
Serikali ipo mbioni kuanzisha Mpango wa Mageuzi ya Kijani utakaolenga kukijanisha Tanzania na kusafisha Mazingira ambao programu zake zitasambaa nchi nzima ikiwa moja ya njia ya kuhifadhi na utunzaji wa Mazingira.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Hamad Yussuf Masauni ameyasema hayo wakati wa ziara yake ya kikazi mkoani Mwanza, Machi 13, 2026 ambapo amesisitiza kuwa kila mmoja anaowajibu wa kulinda mazingira na Serikali itawapongeza wale wanaozingatia sheria za Uhifadhi na Utunzaji wa Mazingira na pia kuwachukulia hatua kali wanaoharibu Mazingira.
Amesema Mpango huo umegusa takribani maeneo yote ili kuhakikisha Mazingira yanakuwa safi na salama hususani katika upandaji miti ili kuepuka majangwa na kuongeza bustani, usafishaji wa miji, ulinzi wa vyanzo vya maji, utakaochangia kwa kiasi kikubwa kupunguza maradhi.
Aidha, Mhe. Waziri amewataka wawekezaji na watanzania wote kulinda Mazingira huku akisisitiza kuwa Serikali haitasita kuwachukulia hatua wale wote wanaosababisha uharibifu wa Mazingira kwa namna yoyote.
"Tunawajibu wa kulinda Mazingira Ili Mazingira yawe mazuri ni lazima sisi tuyalinde, na ili yawe mabaya ni lazima sisi tuyaharibu, Serikali inawajibu wa kuhakikisha watanzania wanaendelea kutunza Mazingira, na katika kuhakikisha hilo, Serikali haitasita kuwachulia hatua wale wote wanaoharibu Mazingira kwa namna Moja ama nyingine.
Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhe. Said Mtanda amesema Ofisi yake inafanya juhudi kuhakikisha Mazingira yanalindwa na kutunzwa katika mkoa huo licha ya changamoto zinazoikabili Ofisi hiyo hasa katika udhibiti wa Kelele chafuzi za Maeneo ya kumbi za starehe.
Mhe. Mtanda ameiomba Ofisi ya Makamu wa Rais kuendelea na jitihada za kuondoa Gugumaji katika Ziwa Victoria ili kulinda samaki na ikolojia ya mazalia ya majini akielezea kuwa shughuli za uvuvi ni muhimili muhimu kwa wananchi wa Mkoa wa Mwanza.
Amesema asilimia 53 ya eneo la Mkoa wa Mwanza linazungukwa na maji hivyo linahitaji uangalizi wa kipekee katika uhifadhi wa mazingira hususan vyanzo vya maji na mwambao wa Ziwa Victoria ili kuhakikisha rasilimali za uvuvi zinaendelea kuwepo.
Katika hatua nyingine Mhe. Masauni pia aliweza kutembelea eneo lililoathirika na mafuriko hivi karibuni na kuharibu miundombinu mbalimbali ikiwemo barabara, nyumba na mali za wananchi.












No comments:
Post a Comment