Meneja wa NSSF Mkoa wa Singida, Oscar Kalimilwa akizungumza wakati wa kuhitimisha maadhimisho ya wiki ya huduma kwa wateja Oktoba 10, 2025.
...................................
Na Waandishi Wetu
SHIRIKA la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF) Mkoa
wa Singida limehitimisha Maadhimisho ya wiki ya huduma kwa wateja kwa kupata
elimu ya damu salama kutoka kwa wataalam wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa
Singida ya Mandewa.
Mtaalam wa Damu Salama kutoka hospitali hiyo,
Anyelwisye Philimoni akizungumza wakati wa utoaji elimu hiyo alisema uchangiaji
wa damu siyo vita bali inasaidia kuokoa maisha ya watu.
Alisema uchangiaji wa damu hauna madhara yoyote
hivyo amewatoa watu waliokuwa na wasiwasi wa kuchangia na kuwataka kujitokeza
kuchangia.
“ Mahitaji ya damu katika hospitali zetu ni
makubwa mno hivyo inahitajika kwa wingi ili kupunguza changamoto ya upungufu
katika Hospitali zetu ya Rufaa, Mkoa na Makiungu,” alisema Philimoni.
Alisema mahitaji hayo yamekuwa yakiongezeka
kila siku na kuwa huduma hiyo wamekuwa wakiitoa katika hospitali mbalimbali za
binafsi na Serikali na ndiyo maana Serikali imekuwa ikifanya jitihada za
kupatikana kwake kwa kuunda timu ya kuitafuta.
Meneja wa NSSF Mkoa wa Singida, Oscar Kalimilwa
akizungumza wakati wa kuhitimisha maadhimisho hayo alisema kwao ni siku muhimu
sana kwa kuwakumbuka wanachama wao na kushirikiana nao kwani bila yao wao
wasingekuwepo.
Alisema kuwa hivi sasa shirika hilo limepiga
hatua kubwa kwani huduma zao zote zinapatikana mkononi kama ilivyo kauli mbiu
yao ya mwaka huu isemayo ‘Kidijitali Tumeweza, kwani mwanachama anaweza
kufungua madai mwenyewe na mwajiri anaweza kulipa kupitia mfumo huo wa
kidijitali.
“Mwanachama anaweza kuona michango yake
mwenyewe bila ya kufika kwenye ofisi yetu hii ni hatua kubwa kama shirika
tuliyoifikia,” alisema Kalimilwa.
Akizungumza kwa niaba ya waajiri Fr.
Constantine Missanga kutoka Hospitali ya Makiungu aliishukuru NSSF kwa ushirikiano
ambao imekuwa ikiwapa na kutambua mchango wao wa kuwachangia wafanyakazi wao.
Katika maadhimisho hayo
NSSF Mkoa wa Singida imezitambua taasisi na waajiri wanaojitolea kwa hali na
mali kuhakikisha michango ya wanachama wake inawasilishwa kwa wakati na
kuwatunuku vyeti maalum wakiwemo watu binafsi ambao ni wanachama wao.
Fuatilia mitandao yetu ya kijamii
Instagram: @singidaniblog
YouTube: singidani tv online
Tiktok: @singi.daniblog
Contact: +255 754362990
Email: singidani77@gmail.com







No comments:
Post a Comment