Na Munir Shemweta, Lushoto WANMM
Katika jitihada za
kuhakikisha maeneo ya umma hayavamiwi na kusababisha migogoro ya ardhi,
Serikali imeendelea kusisitiza taasisi za umma nchini kupima na kuyalinda
maeneo yake.
Kauli hiyo ya Serikali
inafuatia kujitokeza kwa changamoto za ardhi katika eneo la Ofisi ya Mkuu wa
wilaya ya Lushoto (Bomani) pamoja na Halmashauri ya wilaya ya Bumbuli ambapo
baadhi ya wananchi wamedai kuondolewa kwenye maeneo wanayomiliki wakati wa
ziara ya Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba wilayani Lushoto mkoa wa Tanga.
Akizungumza kwa nyakati tofauti katika mikutano ya hadhara kwenye eneo la Lushoto, Soni pamoja na Mlalo tarehe 17 Februari, 2026, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dkt. Leonard Akwilapo, amesema kuwa katika kukabiliana na tabia ya uvamizi wa maeneo ya umma, taasisi za Serikali zinatakiwa kuchukua hatua za kupima maeneo yake yote pamoja na kuyalinda.
“Nitoe maelekezo kwa taasisi zote za Serikali, Wizara ya Ardhi tupo; tupo kutoa hati katika maeneo ya Serikali,” amesema Mhe. Dkt. Akwilapo.
Pamoja na kuzitaka
taasisi za Serikali kuchukua hatua hiyo, Dkt. Akwilapo amesisitiza pia wananchi
kupima maeneo yao wanayomiliki, sambamba na kuacha kujenga kiholela ambapo
aliwataka kuomba vibali vya ujenzi pale wanapotaka kufanya maendelezo.
“Ninyi wananchi msijenge kiholela. Tupo kuwapa hati; ombeni hati, tutawapa, na baadaye muombe vibali vya ujenzi ili mjenge nyumba mkiwa na amani na muwe na furaha,” amesema Waziri wa Ardhi.
Waziri Mkuu wa Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania, amehitimisha ziara yake mkoani Tanga jana ambapo
alizindua Jengo la Oxygen katika Hospitali ya Wilaya ya Lushoto pamoja na Shule
Mpya ya Amali ya Majulai, Mlalo pamoja na kuzungumza na wananchi wa Soni katika
halmashauri ya Bumbuli.
Katika ziara yake hiyo
Dkt Mwigulu Nchemba alikagua na kuzindua miradi ya maendeleo, iliyoambatana pia
na kupokea kero kutoka kwa wananchi, pamoja na kuchukua hatua stahiki katika
maeneo yenye changamoto.















No comments:
Post a Comment