Meneja wa NSSF Mkoa wa Singida, Oscar Kalimilwa, akizungumza wakati wa ufunguzi wa Maadhimisho ya wiki ya huduma kwa wateja yaliyoanza leo Oktoba 6, 2025.
.................................
Na Mwandishi Wetu
WAKATI Maadhimisho ya wiki ya huduma kwa wateja yakiadhimishwa
Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF) linajivunia hatua ya matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano
(TEHAMA), ambayo imerahisisha utoaji wa huduma kulingana na kasi ya ukuaji wa
teknolojia duniani.
Hayo yamebainishwa na
mgeni rasmi wa ufunguzi wa maadhimisho hayo Mrakibu Msaidizi wa Jeshi la
Zimamoto na Uokoaji Mkoa wa Singida (ASP) Mwantumu Bakari wakati akifungua
maadhimisho hayo kwa niaba ya Kamanda wa jeshi hilo Mkoa wa Singida.
Mwantumu alisema kwa
sasa mfuko huo umewezesha wanachama kufungua madai ya mafao mbalimbali kwa njia
ya mtandao (Online claim lodging) na kutoa fursa kwa wanachama walioko mbali na
matawi ya shirika hilo kuweza kufungua madai mahali popote walipo na hatimaye
kulipwa kwa mujibu wa sheria na kanuni za ulipaji wa mafao.
Alisema Wiki ya huduma kwa wateja ilianzishwa rasmi
kimataifa mwaka 1987 na kupata utambuzi rasmi mwaka 1992 nchini Marekani na kupewa
hadhi kama sherehe ya kimataifa kwa lengo la kutambua umuhimu wa huduma bora
kwa wateja na juhudi za wafanyakazi wanaotoa huduma bora kwa wateja.
“Kwa mwaka huu (2025) maadhimisho yanaanza leo Oktoba
6, 2025 na kilele chake ni Oktoba 10, 2025, “ alisema
Mwantumu.
Alisema kwa kutambua umuhimu wa wanachama, waajiri,
wadau na wateja , mfuko huo umeandaa hafla hiyo fupi ili kuwashukuru wateja kwa
ushirikiano wanaotoa katika nyanja mbalimbali kama vile kujiandikisha,
kulipa michango, kununua au kutumia bidhaa na huduma zitolewazo na mfuko kama vile nyumba, viwanja, daraja la
mwalimu Nyerere au kupanga katika majengo mbalimbali yanayomilikiwa na mfuko
nchi nzima na hivyo kuufanya kukua na kuendelea kumudu kulipa mafao ya
wanachama wa NSSF wakiwemo wastaafu.
Mwantumu aliongeza kuwa kwa kuona umuhimu huo mfuko
umeamua kuadhimisha kwa pamoja na wateja wake kama shukrani kwa ushirikiano wao
na kuwapa hamasa ya kuendelea kuchagua kuhudumiwa na Mfuko wa NSSF.
“ Kama ilivyo kauli
mbiu ya mwaka huu, “Kidijitali
Tumeweza’’ Mfuko unajivunia hatua kubwa uliyofikia katika matumizi ya
Tehama ambayo yamerahisisha sana utoaji wa huduma,” alisema Mwantumu.
Alisema vilevile
wastaafu wa mfuko wamewezeshwa kuhakiki taarifa zao kwa njia ya mtandao (online
verification) na hivyo kuwapunguzia adha wazee ya kufika katika ofisi zao kwa
ajili ya zoezi la kujihakiki.
Aliongeza kuwa waajiri hawajaachwa nyuma kwani Mfuko
umewawezesha kulipa michango yao moja kwa moja kwa kutumia lango la waajiri
(Employers portal) ambapo wanaweza kujihudumia kwa kuwasilisha michango na
kupata risiti za uchangiaji na pia kuona maendeleo ya michango ya wafanyakazi
wao bila kufika katika matawi.
Alisema kwa kupitia mfumo huo mwajiri pia anaweza
kuona malimbikizo yake ya michango na kuweza kupata namba ya malipo (Control
number) pasipo kulazimika kufika katika tawi la NSSF hivyo kuokoa muda wa
uzalishaji.
“ Nitoe rai kwa
waajiri wote kuhakikisha wanajiandikisha na kuanza kuchangia wafanyakazi wao
kwa mujibu wa Sheria kwani Mfuko umejidhatiti kuwafikia waajiri wote ambao
hawajajiandikisha na kuwachukulia hatua stahiki wale wote wanaolimbikiza
michango ya wanachama,” alisema.
Aidha, Mwantumu
alisema mfuko pia umewezesha wanachama wake kujihudumia wenyewe kutumia Mfumo
wake wa lango la wanachama (Member portal) ambapo wanachama wanaweza kuangalia
michango yao pasipo kufika katika matawi.
Alisema mfuko unatoa
fursa kwa wanachama wake kuweza kupitia taarifa zao za uandikishwaji na kuomba
marekebisho pale wanapoona haziendani na taarifa zao zilizoko katika Mfumo wa
vitambulisho vya Taifa (NIDA). Kupitia lango husika wanachama pia wanaweza
kuwasilisha malalamiko kwenye Mfuko.
Mwantumu alisema mfuko
umeendelea kupata mafanikio hayo kutokana na jitihada za Serikali ya awamu ya
sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia
Suluhu Hassan.
“Mfuko unatumia hafla
hii kumpongeza na kumshukuru kwa juhudi kubwa zilizofanywa na zinazoendelea
kufanywa na Serikali ya awamu ya sita kwa namna inavyoendelea kutoa kipaumbele katika kuboresha huduma za jamii
na kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji wa ndani yaliyowezesha Mfuko kukua na
hatimaye kumudu kupandisha kima cha chini cha Pensheni ya wastaafu kutoka kiasi
cha Sh.100,000 mpaka kufikia Sh. 150,000," alisema Mwantumu.
Akizungumzia kwa upande wa watumishi, alisema Serikali ya awamu ya sita
imeboresha mifumo ya watumishi kujipima kwa malengo
kwa kuandaa mfumo wa (PEPMIS) ambao umewezesha watumishi kujiwekea malengo na hatimaye kujipima
kwa kutumia malengo ambayo wamejiwekea.
Mwantumu alisema mfumo huo umesaidia sana katika kuongeza
ufanisi na utendaji kazi wa watumishi wa Mfuko na watumishi wa Serikali kwa
ujumla ambapo alitoa rai kwa watumishi wote wa Mfuko kuhakikisha wanatumia
Mfumo huo kujaza utekelezaji wa malengo yao kwa muda waliopangiwa.
Aidha, Mwantumu alitumia fursa hiyo kwa niaba ya Mkurugenzi
Mkuu na Bodi ya wadhamini kuwashukuru na kuwapongeza watumishi wote kwa juhudi
kubwa za pamoja wanazozifanya katika kuwahudumia wanachama wa NSSF na kuwa mfuko
unatambua mchango wao katika kutekeleza majukumu waliyonayo.
Mwantumu alikumbusha kuwa maadhimisho ya mwaka huu
yamejikita katika kusheherekea mafanikio yaliyofikiwa na Mfuko lakini wasisahau
kutambua kwa upekee umuhimu wa wanachama wa NSSF katika mafanikio yote ambayo
Mfuko umeyafikia kwani bila wao Mfuko usingeliweza kuyafikia.
Aliwataka watumishi wa Mfuko huo kuvaa viatu vya
wateja na kuzingatia kauli zenye staha, utu na ubinadamu wanapokuwa wanatoa
Huduma za Mfuko lakini pia wazingatie miongozo ya utendaji ili kutoa haki na
usawa.
Meneja wa NSSF Mkoa wa Singida, Oscar Kalimilwa
akizungumza wakati akimkaribisha mgeni rasmi alisema wamekuwa wakishiriki
kuadhimisha wiki hiyo na wateja wao kama njia mojawapo ya kuwatambua na
kuwaenzi kwani wao ndiyo nguzo yao muhimu.
“Tunafanya hivyo ili nao waweze kutambua kwamba ni
watu wa dhamani kwetu na ndiyo wanao tufanya tuendelee kuwepo,” alisema
Kalimilwa.
Kwa upande wake Afisa Matekelezo Mwandamizi wa NSSF
Mkoa wa Singida, Marini Kimario alitaja majukumu manne ya shirika hilo kuwa ni
kuandikisha wanachama, kukusanya michango kutoka kwa wanachama na waajiri, uwekezaji
kwa lengo la kuongeza mtaji kutokana na michango ya wanachama ili wanapostaafu
waweze kulipwa kwa wakati na jukumu la mwisho ni ulipaji wa mafao ya wanachama
wao.
Katika maadhimisho hayo Jeshi la Zimamoto na Uokoaji
Mkoa wa Singida lilitoa elimu ya namna ya kujikinga na majanga ya moto, elimu
iliyotolewa na ASP Mwantumu Bakari kwa kushirikiana na Konstebo John Mduma.
Mrakibu Msaidizi wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Mkoa wa Singida (ASP) Mwantumu Bakari akizungumza wakati akifungua maadhimisho hayo kwa niaba ya Kamanda wa jeshi hilo Mkoa wa Singida.
Wateja wa NSSF na wageni waalikwa wakiwa kwenye maadhimisho hayo.
Wafanyakazi wa NSSF wakiwa kwenye maadhimisho hayo ya wiki ya huduma kwa mteja. Kutoka kushoto ni Mfaume Mfaume, Asha Iddi, Hafsa Ally na Latifa Singano.
Maadhimisho yakiendelea. Mwenye fulana nyeupe ni Afisa Matekelezo Mwandamizi kutoka PSSSF Mkoa wa Singida, Valency Masebu.
Meneja wa NSSF Mkoa wa Singida, Oscar Kalimilwa na ASP Mwantumu Bakari wakiwa kwenye maadhimisho hayo.
Wateja wa NSSF na wageni waalikwa wakiwa kwenye madhimisho hayo.
Muonekano wa keki maalum wakati wa maadhimisho hayo.
Meneja wa NSSF Mkoa wa Singida, Oscar Kalimilwa (kushoto),Mrakibu Msaidizi wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Mkoa wa Singida (ASP) Mwantumu Bakari (katikati) ambaye alikuwa mgeni rasmi na Mteja wa shirika hilo kutoka Iguguno mkoani hapa Mzee Ansay Shila wakikata keki maalum ya maadhimisho hayo.Mrakibu Msaidizi wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Mkoa wa Singida (ASP) Mwantumu Bakari akimlisha keki Konstebo John Mduma.
Mfanyakazi wa NSSF Mkoa wa Singida, Mfaume Mfaume. akilishwa keki.
Mfanyakazi wa NSSF Mkoa wa Singida, Hafsa Ally akilishwa keki.
Afisa Mambo ya Ndani wa NSSF Makao Makuu, Leopold Kambona akilishwa keki.
Afisa Huduma kwa Wateja NSSF Mkoa wa Singida, Latifa Singano, akilishwa keki.
Picha ya pamoja wakati wa maadhimisho hayo.









No comments:
Post a Comment