Meneja wa Tanesco Mkoa wa Singida, Mhandisi Mwamvita Ally, akizungumza na madiwani na baadhi ya wakuu wa taasisi zilizo chini ya Serikali zilizopo Manispaa ya Singida (hawapo pichani) wakati wa semina ya wadau wa nishati ya umeme iliyoandaliwa na shirika hilo Januari 8, 2024.Na Dotto Mwaibale, Singida
MADIWANI wa Halmashauri ya Manispaa ya Singida wamelipongeza Shirika la
Umeme Tanzania (TANESCO) Mkoa wa Singida kwa huduma nzuri linazozitoa na
kulitaka linapotekeleza miradi yake liwe linawashirikisha madiwani wa maeneo
husika ili kutambua vijiji na vitongoji vyenye uhitaji wa huduma ya nishati ya
umeme.
Mapendekezo hayo yametolewa na madiwani hao kwenye kikao cha wadau wa
nishati ya umeme Mkoa wa Singida kilichoandaliwa na shirika hilo na kuwashirikisha baadhi ya wakuu wa taasisi zilizo chini ya Serikali chenye lengo
la kutangaza huduma zinazotolewa pamoja na kupokea maoni na changamoto
mbalimbali.
Madiwani hao walisema Tanesco ikiweka utaratibu wa kuwashirikisha
wawakilishi hao kutaondoa malalamiko ya
wananchi ambao baadhi ya vijiji vyao bado havijafikishiwa huduma ya umeme.
Akizungumzia umuhimu wa ushirikishwaji wa madiwani kwenye miradi hiyo
Diwani wa Kata ya Kisaki, Moses Ikaku alitoa mfano wa Kitongoji cha Ilahu kuwa
na umeme lakini Tanesco wakakitaja kitongoji cha Ikenda kuwa ndicho chenye
umeme badala ya Ilahu jambo ambalo linaweza kuwaletea wananchi usumbufu.
Kwa upande wao Mstahiki Meya wa Manispaa ya Singida Yagi Kiaratu na
Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Singida, Lusia Mwiru
walimpongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa kutoa zaidi ya Sh.Bilioni 3.4 kwa
ajili ya kutekeleza miradi ya umeme katika Mkoa wa Singida ambapo pia
walilishukuru Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) Mkoa wa Singida kwa
ushirikiano mkubwa wanao utoa kwa CCM na Serikali na kuliomba kuzitendea haki fedha
hizo kwa kufanya kazi iliyokusudiwa na Serikali.
Hata hivyo viongozi hao waliziomba taasisi za umma mkoani hapa kushirikiana wakati wa utekelezaji wa miradi yao ili kuepusha migongano kama Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) kuilalamikia Tanesco kuwa wameweka nguzo zao kwenye hifadhi ya barabara au Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira singida (SUWASA) wamepitisha mabomba ya maji kwenye miundombinu ya umeme.
“Nimemsikia hapa mmoja wa kiongozi wa taasisi ya umma akilalamika dhidi ya
Tanesco. Tanroads ni taasisi, Tarura ni taasisi, Suwasa na Ruwasa zote ni
taasisi za umma naombeni mkae pamoja muweze kuunganisha mambo yenu kwani ninyi
mkianza kulalamika, diwani analalamika, mkuu wa taasisi analalamika, watu wote
tunalalamika hiyo sio sawa,” alisema Mwiru.
Mwiru alisema ni vizuri taasisi hizo zote zikakaa kwenye vikao vyao kwa
pamoja kujadili wakati wa utekelezaji wa miradi kwa kuwa kazi zao sinashabihana
kwa namna moja au nyingine hivyo aliwaomba kulifanyia kazi jambo hilo.
Naye Meya wa Manispaa ya Singida Yagi Kiaratu alizitaka taasisi zote za
Serikali mkoani Singida kuwa na mahusiano na mawasiliano na kueleza kuwa
haiwezekani kwenda holelaholela tu huku wakilalamika nguzo ya umeme sijui
imekaa wapi, bomba langu limekatwa.
Kiaratu alisema wamekuwa wakikutana na changamoto hizo wakati wa
utekelezaji wa miradi mbalimbali na kuwa Manispaa ya Singida katika mpango wao
kabambe wa kupanga mji walizishirikisha taasisi zote na kukubaliana lakini
anashangaa wakati wa utekelezaji wa miradi hiyo wanakwenda tofauti.
Alisema taasisi moja inapokuwa na mradi ni vizuri kabla ya kuuanza itoe
taarifa kwa taasisi zingine ili kuondoa kadhia hiyo ambayo mara nyingi
husababisha miundombinu iliyopo kubomolewa na kuisababishia hasara Serikali.
Meneja wa Tanesco Mkoa wa Singida, Mhandisi Mwamvita Ally alisema
wamezipokea changamoto za madiwani hao na kuwa zitafanyiwa kazi ili kuhakikisha
wananchi wanapata huduma sahihi, bora na kwa wakati.
Alisema kwa kutoa semina hiyo kwa madiwani hao anaamini kupitia wao
wananchi wote wa Manispaa ya Singida watafikiwa na elimu hiyo.
Aidha, Ally alisema ili kukabiliana na ukatikaji umeme wa mara kwa mara
shirika hilo linafanya maboresho kwa kubadilisha nguzo zilizooza na vikombe.
Mbunge wa Jimbo la Singida mjini, Musa Sima
amempongeza Meneja wa shirika hilo mkoani hapa Mhandisi Mwamvita Ally kwa kuja
na mbinu mpya ya kutoa semina kwa madiwani wa Halmashauri ya Manispaa ya
Singida na kujitambulisha baada ya kuhamia Singida akitokea Wilaya ya Kilolo
mkoani Iringa.
“Ndugu zangu madiwani wote tunakubaliana inawezekana
ni mara ya kwanza kuona taasisi bila kushinikizwa kiongozi wake anakuja na
kuona ili aweze kujitambulisha hana sababu ya kwenda kwenye baraza la madiwani
na kusema mimi ni Meneja wa Tanesco akatengeneza programu ya kujitambusha kwa
kuandaa semina. Hakika semina hii imetupa ufahamu mkubwa na kwa pamoja
tunashiriki kwenye suala ili kubwa la maendeleo kwa kweli ni jambo jema sana
naamini na taasisi zingine zitajifunza kupitia Tanesco,” alisema Sima.
Afisa Uhusiano na huduma kwa wateja wa shirika hilo, Mkoa wa Singida Rehema Mwaipopo, akielezea utekelezaji wa miradi ya Wakala wa Nishati Vijijini (REA) Mkoa wa Singida alisema shirika hilo kwa sasa inasimamia miradi miwili ya maendeleo ambao ni mradi wa Peri Urban III na mradi wa Kusambaza Umeme Maeneo Ya Madini, Viwanda Vidogovidogo na Kilimo cha Umwagiliaji unaofadhiliwa na serikali kupitia REA kwenye jimbo la Singida mjini ambayo ina thamani ya Sh. Bilioni 7.7 ambao upo kwenye hatua za utekelezaji.t
Alisema mradi huo wa kupeleka umeme katika maeneo, vitongoji na mitaa iliyopo pembezoni mwa miji (Vijiji-Miji) yaani peri urban ambayo yanauhitaji mkubwa wa umeme lakini pia hali ya maeneo hayo inashabihiana na maeneo ya vijijini.
Alisema mradi huo unatekelezwa na mkandarasi M/S
Central Electricals International Ltd katika Lot 6 vijiji 13 vyenye jumla ya vitongoji 34 ndani
ya jimbo la Singida mjini na kuwa mkataba unategemewa kukamilika Julai 19, 2024 na unathamani ya zaidi ya Sh.
Bilioni 7.1 na kuwa mpaka kufikia Januari 7, 2024 wamefanikiwa kuwasha
vitongoji 10 kati ya 34 ambapo ni sawa na asilimia 29.4

















No comments:
Post a Comment