Na. Peter Haule, WF, Dar es Salaam
Benki ya Dunia (WB) imeahidi kuendelea kuimarisha ujuzi wa Watumishi wa Benki hiyo waliopo nchini ili waweze kutoa ushauri na ujuzi utakao endelea kuchochea maendeleo ya sekta ya umma na binafsi.
Hayo yamebainishwa katika Ofisi Ndogo za Hazina, jijini Dar es Salaam na Makamu wa Rais wa Benki ya Dunia anaesimamia Rasilimali Watu, Bi. Radoslava Dimitrova Anguelova, wakati wa Mkutano kati yake na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Bi. Amina Khamis Shaaban.
Bi. Anguelova alisema kuwa kuna umuhimu mkubwa wa kuhakikisha Benki ya Dunia inafanya kazi kwa ukaribu na Tanzania ili Taifa liweze kufikia malengo ya maendeleo iliyojiwekea.
Alisema kuwa anayofuraha kusikia tayari kuna juhudi kubwa zimefanyika katika kutekeleza malengo na ameahidi kuhakikisha Watumishi wa Benki hiyo nchini Tanzania wanakuwa na ushauri mwafaka na ujuzi wa kiwango cha juu ili kuwa chachu ya maendeleo.
Akizungumza kwa niaba ya Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-maamry Mwamba, Naibu Katibu Mkuu, Bi. Amina Shaaban, aliishukuru Benki ya Dunia (WB) kwa kuipatia Serikali fedha za mikopo kwa ajili ya kutekeleza miradi 35 yenye thamani ya takribani dola za Marekani bilioni 8.5 inayoendana na vipaumbele vya Taifa.
Kuhusu Watumishi wa Kundi la Benki ya Dunia (WBG) wanaofanya kazi nchini Tanzania, alisema kuwa watumishi hao wamekuwa na mwitikio mzuri wa kusikiliza, kuzoea mazingira na kushirikiana na Serikali ambao umekuwa nguzo muhimu ya kufikia malengo ya vipaumbele vya Mipango ya Taifa”, alisema Bi. Shaaban.
Aidha, Bi. Shaaban alisema kuwa Serikali inathamini ushirikiano na Kundi la Benki ya Dunia na kuahidi kuendeleza ushirikiano huo wenye tija kwa pande zote, huku akibainisha kuwa kwa pamoja wanaweza kuhakikisha ajenda ya maendeleo ya Tanzania inafikiwa kupitia sera madhubuti, programu zenye ufanisi na watumishi walio na hamasa ya kuleta mabadiliko chanya.
Mkutano huo pia ulihudhuriwa pia na Mkurugenzi wa Benki ya Dunia kwa nchi za Tanzania, Malawi Zambia na Zimbabwe Bw. Nathan Belete, Meneja wa Uendeshaji wa Benki ya Dunia kwa nchi hizo, Bi. Milena Stefanova, Meneja wa Shirika la Benki ya Dunia la Kimataifa linalosimamia Sekta Binafsi (IFC), Bi. Martine Valcine, pamoja na Kamishna wa Idara ya Fedha za Nje, Wizara ya Fedha, Bw. Rished Bade.










No comments:
Post a Comment