mrajisi Msaidizi na maafisa ushirika wa maeneo husika kuunda mara moja Amcos 8 za wafugaji 4 kutoka Mvomero na 4 Kilosa ili tuanze nao kwenye mafunzo kama darasa la mfano kwa wengine, tuone tatizo liko wapi,” alisema Malima na kuongeza;

“Dhana ya mafunzo haya ni kuongeza viwango na ubora wa maziwa na mazao mengine ya mifugo kwa afya, uchumi, soko, usalama, na maendeleo ya sekta ya mifugo kwa ujumla.”

Zaidi alisisitiza umuhimu wa wanaushirika kufanya tathmini za kila mwaka ili kubaini mafanikio na changamoto, katika muktadha wa maboresho kwenye huduma na utendaji wa chama, uwajibikaji wa viongozi, kulinda maslahi, sanjari na kuweka msingi wa maendeleo endelevu.

“Ushirika una nidhamu yake, wale wanaoingia huku kwa lengo la kutupiga tuwakatae, na adui yetu mkubwa hapa ni ubadhirifu…tusikubali mana unapunguza mapato ya wanaushirika, unavunja imani ya wanachama, unadhoofisha huduma, na hatimaye unaweza kuua chama kabisa,” alisema RC Malima huku akionya kwamba ubadhirifu hautavumiliwa, wala kuachwa kuendelea ndani ya vyama vya ushirika bila kuchukuliwa hatua kali.


Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Adam Malima akiwa kwenye picha ya pamoja na viongozi, wadau  na wanachana wa Jukwaa hilo

Mkutano ukiendelea.

Mwenyekiti wa Jukwaa la Maendeleo ya Ushirika mkoa wa Morogoro Mwalimu Iddi Bilali akizungumza,

 Wanachama na wadau wa Jukwaa la Maendeleo ya Ushirika Morogoro wakifuatilia matukio mbalimbali kwenye mkutano wa 5 wa Jukwaa hilo.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad