MGONJWA ALIYEPATIWA RUFAA AZUILIWA HOSPITALI YA BENJAMIN MKAPA KWA DENI LA SH.1,175,000 - SINGIDANI BLOG

Habari za Hivi Punde

Post Top Ad

Thursday, 19 March 2026

MGONJWA ALIYEPATIWA RUFAA AZUILIWA HOSPITALI YA BENJAMIN MKAPA KWA DENI LA SH.1,175,000

Muonekano wa jengo la Utawala Hospitali ya Benjamin Mkapa jijini Dodoma

..................................................

Na  Dotto Mwaibale Dodoma


Mgonjwa Ester John Furaha (32) hali yake ni tete na hajiwezi kwa lolote baada ya kupata rufaa kwenda Taasisi ya Kansa Ocean Road Jijini Dar es Salaam kwa ajili ya matibabu amezuiliwa kutoka Hospitali ya Benjamin Mkapa Jijini Dodoma mpaka atakapolipa deni la Sh. 1,175,000 anazodaiwa baada ya kupatiwa matibabu.


Rufaa hiyo alipewa Machi 18, 2026 lakini kutokana na deni hilo kitengo cha huduma za ustawi wa jamii katika hospitali hiyo kimemzuia asiondoke mpaka atakapolipa deni hilo.


Mgonjwa huyo mwenye namba ya matibabu DM-00280606 yupo wodi namba mbili chumba namba 8 akiwa na mdogo wake Celina John Furaha anayemuuguza huku wakiishi kwa kutegemea kupewa msaada wa chakula na mahitaji mengine na ndugu za wagonjwa wengine wanapofika kuwaona jamaa zao waliolazwa hospitalini hapo.


Akizungumzia hali waliyo nayo Celina amesema hajui cha kufanya, dada yake hali yake ni mbaya na hawajui deni hilo watalilipaje kwani hawana fedha na hata jinsi ya kwenda Dar es Salaam kupata matibabu.


“Tumekuwepo hapa hospitali kwa zaidi ya miezi mitatu tukitokea Hosptali ya Makiungu wilayani Ikungi mkoani Singida ambapo walibaini kuwa anasumbuliwa ugonjwa wa kansa na tumelipia matibabu yake zaidi ya Sh. Milioni 3.2 tumeishiwa na hatuna msaada wowote,” alisema Celina huku akiwa na huzuni.


Celina alisema Machi 18, 2026 majira ya saa 10 jioni alikwenda ofisi ya huduma ya ustawi wa jamii hospitalini hapo ambapo aliambiwa mgonjwa hataruhusiwa kuondoka mpaka alipe deni hilo na kuwa wapo wodini na dada yake hapati matibabu yoyote na hali yake ni mbaya  kwani anatapika na hawezi hata kuinuka zaidi ya kulala wakati wote.


Akifafanua kuhusu deni hilo alisema Afisa mmoja wa kitengo hicho cha huduma ya ustawi wa jamii alimuandikia kuwa matibabu yake gharama ilikuwa ni Sh.685,000, gharama za kitanda Sh.490,000 na Sh.70,000 jumla kuu ikiwa ni Sh.1,175,000.


Jitihada za kumpata Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Benjamin Mkapa (BMH), Prof. Abel Makubi ili kuzungumzia suala hilo hazikuweza kuzaa matunda.


Hata hivyo Afisa Habari wa Hospitali hiyo, Ludovick Kazoka akizungumzia suala hilo alisema kuhusu deni hilo mgonjwa huyo anapaswa kwenda ofisi ya huduma ya ustawi wa Jamii ambao watafanya tathimini na kama itaonesha kweli hawezi kulipa wataona namna ya kufanya na kuwa huo ndiyo utaratibu uliopo.


Mwaka jana katika Uzinduzi wa kampeni za Chama Cha Mapinduzi (CCM), kitaifa uliofanyika Agosti 28, 2025, katika Viwanja vya Tanganyika Packers, Kawe jijini Dar es Salaam.


, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye alikuwa mgombea nafasi ya urais wakati akihutubia moja ya ahadi yake ilikuwa ni kupiga marufuku kuzuia miili ya marehemu ambayo ilikuwa ikizuiliwa kwa kushindwa kuilipia katika hospitali mbalimbali lakini  kwa wagonjwa kama Ester Furaha inapaswa pia kuwekwa muongozo wa wazi ili kuondoa hali hiyo ya kuzuiliwa wakati alipaswa kukimbizwa hospitalini alikopewa rufaa jambo litakalosaidia kuokoa maisha yake badala ya kumzuia wodini bila ya kumpatia matibabu na pengine kusababisha kifo kwa mgonjwa  husika.


Taarifa hii imeandaliwa na Dotto Mwaibale simu namba 0754362990.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad