KATA YA UNYIANGA MANISPAA YA SINGIDA YATUMIA BILIONI 1 KUTEKELEZA MIRADI - SINGIDANIBLOG

Habari za Hivi Punde

Post Top Ad

Friday, May 26, 2023

KATA YA UNYIANGA MANISPAA YA SINGIDA YATUMIA BILIONI 1 KUTEKELEZA MIRADI

 

Diwani wa Kata ya Unyianga, Geofrey Mdama, akizungumza wakati akitoa taarifa ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwa wajumbe wa kamati ya siasa ya Wilaya ya Singida baada ya kutembelea na kukagua miradi hiyo juzi.

 

Na Dotto Mwaibale, Singida

ZAIDI ya Sh. Bilioni 1.1 zimetumika kwa ajili ya kukamilisha miradi mbalimbali ya maendeleo katika Kata ya Unyianga, Manispaa ya Singida.

Hayo yamebainishwa na Diwani wa kata hiyo, Geofrey Mdama wakati akitoa taarifa ya utekelezaji wa miradi hiyo mbele ya wajumbe wa kamati ya siasa ya Wilaya ya Singida wakiongozwa na Mwenyekiti wa kamati hiyo ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wa wilaya hiyo, Lusia Mwiru wakati ilipokuwa ikikagua miradi hiyo juzi.

Alisema shughuli za miradi hiyo ni utekelezaji wa ilani ya chama hicho ya 2020/ 2025 yenye nia ya kuwaletea wananchi maendeleo.

Mdama alisema matumizi ya fedha hizo ni ujenzi wa barabara, zahanati na madarasa ya shule shikizi, sekondari na Msingi.

Alisema katika ujenzi wa barabara ya Unyianga hadi Mtamaa fedha zilizotumika ni Sh.Milioni 168 ambapo barabara ya kutoka Unyianga kwenda Mwankoko zimetumika Sh.Milioni 378.

Alitaja barabara nyingine kuwa ni ya Utalii kupitia Unyianga B ambayo imetumia Sh. Milioni 146 sambamba na barabara ya Sima kwenda Unyianga B.

Akizungumzia kuhusu ujenzi wa madarasa na zahanati alisema walipokea Sh.Milioni 50 kwa ajili ya ujenzi wa zahanati ya Unyianga ambayo ujenzi wake umekwisha kamilika.

Aidha, Mdama alisema walipokea Sh. Milioni 25 kwa ajili ya ujenzi wa shule Shikizi na Sh.Milioni 25 nyingine kwa ajili ya ujenzi wa madarasa mawili katika Shule ya Msingi Unyianga.

Alitaja fedha nyingine walizopokea ni Sh.Milioni 75 kwa ajili ya ujenzi wa madarasa manne ya Shule ya Sekondari ya Unyianga.

Alisema wamepokea Sh.Milioni 263 kwa ajili ya ujenzi wa madarasa ya shule za sekondari, msingi na uanzishwaji wa shule shikizi ya Unyianga B.

Alitaja miradi mingine ambayo ipo katika hatua za mwisho kukamilika ni umeme,maji na zahanati ambayo itaanza kutoa huduma haraka iwezekanavyo.

Mdama alitumia nafasi hiyo kumshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha hizo ambazo zimeleta maendeleo makubwa katika kata hiyo.

Aidha, kwa nafasi ya pekee ana mshukuru Mbunge wa Singida Mjini Musa Sima kwa mchango wake mkubwa pamoja na uongozi mzima wa Manispaa ya Singida na wananchi kutokana na ushirikiano wanaoutoa kufanikisha maendeleo katika kata hiyo.

Mwenyekiti wa kamati hiyo, Lucia Mwiru alipongeza uongozi wa kata hiyo kwa utekelezaji wa miradi hiyo kwa haraka na kwa ubora wa kiwango cha juu ambapo pia alitumia nafasi hiyo kutoa nasaa kwa wazazi na walezi kusimamia maadili na malezi kwa watoto wao.

Aidha, Mwiru alihimiza suala zima la uhai wa chama pamoja na usajili kwa wingi wanachama kwa njia ya kielektroni.


Wananchi wakifurahia baada ya ukaguzi wa miradi hiyo.


Shamra shamra zikiendelea.



No comments:

Post a Comment

Post Top Ad