MASOKO YA MADINI NA MAPINDUZI YA UCHUMI WA DHAHABU TANZANIA - SINGIDANI BLOG

Habari za Hivi Punde

Post Top Ad

Saturday, 7 February 2026

MASOKO YA MADINI NA MAPINDUZI YA UCHUMI WA DHAHABU TANZANIA

Uchambuzi yakinifu wa faida mapato na mustakabali wa wachimbaji wadogo

Fundi Sanifu Tume ya Madini Geita, Peter Jamhuri,  akiwa kazini

............................................
Kwa muda mrefu, sekta ya madini hususan dhahabu imekuwa ikitajwa kama uti wa mgongo wa uchumi wa Tanzania. Hata hivyo, kwa miaka mingi mchango huo haukuwa ukijidhihirisha kikamilifu kwa wachimbaji wadogo wala kuakisi kiwango halisi cha mapato kilichokuwa kinapaswa kuingia kwenye hazina ya taifa. Biashara ya madini ilikuwa ikifanyika kwa kiasi kikubwa nje ya mifumo rasmi, hali iliyochochea utoroshaji wa madini, kukosekana kwa bei shindani, unyonyaji wa wachimbaji wadogo na upotevu mkubwa wa mapato ya serikali.

Mageuzi ya kweli yalianza pale serikali ya Tanzania ilipoamua kuisimamia sekta ya madini kwa misingi madhubuti ya kisheria, kitaasisi na kimfumo, kwa kuanzisha masoko rasmi ya madini na vituo vya ununuzi wa dhahabu nchi nzima. Hatua hii imeleta mabadiliko ya kihistoria katika biashara ya madini, hususan katika mikoa ya kimadini kama Geita, na kuifanya dhahabu kuwa rasilimali inayoonekana na kunufaisha taifa.

Msingi wa Kisheria wa Uanzishwaji wa Masoko ya Madini

Uanzishwaji na uendeshaji wa masoko ya madini nchini unasimamiwa na Sheria ya Madini, Sura ya 123 ya Sheria za Tanzania ya mwaka 2010, kama ilivyorekebishwa mwaka 2017. Sheria hii inaipa serikali mamlaka ya kusimamia, kudhibiti na kurasimisha shughuli zote za madini ili kuhakikisha rasilimali za taifa zinawanufaisha wananchi na serikali kwa uwiano unaostahili.

Kupitia marekebisho ya mwaka 2017, sheria iliweka msisitizo mkubwa katika:

Urasimishaji wa biashara ya madini

Uanzishwaji wa masoko ya madini yanayosimamiwa na Tume ya Madini

Uthaminishaji wa madini kwa uwazi

Uwekaji wa bei elekezi

Uhakika wa ukusanyaji wa mrabaha, kodi na tozo za serikali

Sheria hii ndiyo nguzo kuu iliyobadilisha mwelekeo wa biashara ya madini kutoka mfumo usio rasmi kwenda mfumo wa wazi, unaosimamiwa na wenye manufaa ya moja kwa moja kwa taifa.

Geita: Kitovu cha Ufanisi wa Masoko ya Madini

Kwa mujibu wa John Maganga, Mujiolojia wa Mkoa wa Kimadini Geita, mkoa huo unasimamia masoko mawili ya madini pamoja na vituo tisa vya ununuzi wa dhahabu vilivyopo karibu na maeneo yenye shughuli kubwa za uchimbaji mdogo. Hatua hii imelenga kuwarahisishia wachimbaji kuuza madini yao karibu na maeneo ya uzalishaji, hivyo kupunguza gharama, hatari za usalama na mianya ya utoroshaji.

Kwa mujibu wa sheria, wachimbaji na wafanyabiashara wa madini kutoka mikoa mingine au hata nje ya nchi wanaruhusiwa kuuza madini yao katika Soko Kuu la Madini Geita na Katoro, kwa kulipa tozo stahiki. Hali hii imefanya Geita kuwa kitovu muhimu cha biashara ya dhahabu kitaifa.

Takwimu za Miaka Mitano: Dhahabu Inapoongea kwa Ushahidi

Katika kipindi cha miaka mitano, kuanzia mwaka wa fedha 2021/2022 hadi 2025/2026 (hadi Desemba 31, 2025), masoko ya madini ya Mkoa wa Geita yamekusanya takwimu zifuatazo:

Uzito wa dhahabu iliyouzwa: kilo 14,762.67

Thamani ya dhahabu: TZS 2,493,774,821,918.10

Takwimu hizi ni ushahidi dhahiri kuwa uanzishwaji wa masoko ya madini umefanikiwa kuirejesha dhahabu iliyokuwa ikipotea kwenye biashara isiyo rasmi na kuiweka kwenye mzunguko halali wa uchumi wa taifa.

Mapato ya Serikali na Uwajibikaji wa Kifedha

Kwa mujibu wa Peter Jamhuri Nyawegana, Fundi Sanifu wa Tume ya Madini Mkoa wa Geita, ofisi yake ina majukumu ya uthaminishaji wa dhahabu na madini ya fedha, ukataji wa mrabaha na ada za ukaguzi, pamoja na usimamizi wa biashara ya madini.

Katika kipindi cha 2021/2022 hadi 2025/2026, serikali ilikusanya:

Mrabaha na ada za ukaguzi: TZS 167,732,533,279.78

Mrabaha, ada za ukaguzi pamoja na HIV Levy: TZS 168,270,531,069.57

Haya ni mapato ambayo kwa miaka mingi yalikuwa hayakusanyiki kutokana na mifumo dhaifu ya biashara ya madini.

Kupungua kwa Utoroshaji na Kuimarika kwa Uwazi

Masoko ya madini yamepunguza kwa kiwango kikubwa utoroshaji wa dhahabu. Biashara sasa inafanyika kwa bei elekezi, uthaminishaji wa wazi na uwepo wa maafisa wa serikali. Hii imewezesha ukusanyaji wa kodi mbalimbali ikiwemo mrabaha, kodi ya ongezeko la thamani (VAT) na tozo za huduma.

Manufaa ya Moja kwa Moja kwa Wachimbaji Wadogo

Kwa mujibu wa George Paulo Maloba, Mwenyekiti wa Soko la Madini Geita na mmiliki wa Maloba Limited, masoko ya madini yamewapa wachimbaji wadogo soko la uhakika, bei shindani na usalama wa kifedha. Anasema soko hilo lina wafanyabiashara wakubwa wa dhahabu 95, jambo linaloashiria ukuaji wa uchumi wa eneo hilo.

Wanunuzi wa dhahabu akiwemo Magambo N. Magambo, Mkurugenzi wa Gambo Mine Limited, na Blessing John, wanakiri kuwa masoko ya madini yameondoa unyonyaji na kuleta mfumo wa haki unaompa mchimbaji thamani halisi ya jasho lake.

Changamoto ya Mfumo wa MMIMS

Pamoja na mafanikio hayo, bado kuna changamoto za kimfumo, hususan kwenye Mfumo wa Mineral Market Information Management System (MMIMS). Maboresho ya mfumo huu yanahitajika ili kuimarisha mtandao, kuongeza uwazi wa taarifa na kuhakikisha miamala inafungwa kwa wakati bila hasara.

Mabenki, Mitaji na Mustakabali wa Sekta

Mchimbaji mdogo Hassan Sadick, akiungwa mkono na Zahida Adam, Mkurugenzi wa Aman Elution, wanaeleza kuwa mustakabali wa sekta ya dhahabu upo katika uwezeshaji wa kifedha wa wachimbaji wadogo kupitia mabenki. Mitaji na vifaa vikapatikana, uzalishaji utaongezeka, ajira zitapanuka na mapato ya serikali yataongezeka maradufu.

Hitimisho

Masoko ya madini yamejidhihirisha kuwa nyenzo madhubuti ya maendeleo ya kiuchumi, uwazi wa biashara na ulinzi wa wachimbaji wadogo. Kwa kuendelea kusimamia kikamilifu Sheria ya Madini, Sura ya 123, kuboresha mifumo ya TEHAMA na kuimarisha ushirikiano na sekta ya fedha, masoko ya madini yataendelea kuwa injini muhimu ya maendeleo endelevu ya Tanzania.

John Maganga (wa pili kutoka kushoto) akitoa ufafanuzi wa jambo kwa maafisa Habari wa tume ya madini Dodoma
Hassan Sadick mchimbaji mdogo akizungumza na waandishi wa habari hawapo pichani
Mwenyekiti wa Soko la Madini Geita, George Paulo (kulia), akiwa Ofisi za Tume ya Madini ndani ya soko kuu la madini Geita
Mwanahabari Victor Bariety, akiwajibika

..........................
 Imeandaliwa na Victor Bariety 
Simu: 0757 856 284
Geita

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad