WIZARA YA AFYA YAITAKA MSD KUITAMBUA BIMA YA AFYA KWA WOTE - SINGIDANIBLOG

Habari za Hivi Punde

Post Top Ad

Monday, 11 December 2023

WIZARA YA AFYA YAITAKA MSD KUITAMBUA BIMA YA AFYA KWA WOTE

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Afya Dk.Grace Magembe, akifungua kikao kazi cha Bohari ya Dawa (MSD) na wateja wake wakubwa.kilichofanyika jijini Dodoma Disemba 10, 2023.

..................................................................

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

 

WIZARA ya Afya imeitaka Bohari ya Dawa (MSD) kuitambua Bima ya Afya kwa wote na kuzingatia upatikanaji wa bidhaa za afya, ubora na bei zilizo katika muongozo wa matibabu wa Serikali.

 Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Afya Dk.Grace Magembe ametoa maagizo hayo Disemba 10, 2023     jijini Dodoma wakati akifungua kikao kazi cha MSD na wateja wake wakubwa. 

Dk.Magembe alisema  MSD iwahudumie wananchi kulingana na mahitaji ya taasisi zote za afya na  kuangalia mifumo ya utoaji huduma inavyoweza kukidhi mahitaji ya Bima ya Afya kwa wote.

Aidha, Naibu Katibu mkuu huyo alizitaka taasisi za afya kuangalia upya mifumo ya utoaji huduma lengo likiwa kukidhi mahitaji ya Bima ya Afya kwa wote.

“Tuangalie upya mifumo yetu ya utoaji huduma namna inavyoweza kubadilika ili kukidhi mahitaji ya Bima ya Afya kwa wote.Tusisumbue wananchi, muwasiliane wenyewe kwa kuwa wao wanataka hudum,”alisema.

Dk.Mgembe alisema muswada wa Bima ya Afya umepitishwa na Bunge hivyo kinachotakiwa sasa ni kuufanyia kazi kwa kutunga kanuni kwakushirikiana na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Ofisi ya Waziri Mkuu,Wizara ya Fedha,Ikulu na wadau wengine.

Naye Mfamasia  Mkuu wa Serikali Daud Msasi alisema, kikao hicho kitajadili changamoto na kutafuta  suluhuhisho ili MSD iweze kuwahudumia wateja wakubwa kwa bidhaa wanazozihitaji.

“Tumeshiriki kikao cha MSD ambacho kinaunganisha wateja wake wakubwa kutoka katika hospitali kubwa lengo ni kuboresha huduma za kuwahudumia wananchi na kupata bidhaa wanazohitaji,..

Alisema  changamoto iliyopo inatokana na utendaji ni kwamba wateja hawa wanapokosa bidhaa MSD huagiza bidhaa zao  nje ya nchi ambapo ni kinyume na sheria .

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa MSD Mavere Tukai alisema, lengo la kuwakutanisha wateja wakubwa ni kwasababu  mahitaji yao ya dawa ni makubwa tofauti na hospitali nyingine.

Alitaja wateja ambao wamekutana nao kuwa ni  Hospitali ya Kibong’oto, Muhimbili, Ocean Road, Benjamini Mkapa na Hospitali ya Mirembe.

“MSD inamikakati ya kuongeza zaidi wateja wakubwa kwa kuweka utaratibu mzuri kwa ajili ya kufanya biashara nao," alisema Tukai...

Alisema wanatengeneza mkakati wa pamoja na kuanza kutoa huduma kwa wananchi kwa ufanisi mkubwa..

Awali Mkurugenzi Mtendaji wa Mfuko wa Bima ya Afya (NHIF) Benard Konga  alisema, Rais Dk.Samia Suluhu Hassan  amesaini sheria ya Bima ya Afya kwa wote na utekelezaji wake  unaanza hivi karibuni.

“Leo tumeshiriki katika kikao kilichoandaliwa na MSD ambapo kinalengo la kutafuta suruhu ya pamoja  kuhusu suala zima la upatikanaji wa dawa nchini.

Aliongeza kuwa ili kutimiza adhma ya Serikali ya Awamu ya Sita ya Bima ya Afya kwa wote lazima wakae pamoja na  kuwa na mikakati ambayo  itafanya adhma hiyo itimie pasipo vikwazo vyovyote,

Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Temeke Dk. Joseph Kimaro alisema kumekuwa na maendeleo makubwa kwa MSD  hasa katika kipindi hiki cha uongozi wa Serikali ya Awamu ya Sita.

“Lengo la kikao hiki ni kuimarisha ushirikiano katika utoaji huduma za afya ambapo inaenda sambamba na uwepo wa dawa na vifaa tiba jukumu ambalo imepewa MSD.Mkurugenzi Mkuu wa MSD Mavere , akichangia jambo kwenye kikao hicho.

 Mfamasia  Mkuu wa Serikali Daud Msasi , akizungumza kwenye kikao hicho.
 

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad