ORYX, DKT. MWIGULU WA MUUNGA MKONO RAIS SAMIA UTUNZAJI MAZINGIRA - SINGIDANIBLOG

Habari za Hivi Punde

Post Top Ad

Sunday, 7 January 2024

ORYX, DKT. MWIGULU WA MUUNGA MKONO RAIS SAMIA UTUNZAJI MAZINGIRA

Wanawake Wajasiriamali wa Wilaya ya Iramba ambao wanajishughulisha na Mama Lishe wakiwa wamebeba mitungi ya gas yenye majiko baada ya kukabidhiwa Januari 6, 2024. Mitungi hiyo imetolewa na Kampuni ya Oryx Tanzania kupitia Mbunge wa Jimbo la Iramba Magharibi Dkt. Mwigulu Nchemba ili kukabiliana na uharibifu wa mazingira.

.....................................................

Na Dotto Mwaibale, Iramba

JITIHADA za Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan za kutunza mazingira zimeendelea kuungwa mkono na wadau mbalimbali ambapo Kampuni ya Gas ya Oryx Tanzania kupitia Mbunge wa Jimbo la Iramba Magharibi, Dkt. Mwigulu Nchemba ambaye pia ni Waziri wa Fedha kutoa mitungi ya gas yenye majiko yake kwa Mama lishe na Baba lishe zaidi ya 700 kutoka maeneo mbalimbali ya Wilaya ya Iramba mkoani Singida.

Mkuu wa Wilaya ya Iramba, Suleiman Mwenda akizungumza katika hafla ya makabidhiano ya mitungi hiyo iliyofanyika Januari 6, 2024 ukumbi wa mikutano wa Halmashauri ya Wilaya ya Iramba    kwa niaba ya Dkt. Nchemba alisema mitungi hiyo imetolewa na mbunge huyo kwa ajili ya kuunga mkono jitihada za Rais Samia za utunzaji wa mazingira kazi ambayo aliianza tangu alipokuwa  makamu wa Rais.

"Mhe. Mbunge alituita Dodoma mimi na Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya Innocent Msengi na kutueleza kuwa amefanya mazungumzo na viongozi wa Kampuni ya Oryx gas Tanzania ambao watatusaidia kutupatia mitungi ya gas lengo kuu likiwa ni kuziunga mkono juhudi za Rais Samia alizozianza tangu akiwa Makamu wa Rais za kulinda na  kutunza mazingira," alisema Mwenda.

Alisema kulingana na kumbukumbu za wanamazingira hapa nchini zinaonesha kuwa uharibifu mkubwa wa mazingira unaotokea unatokana na ukataji wa miti mikubwa inayohitajika kwa ajili ya nishati ya kupikia (kuni)

Alisema takwimu hizo zinatishia na kuonesha wazi kuwa tukiendelea na  utaratibu huo wa ukataji miti kwa ajili ya nishati hiyo ya kupikia ifikapo miaka 10 hadi 20 ijayo nchi yetu itabadilika na kuwa jangwa.

Mwenda alisema kutokana na hali hiyo Dkt.Nchemba ameziiunga mkono juhudi hizo za Rais na kuwataka kupande miti ya kutosha kwa ajili ya kulinda tabia nchi na ndio sababu iliyomfanya azungumze na viongozi wa Kampuni ya Oryx Tanzania ambao walikubali kumpa mitungi ya gas 700 na wao wakatoa mingine 200 na kufanya jumla ya mitungi kuwa 900 ambayo itatumiwa na wananchi wa wilaya hiyo badala ya kutumia mkaa na kuni kwani nao wameguswa na athari za uharibifu wa mazingira.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkazi wa Kampuni ya Oryx Tanzania, Benoit Araman alisema kuanzia mwezi Julai, 2021 kampuni hiyo imekuwa mstari wa mbele kutekeleza maelekezo ya Serikali waliyoyapokea kutoka kwa Rais kuwa ifikapo mwaka 2023 wananchi wote wa Tanzania wawe wanatumia nishati safi ya kupikia.

Alisema kupitia mipango hiyo Oryx imepanga kutokomeza kabisa matumizi ya nishati ya kuni na mkaa ambayo si mbaya kwa afya za watu bali pia ni hatari kwa uharibifu wa mazingira.

Mkurugenzi huyo mkazi wa kampuni ya Oryx Tanzania alisema wanajipongeza kwa kuwa kinara wa usambazaji wa gas ya APG kwa watanzania na kuwa wataendeea zaidi kuwekeza, kuratibu,  kueneza nishati safi kwa kutumika gas hiyo kwa manufaa ya wote.

Baadhi ya wananchi waliopata mitungi hiyo ya gas wakiwemo viongozi wa dini waliipongeza kampuni ya Oryx kwa kutoa mitungi hiyo ambayo itasaidia kutunza mazingira na kuacha kabisa matumizi ya nishati ya kuni na mkaa.

Askofu Robert Lugiko  wa Kanisa la Baptisti Tanzania Jimbo la Singida, akizungumza kwa niaba ya viongozi wa dini, alimshukuru Rais Samia na kampuni hiyo kwa kutoa mitungi hiyo ya gas na kuwa matumizi ya kuni na mkaa yamekuwa yakiwaathiri sana wanawake na kueleza kuwa kuanzia sasa anakwenda kuwa balozi wa kuhimiza matumizi ya nishati ya gas kwa ajili ya utunzaji wa mazingira.

Katika makabidhiano ya mitungi hiyo ya gas na majiko yake maafisa wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Mkoa wa Singida, Konstebo Rahma Abdarabi, Konstebo John Mduma wakiongozwa na Mkaguzi wa jeshi hilo mkoani hapa, Mwantumu Bakari walipata fursa ya kutoa elimu ya namna bora ya kukabiliana na majanga ya moto ambao unaweza kutokea wakati wa matumizi ya  majiko hayo.

 Mkurugenzi Mkazi wa Kampuni ya Oryx Tanzania, Benoit Araman (kulia) na Mkuu wa Wilaya ya Iramba, Suleiman Mwenda wakimkabidhi mtungi wa gas wenye jiko lake kwa niaba ya wenzake,Mama Lishe Sada Said anayefanya shughuli zake Misigiri wilayani humo.
 Mkurugenzi Mkazi wa Kampuni ya Oryx Tanzania, Benoit Araman (kulia) na Mkuu wa Wilaya ya Iramba, Suleiman Mwenda wakimkabidhi mtungi wa gas wenye jiko lake kwa niaba ya wenzake, Baba Lishem Ezekiel Emanuel anayefanya shughuli zake Ulemo wilayani humo.
Meneja Masoko wa Kampuni ya Oryx Tanzania, Peter Ndomba (kushoto) na Meneja Masoko wa kampuni hiyo, Angela Bitungwa  wakielekeza namna ya matumizi ya mitungi ya gas na majiko yake kwa wananchi na wajasiriamali wa Wilaya ya Iramba wakati wa hafla ya makabidhiano.
Meneja Mauzo wa kampuni hiyo, Alex Wambi akitoa elimu ya matumizi ya mitungi hiyo ya gas na majiko yake.
Mkurugenzi Mkazi wa Kampuni ya Oryx Tanzania, Benoit Araman (kulia) na Mkuu wa Wilaya ya Iramba, Suleiman Mwenda wakiteta jambo wakati wa hafla hiyo.
Muonekano wa mitungi hiyo ya gas.
Wadau mbalimbali wakisubiri kukabidhiwa mitungi hiyo kwenye hafla hiyo.
Konstebo Rahma Abdarabi wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Mkoa wa Singida akitoa elimu ya namna ya kukabiliana na moto wakati wa matumizi ya majiko ya gas.
Konstebo, John Mduma wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Mkoa wa Singida akionesha namna ya kuzima jiko la gas ambalo limelipuka kwa moto kwa kulifunika kwa kutumia karatasi maalumu au nguo nzito (blangeti) lililolowanishwa kwenye maji. Kulia ni Konstebo Rahma Abdarabi akitoa maelezo ya namna kuzima moto huo iwapo utatokea.
Mkaguzi wa jeshi hilo mkoani hapa, Mwantumu Bakari na Konstebo, John Mduma wakitoa mafunzo ya njia sahihi ya kukabiliana na majanga ya moto.
Wananchi wa Wilaya ya Iramba wakisubiri kukabidhiwa mitungi hiyo.
Viongozi wa dini wakiwa na mitungi ya gas baada ya kukabidhiwa. Kutoka kushoto ni Askofu wa Kanisa la Baptisti Tanzania Mkoa wa Singida, Robert Lugiko,  Sheikh wa Old Kiomboi, Haruna Yahaya Haji na Ustadh  Khalifa Idd Salim.
Wajasiriamali wakiondoka na mitungi yao ya gas baada ya kukabidhiwa. 

............................................................
ANGALIA VIDEO HAPA CHINI

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad