TANZANIA KUIMARISHA ZAIDI MFUMO IMARA WA UFUATILIAJI NA UDHIBITI UTAKASISHAJI FEDHA HARAMU - SINGIDANI BLOG

Habari za Hivi Punde

Post Top Ad

Wednesday, 4 February 2026

TANZANIA KUIMARISHA ZAIDI MFUMO IMARA WA UFUATILIAJI NA UDHIBITI UTAKASISHAJI FEDHA HARAMU

Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi. Mshamu Ali Munde (Mb), akizungumza wakati akifungua Mkutano wa Kimataifa wa Ubadilishaji wa Taarifa za Udhibiti wa Fedha Haramu Duniani (EGMONT Group meeting), uliozikutanisha nchi wanachama zaidi ya 182, uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano Arusha (AICC), jijini Arusha, kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb).
Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi. Mshamu Ali Munde (Mb), akiagana na Mwenyekiti wa Sekretarieti ya EGMONT, Bi. Elżbieta Franków- Jaśkiewicz, baada ya kufungua Mkutano wa Kimataifa wa Ubadilishaji wa Taarifa za Udhibiti wa Fedha Haramu Duniani (EGMONT Group meeting) uliozikutanisha nchi wanachama zaidi ya 182, uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano Arusha (AICC), jijini Arusha.
Mwenyekiti wa Sekretarieti ya EGMONT, Bi. Elżbieta Franków- Jaśkiewicz, akizungumza wakati wa hafla ya ufunguzi wa Mkutano wa Kimataifa wa Ubadilishaji wa Taarifa za Udhibiti wa Fedha Haramu Duniani (EGMONT Group meeting) uliokutanisha nchi wanachama zaidi ya 182, uliofunguliwa na Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi. Mshamu Ali Munde (Mb) kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano Arusha (AICC), jijini Arusha.
Baadhi ya Washiriki  wa Mkutano wa Kimataifa wa Ubadilishaji wa Taarifa za Udhibiti wa Fedha Haramu Duniani (EGMONT Group meeting) uliokutanisha nchi wanachama zaidi ya 182, wakimsikiliza Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi. Mshamu Ali Munde (Mb) akihutubia kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), wakati akifungua Mkutano huo uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano Arusha (AICC), jijini Arusha.
Kamishna wa Kitengo cha Kudhibiti Fedha Haramu (FIU), Bw. Majaba Magana, akizungumza jambo wakati wa Mkutano wa Kimataifa wa Ubadilishaji wa Taarifa za Udhibiti wa Fedha Haramu Duniani (EGMONT Group meeting) uliokutanisha nchi wanachama zaidi ya 182, uliofunguliwa na Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi. Mshamu Ali Munde (Mb) akihutubia kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano Arusha (AICC), jijini Arusha.
Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi. Mshamu Ali Munde (Mb) (Katikati aliyeketi), Mwenyekiti wa Sekretarieti ya EGMONT, Bi. Elżbieta Franków-Jaśkiewicz (kushoto aliyeketi), Kamishna wa Kitengo cha Kudhibiti Fedha Haramu (FIU), Bw. Majaba Magana (wa pili kushoto) aliyeketi, na Mwenyekiti wa Kamati ya Kitaifa ya Wataalamu wa Kuzuia Utakasishaji Fedha Haramu ambaye pia ni Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Bi. Sauda Msemo (kulia aliyeketi), wakiwa katika picha ya pamoja na Kamati ya Maandalizi wa Mkutano wa Mkutano wa Kimataifa wa Ubadilishaji wa Taarifa za Udhibiti wa Fedha Haramu Duniani (EGMONT Group meeting) uliokutanisha nchi wanachama zaidi ya 182, uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano Arusha (AICC), jijini Arusha.
-------------------------------------------

Tanzania imeihakikishia Jumuiya ya Kimataifa inayojihusisha na  ufuatiliaji na udhibiti wa Utakasishaji fedha haramu, ufadhili wa ugaidi na ufadhili wa silaha za maangamizi. Kwamba Serikali itaendelea kuimarisha na kuboresha mifumo yake ya udhibiti wa vitendo hivyo nchini.

 

Hayo yamesemwa na Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi. Mshamu Ali Munde (Mb), kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi. Khamis Mussa Omar (Mb), wakati wa Mkutano wa Kimataifa wa Ubadilishaji wa Taarifa za Udhibiti wa Fedha Haramu Duniani (EGMONT Group meeting), uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano Arusha (AICC), jijini Arusha.

 

Alisema Tanzania imepiga hatua kubwa katika kujenga mfumo imara wa kupambana na uhalifu wa kifedha, ikiwa ni pamoja na kuimarisha taasisi za udhibiti na ushirikiano wa kimataifa, hatua ambayo imewezesha Tanzania kuondolewa kwenye orodha ya nchi zenye mapungufu katika udhibiti wa utakasishaji fedha na ufadhili wa ugaidi, baada ya kutekeleza kwa mafanikio mpango wa hatua uliowekwa na Kikosi Kazi cha Kudhibiti Utakatishaji Fedha (FATF).

 

“Uamuzi wa Umoja wa Ulaya kuiondoa Tanzania kwenye orodha ya nchi zenye hatari kubwa umefungua ukurasa mpya wa uaminifu wa kifedha na kuvutia uwekezaji wa kigeni na Tunajivunia mafanikio haya ambayo ni matokeo ya uongozi thabiti, mageuzi ya kisheria, na ushirikiano wa karibu kati ya taasisi zetu za ndani na washirika wa maendeleo,” alisema Mhe. Mhandisi Munde.

 

Alisisitiza kuwa Tanzania itaendelea kushirikiana na nchi wanachama wa Kikundi cha EGMONT na makundi mengine kama Kikundi cha Afrika Mashariki na Kusini cha Kuzuia Utakasishaji Fedha - ESAAMLG, ili kuhakikisha mifumo ya ndani inalingana na viwango vya kimataifa vya uadilifu wa kifedha.

 

 

“Uhalifu wa kifedha hauna mipaka nchi moja haiwezi kushinda vita hii peke yake na tunapaswa kushirikiana, kubadilishana taarifa, na kufuatilia alama za fedha popote zinapopita,” aliongeza Mhe. Mhandisi Munde.

 

Aidha, Mhe. Mhandisi Munde,  alizishukuru taasisi za kimataifa ikiwemo Kitengo cha Hazina cha Uingereza (UK Treasury Unit), Shirika la Ujerumani la Ushirikiano wa Kimataifa - GIZ, Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya kudhibiti dawa za Kulevya na Uhalifu - UNODC, Mfuko wa Kimataifa wa Umoja wa Ulaya wa Kuzuia Utakasishaji Fedha na Ufadhili wa Ugaidi (EU Global Facility), Shirika la Fedha la Kimataifa - IMF na Benki ya Dunia kwa mchango wao mkubwa katika kutoa msaada wa kitaalamu na mafunzo kwa wataalamu wa uchunguzi na udhibiti wa fedha nchini.

 

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Sekretarieti ya EGMONT, Bi. Elżbieta Franków- Jaśkiewicz, alisema kuwa Tanzania kama mwanachama wa EGMONT, imekua bora hasa katika ushirikiano wa kimataifa ambao ni muhimu zaidi katika kulinda uadilifu wa mfumo wa kifedha wa ndani na duniani kote.

 

Bi. Jaśkiewicz alisema Kuwa, EGMONT imejizatiti kusaidia wanachama wake kwa kutoa majukwaa salama kwa vitengo, kubadilishana ujuzi na taarifa za kifedha, na kuwasaidia kupambana na Utakasishaji wa fedha, ufadhili wa ugaidi, na uhalifu unaohusiana.

 

“Tunafurahi sana kukaribishwa hapa Tanzania kwa ukarimu, sehemu ambayo ina nafasi muhimu na ya kuhamasisha katika kuimarisha ushirikiano katika Ukanda wa Afrika Mashariki na Kusini, na inaendelea kuonesha dhamira yake thabiti katika kuimarisha na kuendeleza ushirikiano wa kikanda na kimataifa katika mapambano dhidi ya utakatishaji wa fedha na ufadhili wa ugaidi” alisema Bi. JaÅ›kiewicz.

 

Aliongeza kuwa kuwapo na zaidi ya wajumbe 400, katika mkutano huo ni ushahidi wa nguvu ya kimataifa ya Jumuiya ya EGMONT na dhamira ya pamoja inayowaunganisha.

 

Naye Kamishna wa Kitengo cha Kudhibiti Fedha Haramu (FIU), Bw. Majaba Magana, alisema kuwa safari ya Tanzania katika kupambana na utakasishaji wa fedha na ufadhili wa ugaidi imekuwa ikikua hatua kwa hatua, na inayolenga mageuzi kwa kuanzishwa kwa Kitengo cha Ujasusi wa Kifedha (Financial Intelligence Unit) chini ya Sheria ya Kuzuia Utakasishaji wa Fedha ambapo ni hatua muhimu ya kitaasisi, iliyounda mamlaka ya kati yenye jukumu la kupokea, na kuchambua taarifa za kifedha.

 

“Tangu kuanzishwa kwake, Tanzania imeendelea kuwa thabiti katika kuzingatia viwango vya kimataifa kwa kutekeleza mageuzi ya kina ya kuimarisha mifumo yetu ya kisheria na kitaasisi” alisema Bw. Magana

 

Aliongeza kuwa juhudi za Tanzania katika marekebisho muhimu ya kisheria, uimarishaji wa usimamizi unaozingatia tathmini ya hatari, na kuongezwa kwa uwezo wa kiutendaji zimeleta matokeo dhahiri, yanayoonekana kupitia kuboreshwa kwa taarifa za miamala yenye kutiliwa shaka, kuongezeka kwa matumizi ya taarifa za kifedha katika mashtaka ya jinai, na kuimarika kwa ushirikiano wa kimataifa.

 

Mkutano huo wa EGMONT, ulikutanisha nchi wanachama wa Jumuiya hiyo zaidi ya 182, ambapo wanachama walibadilishana maarifa, utaalamu na taarifa za kifedha, ili kuimarisha mapambano ya kimataifa dhidi ya utakasishaji wa fedha haramu , makosa ya msingi yanayohusiana na hayo, pamoja na ufadhili wa ugaidi.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad