Na Dotto Mwaibale, Singida
MKUU wa Mkoa wa Singida, Peter Serukamba amesema Rais Dkt. Samia Suluhu
Hassan ametoa mbolea ya ruzuku na mbegu za alizeti kwa ajili ya kuwasaidia
wakulima hivyo hata kuwa tayari kumuona mtu akikwamisha mbolea hiyo kuwafikia
wakulima na watakao thubutu kufanya hivyo watashughulika nao bila ya kuwaonea huruma.
Serukamba ameyasema hayo Disemba 4, 2023 wakati akizungumza na maafisa
watendaji, maafisa ugani, wenyeviti wa vijiji wa Wilaya ya Iramba katika kikao
kazi kilichohudhuriwa na viongozi mbalimbali akiwepo Mkuu wa wilaya hiyo,
Suleiman Mwenda chenye lengo la kuhamasisha kilimo.
“Naombeni watendaji wa kata, vijiji, maafisa kilimo, wagani nisiende kijiji
chochote nikaambiwa moja ya kero yao hawajapata mbolea huo ugomvi utakuwa
mkubwa sana,” alisema Serukamba.
Aliwataka maafisa hao kwenda kwenye maeneo yao wanayotoka kuitisha mkutano
ya wananchi na kuwasajili majina yao ili waweze kupatiwa mbolea na kuwa maeneo
yatakayokuwa hayana mbolea watendaji wake watashughulikiwa.
Aidha, alimtaka Afisa Kilimo wa wilaya hiyo kutoka ofisi kwenda kwa wakulima
kuona kama mbolea imewafikia badala ya kufanya kazi hiyo kwa kutumia simu akiwa
amekaa ofisini.
Serukamba alisema katika msimu huu wa kilimo wilaya hiyo imeanzisha
mashamba mapya ekari 3500 kwa ajili ya kilimo cha zao la alizeti.
Alisema lengo la mkoa ni kuongeza uzalishaji wa zao hilo kutoka asilimia 50 kwa msimu uliopita hadi
kufikia asilimia 70 kwa msimu huu wa 2023/ 2024.
“Mkoa wa Singida ni wa tatu kutoka mwisho kwa uzalishaji wa mazao sasa
tunapaswa kuongeza jitihada tutoke hapa tulipo tupande jambo ambalo
linawezekana kwani Serikali imekwisha maliza kazi yake ya kutuletea mbolea ya
ruzuku na mbegu ya alizeti ambayo kwa msimu huu itatolewa kwa kulipia fedha
taslimu na si kwa mkopo,” alisema Serukamba.
Mkuu wa Wilaya ya Iramba, Suleiman Mwenda alimweleza Serukamba kwamba
maagizo yake yote aliyotoa yatatekelezwa na akawataka watendaji wote kujipanga
vilivyo kwani mapema wiki ijayo ataanza ziara katika kata zote ya kwenda kuona
utekelezaji wa usambazaji wa mbolea.
“Suala hili leo sio mara ya kwanza kwani tulilipitisha katika kongamano letu
la msimu wa kilimo tulilolifanya sasa mtatushangaza iwapo mtashindwa
kulitekeleza,” alisema Mwenda.Mkuu wa Wilaya ya Iramba, Suleimani Mwenda, akizungumza kwenye kikao hicho.
Afisa Kilimo Wilaya ya Iramba, Malietha Kasongo, akizungumza kwenye kikao hicho.







No comments:
Post a Comment