Na Dotto Mwaibale, Dodoma
BUNGE la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kikao chake
cha kwanza cha bunge la 13 kimemchagua rasmi Mbunge wa Jimbo la Ilala Jijini Dar es Salaam, Mhe.
Mussa Azzan Zungu kuwa Spika wa Bunge la 13 la Tanzania akichukua nafasi ya
mtangulizi wake Dkt.Tulia Ackson .
Mhe. Zungu anakuwa Spika wa Nane wa bunge hilo baada ya
kupigiwa kura na wabunge katika uchaguzi uliofanyika Novemba 11, 2025.
Katika uchaguzi huo Mhe. Zungu amepata kura 378 kati ya kura
383 hivyo kupata ridhaa ya kuongoza chombo hicho muhimu kwa kipindi cha miaka
mitano 2025 hadi 2030.
Makada wa Chama Cha Mapinduzi waliowahi kushika nafasi hiyo
ya Uspika tangu Tanzania ipate Uhuru wake ni Adamu Sapi Mkwawa aliyechaguliwa
Novemba 27, 1962, Erasto Andrew Mbwana Mang'enya Novemba 20, 1973, Pius Msekwa
Aprili 28, 1994, Samuel Sitta Desemba 28, 2005, Anna Makinda Novemba 10, 2010,
Job Ndugai Novemba 17, 2015 na Dkt. Tulia Ackson Februari 4, 2022.
Mhe Zungu ambaye katika Bunge la 12 lililopita alikuwa Naibu
Spika kuchaguliwa kwake kuwa Spika ni wazi kuwa amepanda ngazi kwa kushika
nafasi hiyo ambayo awali ilikuwa ikishikiliwa na Dk.Tulia ambaye alijitoa katika kinyang’anyiro hicho.
Zungu ameibuka
kidedea baada ya kuwashinda wagombea wa vyama vingine vitano waliojitosa katika
kinyang’anyiro hicho.
Wagombea hao ni Veronica Charles kutoka Chama cha NRA,
Anitha Mgaya wa NLD, Chhrisant Ndege wa Chama cha DP, Ndonge Said Ndonge kutoka
Chama cha AAFP na Amin Yongo kutoka Chama cha ADC
Kabla ya zoezi la kupiga kura kufanyika, wagombea wa nafasi
ya Spika wa Bunge la 13 la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania waliomba kura mbele
ya wabunge wateule kila mmoja akieleza nia yake ya kuliongoza Bunge lenye
uwajibikaji, ushirikiano na kuwatumikia wananchi.
Mgombea wa kwanza kujinadi kwa wabunge ni Veronica Charles
kutoka Chama cha NRA, ambaye alisema akichaguliwa kuwa Spika atalifanya
Bunge liwe la usawa na la wananchi.
Veronica alisema ataondoa kambi rasmi ya upinzani na
kuanzisha kambi ya majadiliano kwa lengo la kuimarisha umoja na ushirikiano
bungeni.
Aidha, alimpongeza Rais Dk.Samia Suluhu Hassan kwa kuwa
mfano wa kuigwa, akisema ni kiongozi aliyempa ujasiri wa kuwania nafasi hiyo.
Naye Anitha Mgaya kutoka Chama cha NLD amesema dhamira yake ni
kuhakikisha nidhamu, heshima na utulivu vinatawala mijadala yote bungeni.
Mgaya alisema kama kijana ataweka mkazo kwa kuwaelimisha vijana juu ya thamani ya amani,
upendo na utulivu.
Kwa upande wake, Chrisant Ndege wa Chama cha DP amesema ana
nia ya kusimamia Bunge litakalokuwa na uwezo wa kuishauri na kuisimamia
Serikali kwa mujibu wa Katiba.
Amesema kuwa mihimili mitatu ya dola ambayo ni
Serikali, Bunge na Mahakama inapaswa
kufanya kazi kwa ushirikiano, huku kila mhimili ukitekeleza majukumu yake kwa
uadilifu.
Ndege amesema atahakikisha sheria zinazotungwa zinakuwa na
tija kwa maendeleo ya wananchi .
Ndonge Said Ndonge kutoka Chama cha AAFP ameanza kwa
kumpongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa ushindi alioupata.
Aidha, Ndonge
alitumia falsafa ya neno KIONGOZI kueleza misingi yake ya uongozi akisema K ni
kukubali kukosolewa, I kujua tabia za unaowaongoza, O kuonyesha kwa vitendo, N
kunena kauli thabiti, G kugawa madaraka, O kuondoa uonevu, Z kuzuia migogoro na
I kuinua kipato.
Kwa upande wake Amin Yongo, kutoka Chama cha ADC amesema
endapo atachaguliwa kuwa Spika, atahakikisha Bunge linasimamia amani, umoja wa
kitaifa na katiba ya nchi.
Kwa upande wake, Mhe. Musa Azan Zungu kutoka CCM alisema
akipata nafasi ya Uspika, ataunganisha Bunge kwa maslahi ya wananchi na
kuhakikisha linafanya kazi kwa ufanisi ili kufanikisha utekelezaji wa Dira ya
Taifa ya Maendeleo ya 2050.
Zungu alisema ataendelea kuimarisha uhusiano kati ya Bunge
na wananchi ili kuhakikisha hoja zinazojadiliwa bungeni zinagusa moja kwa moja
maisha ya Watanzania.
WASIFU WA SPIKA MPYA WA BUNGE LA TANZANIA MHE. MUSSA AZZAN
ZUNGU.
Mussa Azzan Zungu ni mwanasiasa mkongwe wa Chama Cha
Mapinduzi (CCM) ambaye amehudumu bungeni kwa muda wa miaka 20 mfululizo, huku
akijipatia heshima kubwa kutokana na uzoefu wake wa muda mrefu katika shughuli
za Kibunge na utumishi wa umma.
Mussa Azzan Zungu ni Mhandisi wa ndege aliyepata mafunzo
nchini Tanzania na Canada, akionyesha umahiri katika taaluma ya kiufundi kabla
ya kuingia kwenye siasa.
Kwenye uzoefu wa kibunge amekuwa Mbunge wa Bunge la Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania tangu miaka ya 2000.
Amekuwa mjumbe wa Tume ya Utumishi wa Bunge kati ya mwaka
2016 na 2025, amekuwa
Mwenyekiti wa Bunge kati ya mwaka 2012 na 2021, na pia amekuwa Naibu Spika kati
ya mwaka 2022 na 2025 kabla ya kuchaguliwa kuwa Spika wa Bunge la 13.
Akiwa bungeni amewahi kuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Mambo ya
Nje, Ulinzi na Usalama kwa zaidi ya miaka 16.
Mussa Azzan Zungu amewahi kufanya kazi na Maspika wanne
tofauti, jambo linalompa uzoefu mkubwa wa kiutawala na Kibunge.
Kwenye uongozi wa Kimataifa, amewahi kuwa kiongozi wa Bunge
la Tanzania katika mikutano ya Umoja wa Mabunge ya Nchi za Afrika, Karibiani na
Pasifiki (ACP) pamoja na Bunge la Umoja wa Ulaya (EU).
Pia amewahi kuwa kiongozi wa Chama cha Mabunge ya Jumuiya ya
Madola (CPA – Tanzania Branch) na mwakilishi wake katika vikao vya kimataifa.
Ameshiriki ziara za mafunzo ya Kibunge katika zaidi ya nchi
23, akijenga uelewa mpana wa mifumo ya Mabunge duniani.
Kwenye Serikali amewahi kuhudumu kama Waziri wa Nchi, Ofisi
ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), nafasi iliyompatia uzoefu katika
masuala ya utawala wa Serikali na ushirikiano wa Muungano.
Kwa heshima na sifa binafsi Mhe. Zungu ni mweledi wa kanuni na
taratibu za uendeshaji wa Bunge, mtumishi wa umma mwenye uadilifu, aliyejitolea
kulitumikia Taifa kwa uwazi na uaminifu, na ni mshindi wa Nishani ya Vita ya
Kagera, kama ishara ya uzalendo na mchango wake kwa Taifa.
Makala hii imeandaliwa kutoka vyanzo mbalimbali lengo likiwa ni kuhabarisha umma kuhusu kumjua vizuri Spika Mpya wa Bunge la 13 la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe Mussa Azzan Zungu.








No comments:
Post a Comment