Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Mstaafu Ban Ki Moon akiwa na Dkt.
Asha-Rose Migiro.
.............................
Na Dotto Mwaibale
UTEUZI wa Dkt. Asha-Rose Migiro kuwa Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM),
umeonesha kuwa wanawake sasa wamefikia hatua kubwa ya kuaminika katika uongozi.
Kikao cha Halmashuri Kuu ya
CCM (Taifa) chini ya Mwenyekiti wake na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Dkt.Samia Suluhu Hassan kilichoketi Agosti 23, 2025 pamoja na mambo mengine kilimteua
Dkt. Migiro (Balozi) kushika nafasi ya katibu mkuu wa chama hicho.
Akiongea katika mahojiano maalum na mwandishi wetu kuelezea
maoni yake kufuatia uteuzi wa mwanadiplomasia huyo, Mwenyekiti Mstaafu wa Chama
cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA) na Mhariri Mtendaji wa Clouds
FM, Joyce Shebe alisema uteuzi wake ni
ishara ya mabadiliko makubwa ya kuaminika kwa wanawake katika nafasi za
uongozi.
”Hii ni tofauti na hapo nyuma ambapo ilikuwa ngumu kwa
wanawake kupewa nafasi kama hiyo au wanawake kushika nafasi kubwa”, alisema
Shebe.
Aliongeza kuwa sasa jamii imeanza kuwaamini wanawake kwamba
wanaweza kushika nafasi za uongozi na inatoa picha kujua uwezo wa kitaaluma wa
Dkt. Migiro.
“Sasa mtu anaweza kuhamaki kwamba huyu ataweza, Lakini moja
kati ya sifa ambazo mimi nazijua Dkt. Migiro anazo ni kwamba yeye ni
mwanadiplomasia mzuri na amehudumu kwenye chama kwa muda mrefu. Hii maana yake
chama kimemwamini na tunaamini kuwa ataitendea haki nafasi hiyo,” alisema.
Hata hivyo Shebe amesema wengine wataendelea kuwaamini
wanawake kwani wanapompa mwanamke nafasi ya juu namna hiyo maana yake ni kwamba
wanatengeneza kizazi cha watoto wa kike kwa kufanya uamuzi wa kusomesha watoto
hao ambapo mwisho wa siku wote wanakuja kuleta mchango kwenye taifa letu.
Katibu wa Jumuiya ya Wazazi ya CCM Wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma Angelo Madundo anasema uteuzi huo katika kumbukumbu umeweka rekodi kwa kada wa CCM mwanamke kushika nafasi kubwa ya Katibu Mkuu tangu nchi yetu ipate uhuru.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan alipokuwa Makamu wa Rais akizungumza na aliyekuwa Balozi wa Tanzania Nchini Uingereza Dkt. Asha_Rose Migiro alipotembelea Ofisini kwake Ikulu jijini Dar es Salaam.
..........................
Alisema uteuzi huo ni hamasa ya Rais wa Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania na Mwenyekiti wa CCM Taifa
Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuwahamasisha wanawake kushika nafasi
mbalimbali za uongozi ndani ya chama na Serikali.
Aliongeza kuwa uteuzi huo siyo kwamba ulenge muktadha wa
mwanamke lakini Dkt. Migiro ni mmoja wa wanawake mashuhuri duniani na si tu kwa
Tanzania, tukikumbuka kwamba mwaka 2007 na 2012 Katibu Mkuu Mstaafu wa Umoja wa
Mataifa Ban Ki-moon alimteua kuwa msaidizi wake ambapo aliweza kuyahudumia
mataifa zaidi ya 194 ambayo ni wanachama wa umoja huo.
“Uteuzi wa Dkt. Migiro siyo wa kubahatisha kikubwa
tutakachoweza kukizungumzia ni historia mpya ya mwanamke kushika madaraka ya
katibu mkuu wa chama na tuna amini ni mwanadiplomasia mahiri, uzoefu wake katika
uongozi na siasa, dunia na Afrika anafaa kukisimamia chama cha CCM ambacho ni
kikubwa Afrika,” alisema Madundo.
Kada wa CCM kutoka IItigi mkoani Singida Mhandisi Felix
Dagaki naye anasema Dkt. Migiro ni kiongozi mbobezi wa masuala ya kimataifa, hivyo uteuzi huo ni wa viwango vya hali ya juu
na kuwa chama sasa kinakwenda kufanya mapinduzi makubwa ya utendaji.
“Nitumie nafasi hii kuipongeza Halmashuri
Kuu ya CCM (Taifa) chini ya Mwenyekiti wake Dkt.Samia kwa uteuzi huo mpana na
uliotukuka na wa kipekee”, alisema Dagaki.
Rose Ngunangwa Mkurugenzi Mtendaji, Shirika la Vyombo vya
Habari kwa Maendeleo ya Jamii (TAMCODE) kwa upande wake naye alisema chama
hicho kimefanya vema kwa kumuweka mwanamke kwenye nafasi hiyo ya juu kwa sababu
kumekuwa na changamoto ya mfumo dume kwenye vyama vingi.
Alisema Tume Huru ya Uchaguzi (INEC) inakifungu ambacho
kinasisitiza umuhimu wa kuwepo na madawati ya kijinsia yenye sera ya kutokomeza
ukatili kwa wanawake wakati wa siasa na uchaguzi.
Aliongeza kuwa miaka ya nyuma kulikuwa na malalamiko mengi
kuhusu wanawake kushindwa kupata nafasi za uongozi kutokana na safu ya viongozi
wa vyama kuwa ni wanaume hivyo kuwa vigumu kwao kuupata.
“ Kwawalicho kifanya CCM ni kitu kizuri mwenyekiti wake ni
mwanamke na katibu sasa ni mwanamke hiyo ni fursa nzuri kwao wanawake kupitisha
ajenda zao na kuzijadili”, alisema Ngunangwa.
Hata hivyo alisema kuwekwa Katibu mkuu mwanamke kwenye chama
kutachagiza utekelezaji wa sera ya jinsia na pia miundombinu yote au mikakati
yote na kuhakikisha wanawake waliopo kwenye siasa wanalindwa dhidi ya ukatili
wa aina zote.
Ngunangwa aliongeza kuwa wanawake wa chama hicho watakuwa
huru zaidi kwenda kwake kumueleza madhira watakayo kuwa wakikumbana nayo kuliko
kama angekuwa mwanaume.
Alisema Dkt. Asha-Rose Migiro anauzoefu mkubwa kimataifa na
kitaifa na mwenye umri wa busara na ni mtu mzima ameona mengi anaweza kumshauri
mtu, kumkosoa na akaeleweka atakapokuwa akiongea kwenye chama.
Aliongeza kuwa Dkt.Migiro anatajwa kuwa ni mwenye elimu ya
kutosha na kuwa ni mmoja wa wanawake
waliofanya vizuri sana kwenye masomo ya sheria katika historia ya nchi yetu
kwani alipata ufaulu wa kiwango cha juu.
Mwanachama wa CCM kutoka Zanzibar, Hussein Ramadhan Layya
(maarufu Msokolo), ameipongeza Halmashauri
Kuu ya CCM chini ya Mwenyekiti wake Dkt. Samia na Makamu Mwenyekiti Dkt.
Hussein Ali Mwinyi, kwa uongozi wao thabiti wa kuimarisha safu ya chama hicho.
Alisema uteuzi wa viongozi hao unaonesha imani kubwa juu ya
uwezo wao na kueleza kuwa Dkt. Asha-Rose
Migiro anauzoefu mkubwa na ni mwanadiplomasia ambaye anakwenda kukifanyia
makubwa chama hicho.
Aliongeza kuwa Ali Mwinyi ambaye ameteuliwa kuwa ni Katibu
Mkuu wa Umoja wa Wanawake wa CCM (UWT) ni kielelezo cha dhamira ya chama
kuendeleza usawa wa kijinsia na kumsaidia mwanamke kushiriki ipasavyo katika
uongozi na maendeleo ya taifa.
Aliyekuwa Balozi wa Tanzania nchini Uingereza na sasa ni Katibu Mkuu wa CCM Taifa, Dkt. Asha-Rose Migiro alipokuwa na wanamichezo wa Tanzania kwenye Michezo ya Jumuiya ya Madola alipowatembelea katika kijiji cha wanamichezo katika Chuo Kikuu cha Birmingham Julai 25, 2025







No comments:
Post a Comment