𝐒𝐄𝐑𝐈𝐊𝐀𝐋𝐈 𝐘𝐀𝐉𝐈𝐏𝐀𝐍𝐆𝐀 𝐊𝐔𝐒𝐎𝐆𝐄𝐙𝐀 𝐇𝐔𝐃𝐔𝐌𝐀 𝐁𝐈𝐍𝐆𝐖𝐀 𝐙𝐀 𝐌𝐎𝐘𝐎 𝐊𝐀𝐑𝐈𝐁𝐔 𝐍𝐀 𝐖𝐀𝐍𝐀𝐍𝐂𝐇𝐈 - SINGIDANIBLOG

Habari za Hivi Punde

Post Top Ad

Thursday, April 30, 2026

𝐒𝐄𝐑𝐈𝐊𝐀𝐋𝐈 𝐘𝐀𝐉𝐈𝐏𝐀𝐍𝐆𝐀 𝐊𝐔𝐒𝐎𝐆𝐄𝐙𝐀 𝐇𝐔𝐃𝐔𝐌𝐀 𝐁𝐈𝐍𝐆𝐖𝐀 𝐙𝐀 𝐌𝐎𝐘𝐎 𝐊𝐀𝐑𝐈𝐁𝐔 𝐍𝐀 𝐖𝐀𝐍𝐀𝐍𝐂𝐇𝐈

Meneja wa Rasilimali watu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group Abdulrahman Muya akimkabidhi Waziri wa Kazi Mhe. Deus Clement Sanga zawadi ya mashine ya BP, RBG na Thermometer kama sehemu ya kampeni ya kuhamasisha jamii kujua namba zao za afya alipotembelea banda la taasisi hiyo lililopo kwenye maonesho ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi yanayofanyika katika Viwanja vya Shule ya Msingi Mji Mwema Mjini Njombe.
Daktari bingwa wa magonjwa yatokanayo na kazi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group Elius Birago akimueleza  Waziri wa Kazi Mhe. Deus Clement Sanga huduma zinazotolewa na Taasisi hiyo wakati wa maonesho ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi yanayofanyika katika viwanja vya Shule ya Msingi Mji Mwema Mjini Njombe.
Daktari bingwa wa magonjwa yatokanayo na kazi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group Elius Birago akimpa zawadi Mganga Mkuu wa Mkoa wa Njombe Dkt. Juma Mfanga alipotembelea banda la Taasisi hiyo wakati wa maonesho ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi yanayofanyika katika viwanja vya Shule ya Msingi Mji Mwema Mjini Njombe.
Afisa Uuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group Happiness Shirima akitoa elimu kuhusu magonjwa ya moyo na namna ya kujikinga na magonjwa hayo kwa wanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Lunyanywi walipotembelea banda la Taasisi hiyo wakati wa maonesho ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi yanayofanyika katika viwanja vya Shule ya Msingi Mji Mwema Mjini Njombe.
-----------------------------------------

Na Mwandishi Maalumu – Njombe

30/04/2026 Serikali kupitia Wizara ya Kazi kwa kushirikiana na Wizara ya Afya imeahidi kuweka mikakati madhubuti ya kuiwezesha Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kufikisha huduma bingwa na bobezi za uchunguzi na matibabu ya moyo katika mikoa yote nchini hatua inayolenga kusogeza huduma hizo karibu zaidi na wananchi.


Hayo yamesema jana na Waziri wa Kazi  Mhe. Deus Clement Sanga alipotembelea banda la JKCI katika maonesho ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi yanayoendelea katika viwanja vya Shule ya Msingi Mji Mwema mjini Njombe.


Akiwa katika banda hilo Waziri Sanga alipata fursa ya kujionea huduma mbalimbali zinazotolewa na wataalamu wa JKCI pamoja na mwitikio mkubwa wa wananchi waliojitokeza kupima afya zao.


Mhe. Sanga alisema mahitaji ya huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo yanaendelea kuongezeka kutokana na kasi ya magonjwa yasiyoambukiza hivyo kuna umuhimu mkubwa wa kuhakikisha huduma hizo zinawafikia wananchi kwa urahisi zaidi.


“Mwitikio mkubwa wa wananchi wa Njombe ni ishara tosha ya uhitaji wa huduma hizi za uchunguzi na matibabu ya moyo na kuhimiza JKCI kutumia fursa hiyo kufanya tathmini ya kina itakayosaidia kupanga mikakati ya kufikisha huduma hizo kwa upana zaidi”.


“Kaulimbiu ya mwaka huu inayozungumzia umuhimu wa mazingira bora ya kisaikolojia mahali pa kazi ina uhusiano wa moja kwa moja na afya ya moyo, kwani msongo wa mawazo unaweza kuchangia ongezeko la magonjwa ya shinikizo la damu na matatizo ya moyo”, alisema Mhe. Sanga.


Waziri huyo wa Kazi aliwapongezata wataalamu wa JKCI kwa kutoa elimu ya jinsi ya kujikinga na magonjwa ya moyo katika maonesho hayo huku akisema imewasaidia wafanyakazi na wananchi kuelewa namna ya kujikinga na magonjwa yasiyoambukiza kupitia mabadiliko ya mtindo wa maisha.


Kwa upande wake Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo kutoka JKCI, Moses Manumbu alisema mwitikio wa wananchi wa Njombe umekuwa mkubwa na wenye hamasa ya kujua hali zao za afya.


Dkt. Manumbu alieleza kuwa watu wengi wamejitokeza kupima moyo na kupata ushauri wa kitaalamu  huku wengi wao wakiomba huduma hizo ziendelee kutolewa hata baada ya maonesho hayo kukamilika.


“Tumebaini kuwa kuna watu wengi wanaishi na magonjwa yasiyoambukiza bila ya wao kufahamu  hali inayoonyesha umuhimu wa uchunguzi wa mara kwa mara. Wananchi wameonesha uhitaji mkubwa wa huduma hizi kuendelea kufikishwa hapa Njombe angalau mara moja au mbili kwa mwaka”,  alisema Dkt. Manumbu.


Naye Paulo Mbando mkazi wa Njombe alisema amenufaika na huduma hizo kwa kupima afya ya moyo bure pamoja na kupata elimu ya mtindo bora wa maisha kutoka kwa wataalamu wa JKCI, huduma hizo ni matokeo ya juhudi za Serikali ya awamu ya sita katika kuboresha huduma za afya na kuwajali wananchi wake.


“Leo nimepata fursa ya kupima moyo bila gharama na kupewa elimu muhimu itakayosaidia kulinda afya yangu. Hii ni hatua kubwa kwetu wananchi, naamini kupitia elimu hii nitaweza kujilinda nisipate magonjwa ya moyo”, alisema Paulo.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad