𝐖𝐀𝐙𝐈𝐑𝐈 𝐖𝐀 𝐅𝐄𝐃𝐇𝐀 𝐍𝐀 𝐑𝐂 𝐃𝐎𝐃𝐎𝐌𝐀 𝐖𝐀𝐀𝐍𝐆𝐀𝐙𝐈𝐀 𝐅𝐔𝐑𝐒𝐀 𝐙𝐀 𝐊𝐈𝐔𝐂𝐇𝐔𝐌𝐈 𝐃𝐎𝐃𝐎𝐌𝐀 - SINGIDANIBLOG

Habari za Hivi Punde

Post Top Ad

Thursday, April 30, 2026

𝐖𝐀𝐙𝐈𝐑𝐈 𝐖𝐀 𝐅𝐄𝐃𝐇𝐀 𝐍𝐀 𝐑𝐂 𝐃𝐎𝐃𝐎𝐌𝐀 𝐖𝐀𝐀𝐍𝐆𝐀𝐙𝐈𝐀 𝐅𝐔𝐑𝐒𝐀 𝐙𝐀 𝐊𝐈𝐔𝐂𝐇𝐔𝐌𝐈 𝐃𝐎𝐃𝐎𝐌𝐀

Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (kulia), akikabidhiwa Mkakati wa Maendeleo ya Utalii kwa Mkoa wa Dodoma ambao unaongoza mkoa katika kuendeleza sekta yake ya utalii, na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule, wakati alipotembelea Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, kujitambulisha, baada ya hivi karibuni kuteuliwa na Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kuwa Waziri wa Fedha.
-----------------------------

 

Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), amesema kuwa Mkoa wa Dodoma una fursa nyingi za kiuchumi na kijamii katika sekta mbalimbali ikiwemo kilimo, biashara, utalii na madini ambazo zikiendelezwa na kuchangamkiwa ipasavyo zitakuwa na mchango mkubwa katika maendeleo ya nchi na watu wake.

 

Mhe. Balozi Omar amesema hayo alipomtembelea Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule, ofisini kwake jijini Dodoma kwa ajili ya kujitambulisha, baada ya hivi karibuni kuteuliwa na Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kuwa Waziri wa Fedha.

 

Alisema kuwa Mkoa wa Dodoma uko katikati ya nchi na unaweza kutumika ipasavyo kama kitovu ama kituo cha biashara kwa kuunganika na mikoa mingine kimkakati ikiwemo bandari kavu kwa ajili ya kuhifadhi na kusafirisha makontena na bidhaa nyingine Kwenda maeneo mengine ya ndani na nje ya nchi.

 

“Lakini pia tuna fursa kubwa ya kilimo ambayo imeajiri watanzania wengi zaidi, mazao tofauti, fursa ya utalii lakini kubwa zaidi ni fursa ya madini ambapo mkoa wa Dodoma umebarikiwa kuwa miongoni mwa mikoa yenye utajiri wa madini ambayo yakichanganywa na madini kutoka mikoa mingine yakaongezewa thamani, wananchi wanaweza kunufaika kwa kiasi kikubwa na fursa hizo” alisema Mhe. Balozi Omar.

 

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule, alimweleza Mhe. Balozi Omar kuwa mkoa huo sasa umepiga hatua kubwa kimaendeleo na kwamba mikakati mbalimbali inaelekezwa katika kukuza zaidi biashara, utalii, sekta ya madini, kilimo, pamoja na kuimarisha utoaji wa huduma za jamii.

 

Alitoa wito kwa wadau mbalimbali kutoka Sekta ya Umma na Sekta Binafsi kuwekeza mkoani humo ikiwemo ujenzi wa vituo vya Kimataifa vya mikutano, hoteli za hadhi ya nyota tano, pamoja na kuchakata madini ambayo alisema yako lukuki mkoani mwake.

 

Katika Kikao hicho, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma aliambatana na Katibu Tawala wa mkoa huo, Dkt. Khatibu Kazungu.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad