MCHECHU MTAALAM WA FEDHA ANAYETAJWA KUWA NI HAZINA YA TAIFA - SINGIDANIBLOG

Habari za Hivi Punde

Post Top Ad

Thursday, 17 July 2025

MCHECHU MTAALAM WA FEDHA ANAYETAJWA KUWA NI HAZINA YA TAIFA

Msajili wa Hazina, Nehemia Mchechu, akizungumza na wahariri na waandishi (hawapo pichani), kutoka vyombo mbalimbali vya habari jijini Dar es Salaam.
........................................ 

UZALENDO ni hali ya mtu kuipenda, kuithamini na kujitoa kwa ajili ya nchi yake.

 Mzalendo wa kweli daima anaweka maslahi ya nchi mbele na ya kwake nyuma. 

Kwa maana hiyo mzalendo ni mtu yeyote mzawa na mwenye kuipenda na kujitoa mhanga na wakati mwingine ikibidi kufa kwa ajili ya nchi yake.

Uzalendo unabeba dhana pana ikianzia asili, utamaduni, lugha, siasa, historia na dhana kuu ikiwa ni utaifa.

Tanzania imekuwa na wazalendo wengi wanaolitumikia taifa vizuri na waliokwisha kulitumikia akiwemo Rais wetu wa kwanza Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Mzee Rashid Mfaume Kawawa, Edward Moringe Sokoine na Mwanasiasa maarufu Bibi Titi Mohamed na wengine wengi ambao waliipigania nchi na baadhi yao kupoteza maisha.

Miongoni mwa watanzania kuna wazalendo  wanaotumia elimu na  taaluma zao kulitumikia taifa kwa nguvu zao zote baada ya kuaminiwa na mamlaka za juu kushika nafasi za uongozi.

Leo napenda kumzungumzia Mtaalam wa masuala ya fedha na uongozi, Nehemia Kyando Mchechu Msajili wa Hazina ambaye ni mzalendo wa kweli kutokana na kazi kubwa anayolifanyia taifa.

Mchechu kabla ya kuteuliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kushika nafasi hiyo amefanya kazi katika maeneo mbalimbali, Mkuu wa Ukaguzi Chuo Kikuu cha Tumaini, Mkurugenzi wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC), Mjumbe wa Kamati za Baraza la Biashara la Taifa.

Maeneo mengine aliyofanya kazi ni Afisa Mtendaji Mkuu na Mkurugenzi Mtendaji wa CBA Bank, Standard Chartered Bank Tanzania Limited, Citibank na Barclays Bank Tanzania Limited, Mwenyekiti wa Serengeti Breweries Ltd, Mwenyekiti wa Amboni Sisal Properties Limited, Mwenyekiti wa Amboni Beach Limited, Mwasisi na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Rightway Schools, Mjumbe wa Bodi ya Benki ya KCB Tanzania Limited na Mwenyekiti wa East Africa Breweries Limited.

Mchechu akiwa Mkurugenzi Mkuu wa Benki ya Commercial Bank of Africa chini ya uongozi wake benki hiyo ilipata  mafanikio makubwa hapa nchini, na ni moja kati ya benki tano zilizoanza utaratibu wa kutoa mikopo ya nyumba kwa Watanzania.

Baada ya kufanya kazi katika maeneo hayo kwa mujibu wa kifungu Na. 18 (1) cha Sheria Na. 2 ya 1990, iliyounda Shirika la Nyumba la Taifa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi alimteua kuwa Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), uteuzi ulioanza rasmi Machi 1, 2010.

Mchechu alianza kazi kwa kasi kubwa akishirikiana na bodi na timu ya menejimenti ya shirika hilo huku akiwa amepewa jukumu la kulifanyia mageuzi makubwa shirika hilo.

Shirika hilo lilitakiwa liingie katika biashara kubwa ya kujenga nyumba katika mikoa yote na kuziuza kwa mikopo kwa watanzania wa kipato cha chini na kati, ambalo ndilo lengo kuu la shirika tangu lilipoanzishwa mara tu baada ya Tanganyika kupata Uhuru Desemba 9, 1961.

Kazi kubwa na nzuri na ya kizalendo ilifanyika chini ya uongozi wake ambapo karibu kila mkoa zilijengwa nyumba hizo kwa kiwango cha juu.

Mbali ya kujenga nyumba hizo nyumba za shirika hilo ambazo zinapangishwa alizifanyia ukarabati na kuzipaka rangi pamoja na kuzihakiki ili zitambulike kwani baadhi ya nyumba zilifanywa kama mali ya watu binafsi.

Hata hivyo, kitu kizuri hakikosi kuwa na changamoto au mti wenye matunda ndiyo unaopigwa mawe. Ndivyo. ilivyokuwa kwa Mchechu kwani licha ya kazi hiyo nzuri na kubwa aliyoifanya Rais wa Awamu ya Tano, Hayati Dkt. John Pombe Magufuli alimuondoa katika nafasi hiyo pengine kwa kupotoshwa na wasaidizi wake.

Baadaye Rais Samia alipoingia madarakani alimteua tena kuwa mkurugenzi wa shirika hilo la nyumba ambapo moto wake wa kazi ulikuwa mara dufu,  jambo lililoendelea kuonesha uzalendo wake kwa taifa.

Kwa kutambua uchapakazi na uzalendo wake kwa nchi, Rais Samia kwa mara nyingine alimteua kuwa Msajili wa Hazina nafasi ambayo anaendelea kuitendea haki kwa viwango vya juu.

Moja ya kazi yake kubwa anayoifanya ni utaratibu aliouanzisha wa taasisi zote zilizo chini ya Serikali kufanya mikutano na wahariri na waandishi wa habari kuelezea shughuli zinazozifanya ili wananchi wazijue jambo ambalo lilikuwa halifanyiki hapo awali.

Msajili wa Hazina, Nehemia Kyando Mchechu.

Mchechu hakika ni hazina, mzalendo na tunu ya watanzania kutokana na utumishi wake uliotukuka na ni miongoni wa vijana waliandaliwa vizuri kwa ajili ya kulitumikia taifa.

Lengo la kuyaandika  haya yote ni kutaka kufanya mizania ya uongozi katika utendaji wa utumishi wa umma na Serikali na namna viongozi wanavyotakiwa kuwa.

Ndhairi kuwa taifa likiwa na viongozi wa aina ya Mchechu litapiga hatua kubwa kiutendaji.

MIifano ipo mingi kama nilivyoitaja hapo juu, hivyo ni jukumu la Serikali sasa kuwaandaa vijana vyuoni na maeneo mengine ili waweze kufanya kazi kwa uzalendo na kuzingatia maadili ya utumishi wa umma.

Kumuandika Msechu ni mfano tu wa viongozi wanaopaswa kufanya mambo katika kulitumikia taifa kwa misingi ya uadilifu na moyo.

Lengo lingine ni kutaka kuonesha jinsi viongozi wanavyopaswa kuwa baada ya kuandaliwa na kuwa na utendaji bora kama huo.

Licha ya kuwa ni asili na uwezo wa mtu mmoja mmoja lakini Serikali inaweza kutengeneza viongozi wa namna ya Mchechu  hata katika uongozi wa kisiasa.

Nchi za wenzetu zilizoendelea zina utaratibu wa kuwaandaa viongozi na Serikali yetu ikifanya hivyo tutaweza kuwapata viongozi watakaokuwa mahiri sehemu zao za kazi.

Utendaji mzuri wa Mchechu kila alipofanya kazi ndio uliomsukuma Mhe. Rais Samia kumpa nafasi hiyo ili kulisukuma mbele taifa kimaendeleo na watu wa aina ya Mchechu sio waliibuka tu bali walitengenezwa kuanzia vyuoni na kuwa na uwezo huo mkubwa.

Mbegu ya watu kama akina Mchechu ambaye alipata nafasi ya kuwa Mtendaji Mkuu mwenye umri mdogo katika ukanda wa Afrika Mashariki inatakiwa kuoteshwa ili tuwapate wengi zaidi.

Baadhi ya wachambuzi wa mambo wanamtafsiri Mchechu kama hazina ya taifa kwa alichokifanya katika maeneo yote aliyopita, ni mambo yanayopaswa kuigwa hivyo kuna kila sababu ya kuonekana ni mtu muhimu kwa taifa.

Wahariri na Waandishi wa habari Waandamizi walipohojiwa na mwandishi wa makala haya walimzungumzia Mchechu kama ifuatavyo;

Jabir Idrisa, Mhariri Mwandamizi wa Gazeti la Mwanahalisi anasema Ofisi ya Msajili wa Hazina ipo tangu miaka mingi lakini watu wengi na wanahabari walikuwa hawajui majukumu yake kupitia Mchechu ofisi hiyo sasa inaonekana kama ni mpya.

“ Zamani tulikuwa hatujui kama Serikali imewekeza hisa kwenye makampuni binafsi, mambo ambayo hatukuyajua hapo awali,” alisema Idrisa.

Alisema kazi anayoifanya Mchechu ya kuzilea taasisi hizo  na kusema sasa magawio wayatoe hadharani na kuonesha ni shirika gani bora zaidi ni kitu kikubwa na anatekeleza hata matakwa ya katiba ya nchi ambayo inataka watu kushirikishwa katika usimamizi wa mamlaka ya Serikali.

Alisema sasa kumekuwa na uchangamfu wa taasisi hizo za Serikali kutambua mamlaka yake na wajibu wake wa kuchangia mfuko wa Serikali, basi ionekane kwamba kazi anayoifanya Mchechu ni faida kubwa kwa taifa.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akipokea mfano wa Hundi kama Gawio na Michango kutoka kwa Mashirika mbalimbali na Taasisi za Umma kwenye hafla iliyofanyika Ikulu Jijini Dar es Salaam.

...........................................

“Kutokana na utendaji wake mzuri wa kazi wa uwazi na kuboresha mifumo ya malipo na miamala ya kifedha kwa njia ya TEHAMA imeleta uchangamfu huku tukiona kwenye ripoti zake zikieleza kwa mfano, taasisi hii mwaka jana ilitoa gawio la Sh. Milioni 10 lakini mwaka uliofuata ikitoa gawio kubwa.

Hii inaonesha jinsi utendaji wake ulivyo chagiza ufanisi wa kazi kwenye taasisi hizo za umma.

Kwa upande wake Joyce Shebe Mhariri wa Clouds FM alisema uongozi ni karama, inawezekana muktadha ukachangia na namna ambavyo amepitia hatua zipi za uongozi au mikono ya nani.

“Tofauti ya Mchechu kila anapopita huwa anaacha alama ya tofauti, maana yake ni kwamba pengine ni mtu mwenye karama yake na wakati huo huo ni mtu anayependa kuyaona matokeo na amekuwa mtu wa uwazi sana ‘ transparent’, hivyo kusaidia kujulikana kwa kazi zake,” alisema Shebe.

Aliongeza kuwa Mchechu alitilia mkazo taasisi zote zilicho chini yake zifanye kazi zao ili watanzania wajue zinafanya nini, hiyo ni staili tofauti aliyokuja nayo.

Alisema ni muhimu kuwa na viongozi kama Mchechu ambao wanakuwa na shauku ya kuona matokeo ya nini kimefanyika na kwa kuzingatia sehemu ya kazi anapoongoza ni nyeti sana, hivyo taasisi za umma zinahitajika kuwajibika ipasavyo ili huduma za jamii ziweze kuimarika pia zipeleke gawio.

Alisema Msechu anatakiwa asimame imara na iwapo atakuwa legelege taasisi hizo zitafanya vibaya na mwisho wa siku  zitashindwa kupeleka gawio na jinsi anavyozisimamia kila taasisi ina jichekecha na kujiuliza tusipo peleka gawio itakuwaje.

Mwanahabari Hamisi Magendela anasema hatua hiyo ya Mchechu ya kuzitaka taasisi za umma kukutana na wahariri na waandishi wa habari imesaidia wananchi kuzifahamu kazi zinazofanywa na taasisi hizo.  

 Ofisi ya Msajili wa Hazina (OMH) imeanzishwa kupitia kifungu cha 3 cha Sheria ya Msajili wa Hazina (Mamlaka na Majukumu), Sura 370. Lengo kuu la kuanzishwa kwa OMH ni kusimamia uwekezaji na mali zingine za Serikali katika taasisi na mashirika ya umma, pamoja na kampuni ambazo Serikali ina umiliki wa hisa au kuna maslahi ya umma kwa niaba ya Rais na kwa ajili ya Serikali ya Jamhuri wa Muungano wa Tanzania. 

Mwaka 2014 kufuatia kufutwa kwa lililokuwa Shirika Hodhi la Mali za Mashirika ya Umma (CHC), OMH ilirithi majukumu yake. Kufuatia mabadiliko hayo, OMH ikaongezewa jukumu la kusimamia ubinafsishaji wa mali za umma, usimamizi na ufuatiliaji wa mashirika ya umma, ukusanyaji wa madeni ya Serikali yaliyorithiwa kutoka CHC, na urekebishaji na ufilisi wa mali zisizozalisha faida katika kampuni au mashirika yaliyobinafsishwa.

MAJUKUMU YA OFISI YA MSAJILI WA HAZINA 

Kwa mujibu wa Kifungu cha 10 cha Sheria ya Msajili wa Hazina Sura 370 kama ilivyorekebishwa, Ofisi imepewa majukumu yafuatayo: – 

1. Kufanya mapitio ya kudumu ama kuhakikisha kunafanyika mapitio ya kudumu ya shughuli na mwenendo wa watu ama Taasisi ambazo Msajili wa Hazina anamiliki mali ama ana maslahi kwa mujibu wa Sheria. 

2. Bila kuathiri Kifungu kidogo cha (1) kwa ujumla wake, Msajili wa Hazina anatakiwa: 

• Kutoa ushauri kwa Serikali kuhusu uanzishaji wa mashirika ya umma na kusimamia biashara au mali zilizowekezwa kwenye mashirika hayo;

•Kupitia utendaji wa kifedha wa mashirika kwa lengo la kushauri hatua za kuchukua katika kuunganisha, kuboresha muundo, kufuta au kuboresha utendaji wa mashirika na taasisi za umma;

•Kuweka malengo ya kifedha na vigezo vingine vya utendaji vitakavyotumiwa na mashirika na taasisi za umma;

•Kufanya tathmini mara kwa mara ili kupima utendaji wa bodi menejimenti za mashirika na kutoa mapendekezo kwa Serikali ya hatua za haraka au zilizopo za kuboresha usimamizi wa rasilimali;

•Kuidhinisha uwekezaji wa hisa unaofanywa na mashirika ya umma kwenye mashirika au kampuni nyingine;

•Kuwekeza au kuuza mali za mashirika ya umma;

•Kuhakikisha kuwa kila shirika la umma linaingia mkataba wa Utendaji na Msajili wa Hazina mara moja baada ya kuteuliwa kwa bodi ya wakurugenzi;

•Kufuatilia na kutathmini programu za mafunzo katika mashirika na taasisi za umma;

•Kuelekeza au kuidhinisha matumizi au marekebisho ya kanuni za fedha ili kuhakikisha usahihi wa taarifa za mapato na matumizi ya mashirika ya umma;

•Kuchambua na kuidhinisha miundo na mifumo ya mishahara, kanuni za utumishi na mpango wa motisha kwa mashirika na taasisi za umma;

•Kufuatilia misaada, ruzuku, fedha za mtaji, akiba au malimbikizo ya faida katika mashirika ya umma na kwenye uwekezaji mwingine wa umma;

•Kupendekeza au kuidhinisha mipango ya mwaka ya mashirika na taasisi za umma;

•Kufuatilia na kutathmini utendaji wa mashirika na taasisi za umma; na

•Kufanya ufuatiliaji na kuhakikisha gawio, michango na mikopo kutoka katika mashirika na taasisi za umma inalipwa kwa wakati.

Viongozi wa Serikali, Wakuu wa Mashirika na Taasisi za umma pamoja na Wageni mbalimbali wakiwa kwenye hafla ya kupokea Gawio na Michango kutoka kwa Mashirika na Taasisi za Umma

Makala haya yameandikwa na Dotto Mwaibale simu namba (0754-362990)

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad