Na Dotto
Mwaibale, Singida
MKUU wa Mkoa
wa Singida, Mhe. Halima Dendego amewataka Wahitimu wa Taasisi ya Uhasibu Tanzania
(TIA) Kampasi ya Singida wa mwaka wa masomo 2024/2025 kukumbatia Teknolojia na
Akili Unde (AI) ili kwenda sanjari na zama hizi za mapinduzi ya kidijitali.
Mhe. Dendego ambaye alikuwa mgeni rasmi
ameyasema hayo leo Desemba 2, 2025 wakati akihutubia katika mahafali ya 23 ya
taasisi hiyo Kampasi ya Singida.
“Katika zama
hizi za mapinduzi ya kidijitali na Akili Unde (AI), soko la ajira limebadilika
kwa kasi kubwa. Ajira nyingi sasa zinahitaji ujuzi wa teknolojia, ubunifu na uwezo wa kubadilika,” alisema Dendego.
Aidha, Dendego
aliwataka wahitimu hao kutumia mitandao ya kijamii kwa maendeleo, kutangaza
biashara, kujifunza na kuunda mtandao wa fursa badala ya kuitumia vibaya.
Dendego
alitumia nafasi hiyo kuwapongeza wahitimu hao 1,490 kwa bidii, uvumilivu na
nidhamu waliyoionesha hadi kufikia hatua hiyo.
Wakati huo
huo Dendego alitoa shukurani zake za dhati kwa
Afisa Mtendaji Mkuu wa TIA, Profesa William Pallangyo, pamoja na Bodi ya
Ushauri ya Wizara na Uongozi wote wa Taasisi hiyo kwa kazi kubwa wanayoendelea
kufanya katika kuendeleza elimu ya juu nchini.
Afisa
Mtendaji Mkuu wa TIA, Profesa William Pallangyo akizungumza kwenye mahafali
hayo, alisema katika mwaka huu wa masomo TIA Kampasi ya Singida inajivunia
kutoa jumla ya wahitimu 1,490 (wanawake 733 sawa na asilimia 49.2, na wanaume
757 sawa na asilimia 51.8)
Alisema Kati
yao ngazi ya cheti cha awali ni wahitimu ni 388, Astashahada 389, shahada 373
na shahada 340.
Profesa
Pallangyo alisema wahitimu hao wanawakilisha takribani asilimia 14.4 ya
wahitimu wote 10,334 wa mwaka wa masomo 2024/2025 katika kampasi zote nane za
TIA.
Pallangyo
alisema takwimu hizo zinaonesha wazi kuwa Kampasi ya Singida inaendelea kukua
kwa kasi na inachangia kwa kiasi kikubwa katika kuzalisha wataalamu wa Uhasibu,
Ununuzi na Ugavi, Biashara, Rasilimali Watu na Masoko.
Aisema
Kampasi ya Singida imepata mafanikio makubwa kwenye eneo la miundombinu,
mafunzo, utafiti na ushauri wa kitalaamu.
Profesa
Pallangyo alisema ili kuhakikisha wanaendelea kutoa elimu yenye ufanisi,
Taasisi hiyo imeendelea kuboresha miundombinu ya kimkakati katika kampasi ya
Singida.
Alisema
kupitia Mradi wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Kiuchumi (HEET), unaofadhiliwa na
Benki ya Dunia kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Kampasi ya
Singida imenufaika na Sh. Bilioni 13.5 kwa ajili ya ujenzi wa jengo la Taaluma.
Afisa
Mtendaji Mkuu huyo wa TIA, Profesa Pallangyo alitumia nafasi hiyo kuishukuru
Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uwekezaji huo mkubwa unaolenga kuboresha
mazingira ya kujifunzia na kufundishia na kuongeza tija katika utoaji elimu.
Kwa upande
wake Mwenyekiti wa Bodi ya Ushauri ya Wizara, Profesa Jehovaness Aikael alisema
Udahili katika Kampasi ya Singida umekuwa ukiongezeka mwaka hadi mwaka mathalan
katika mwaka wa masomo 2024/ 2025 kampasi hiyo ilidahili jumla ya wanafunzi
2,623 ikiwa ni ongezeko la asilimia 24, ikilinganishwa na wanafunzi 2,115 kwa
mwaka 2021/ 2022 (kwa kipindi cha miaka mitano ya nyuma) na kuwa hiyo inaonesha
kuongezeka kwa Imani ya elimu itolewao TIA.
Profesa
Aikael aliwataka wahitimu hao kuendelea kutumia ufahamu wa kidijitali na
teknolojia kufanya biashara kwa njia bunifu.
Alisema Ubunifu wa Kidijitali utawawezesha kuunda bidhaa na huduma mpya, kuongeza ushindani katika soko, na kufanikisha biashara ndogondogo kuwa kubwa, hatimaye kuchangia katika Tanzania yenye uchumi imara, jumuishi na wezeshi.
Mahafali hayo yalihudhuriwa na Viongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na vyama vingine vya siasa, Viongozi wa Serikali na Taasisi zisizo za kiserikali katika ngazi mbalimbali, Wahadhiri , Watumishi Waendeshaji, Wanachuo wote wa TIA na Waandishi wa Habari.
Kuhusu kozi zinazotolewa TIA Singida ni Accountancy , Procurement and logistic management, Human resource management, Business Administration na Marketing and public relation.
Kozi zote hizo zinaanzia ngazi ya cheti mpaka masters.
Kwa mawasiliano zaidi kuhusu chuo hicho unaweza kupiga simu namba 0752540341 au kupitia mtandao wao (Website) https://www.tia.ac.tz/
Mkuu wa Mkoa wa Singida, Halima Dendego akipata maelezo ya kazi mbalimbali za ubunifu zinazofanywa na Wanafunzi wa taasisi hiyo wakati alipotembelea banda la wabunifu hao kuona kazi zao.







No comments:
Post a Comment