Katibu Mkuu wa Umoja wa Wanamuziki Tanzania (TAMUFO), Stella Joel na viongozi wengine wa umoja huo wakimuombea Mwanamuziki Mkongwe Zahir Ally Zorro walipomtembelea hivi karibuni nyumbani kwake Kigamboni jijini Dar es Salaam kumjulia hali kutokana na maradhi yanayomsumbua.
Na Kulwa Mwaibale
UMOJA wa Wanamuziki Tanzania (TAMUFO)
umewakumbuka kwa kuwapa fedha wakongwe wa muziki wa dansi nchini, Zahir Ally Zorro na Boniface Kikumbi Mwanza
Mpango 'King Kikii' wanaopitia
changamoto za maradhi ili ziwasaidie kwa chochote.
Tukio hilo lilijiri Novemba 25, 2023 ambapo
viongozi wa TAMUFO, Stella Joel ambaye ni Katibu, Pastor Lucy Wilson wa Kanisa
la Spring of Life Mision la Tabata ambaye pia ni Mkurugenzi wa Idara ya Gospo
TAMUFO na Frank Richard, Mlezi wa TAMUFO walifika kumjulia hali King Kikii nyumbani
kwake Mtoni Kwa Aziz Ally Temeke.
Stella akizungumza na mgonjwa huyo ambaye afya
yake bado haijaimarika baada ya kufanyiwa upasuaji hivi karibuni kabla ya
kwenda Kigamboni nyumbani kwa Zahir Zorro, alisema waliamua kuwafariji
wanamuziki hao kwa sababu ya mchango walioutoa katika Taifa letu kupitia tasnia
ya muziki.
"King Kikii mzee wa kitambaa cheupe na Zahir
Ally Zorro, kupitia muziki wamelifanyia makubwa taifa letu, kuelimisha na
kuburudisha, tungo zao zinaujumbe utakaoishi milele," alisema Stella.
Aliongeza kuwa, wanamuziki hao ni wenzao tangu
TAMUFO ilipoasisiwa ambapo King Kikii ni mmoja wa viongozi wake.
Alisema kuwa wakiwa Arusha walisikia kuhusu
changamoto za maradhi yanayowasibu wanamuziki.hao walioshirikiananao.kwenye
mikutano, matamasha sehemu mbalimbali, walipofika Dar es Salaam wameona vyema
kufika kuwapa pole.
Pastor Lucy aliyeongoza maombi ili Mungu awajalie
afya njema wanamuziki hao, alisema ni mpenzi wa nyimbo za wanamuziki hao tangu
zamani kwa sababu zinaelimisha na kuburudisha na baadhi zinaonesha walivyo
wazalendo wa nchi yao ya Tanzania..
"Wakongwe hawa wa muziki wamelifanyia mengi
taifa letu kupitia muziki, nyimbo ya fungua njia kitoto chaanzatambaa, Kitambaa
Cheupe, Cleopatra na Wazazi ya Zahir Zorro aliyoitunga baada ya vita vya Tanzania
na Uganda vilipoisha na zingine nazipenda sana," alisema Pastor Lucy.
Aliongeza kwa maombi ambayo waliyafanya Mungu
atawaponya wanamuziki hao.
Akizungumza nyumbani kwa Zorro, Dkt. Frank Richard alisema TAMUFO itakuwa sambamba na
wanamuziki hao katika kipindi chote cha udhaifu wa afya zao hadi watakapopona
na kurejea kwenye shughuli zao za muziki na zingine.
"Kwa kuwathamini kama wenzetu na mchango
wenu mkubwa mlioutoa katika nchi yetu kupitia muziki, sisi TAMUFO tutakuwa
nanyi kwenye kipindi cha changamoto ya maradhi mnachopitia," alisema mlezi
huyo wa TAMUFO.
King KikiI aliwashukuru viongozi hao kwa kufika
kumjulia hali na kumpa fedha alizosema zitamsaidia katika kipindi cha maradhi
anachopitia.
Aliwashukuru watanzania akiwemo Waziri Mkuu Kasim
Majaliwa waliomsaidia baada ya kuguswa na changamoto ya maradhi yake, amewaomba
waendelee kumsaidia kwani anahitaji fedha ili akatibiwe nje ya nchi.
Kwa upande wake Zahir Zorro, ameishukuru TAMUFO
Kwa upendo wao wa kwenda kumjulia hali, pia amemshukuru Mkurugenzi wa Shirika
la Habari Tanzania (TBC), Ayub Ryoba kumkatia Bima ya afya inayomsaidia kupata
matibabu.
Amesema kwa sasa anaendelea vizuri isipokuwa
mwili.hauna nguvu.
Aliongeza kuwa alianza kuugua muda mfupi baada ya
kifo cha binti yake Maunda na kufikia kuwa na hali mbaya.
Ameishukuru serikali chini ya Rais Dkt. Samia
Suluhu kwa yote inayoyafanya kwa wasanii.na taifa kwa jumla.
Wanamuziki hao wanatarajia kufyatua vibao vya
Gospo kumshukuru Mungu aliyesimamanao kwenye kipindi kigumu cha kuugua kwao,
TAMUFO imeahidi kushirikiananao kurekodi nyimbo hizo.
Viongozi hao wa TAMUFO wakimuombea mwanamuziki, Boniface Kikumbi Mwanza Mpango 'King Kikii' walipokwenda kumjulia hali nyumbani kwake Mtoni kwa Azizi Ally kutokana na maradhi yanayomsumbua.
Mwanamuziki Mkongwe Zahir Ally Zorro akizungumza na viongozi hao wa TAMUFO (hawapo pichani) walipo mtembelea kumjulia hali.
Viongozi hao wa TAMUFO wakimfanyia maombi, Mwanamuziki Mkongwe Zahir Ally Zorro .









No comments:
Post a Comment