CHUO CHA UHASIBU ARUSHA CHAANZISHA KITUO CHA KULEA MAWAZO YA UBUNIFU - SINGIDANIBLOG

Habari za Hivi Punde

Post Top Ad

Thursday, 30 May 2024

CHUO CHA UHASIBU ARUSHA CHAANZISHA KITUO CHA KULEA MAWAZO YA UBUNIFU

Afisa Uhusiano wa Chuo cha  Uhasibu Arusha (IAA), Stela Kalinga, akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) kwenye maadhimisho ya kimataifa ya elimu, ujuzi na ubunifu mwaka 2024 yanayofanyika jijini Tanga. Mei 29, 2024.

.......................

Mashaka Kibaya, Tanga 

CHUO cha Uhasibu Arusha (IAA) kimeanzisha kituo maalum cha kulea mawazo ya ubunifu kwa Wanafunzi lengo likiwa kuwaondosha kwenye dhana ya kuajiriwa huku wakifikiria kujiajiri sanjari na kuweza kusaidia sehemu nyingine ya jamii.

Taarifa hiyo imetolewa Jana na Afisa uhusiano wa Chuo hicho cha uhasibu Arusha, Stela Kalinga wakati ambapo IAA wakiwa miongoni mwa washiriki kwenye maadhimisho ya Kimataifa ya elimu, ujuzi na ubunifu mwaka 2024 yanayofanyika Jijini Tanga.

Katika taarifa yake kwa Wanahabari Kalinga alisema, IAA ni mali ya Serikali chini ya Wizara ya fedha huku kikitoa mafunzo kuanzi ngazi ya cheti, astashahada, shahada na shahada ya uzamili.

Pamoja na hayo chuo hicho kimekuja program ya kiotamizi (incubator) kozi ya kipekee ya elimu ujuzi inayompa mwanafunzi maarifa, ujuzi hadi kufikia nafasi ya kujiajiri na vilevile kutengeneza mazingira ya kusaidia wengine.

Utaratibu huo umeonekana kuwa wenye  mafanikio makubwa kwa vile umeanza kutoa matokeo chanya katika kukidhi changamoto ya ajira kwa wanafunzi kwa vile tayari wapo waliojiajiri na pia kuweza kuajiri wenzao.

Akizungumzia zaidi program hiyo ya kipekee, Kalinga alisema,ni mtaala wa kielimu ambapo mwanafunzi anapofika chuoni anatakiwa kuja na mawazo yake ya ubunifu ambapo chuo kinachukua jukumu la kumuendeleza pamoja na kumuunganisha na wadau wengine ili kumuongezea uwezo katika yale aliyoyaona kuwa ni fursa kwa upande wake.

"Tumeanzisha program atamizi (incubator) inayolea mawazo ya kibunifu kwa vijana na kusaidiwa kuwa vitu halisi kama biashara,sanaa, na vinginevingi, mpaka sasa wapo waliofanikiwa kuanzisha kampuni zao" alisema Kalinga.

Kalinga aliendelea kusema kuwa chuo hicho kinatoa mafunzo kuanzia ngazi ya cheti, astashahada, shahada na shahada ya uzamili mafunzo ambayo yanatolewa kwa fani mbalimbali.

Kuhusu shahada ya uzamili,Kalinga alisema,IAA ni tofauti na vyuo vingine kwani masomo hayo hutolewa kwa kipindi cha mwaka mmoja mwanafunzi anaweza kusoma akiwa chuoni au kwa njia ya mtandao 'online'.

Kwa mujibu wa Kalinga fani zilizopo chuoni ni pamoja na uhasibu,fedha, tehama,uchumi,kodi,utalii,masoko,bima na mengineyo na pia mafunzo ya muda mfupi yakitolewa kwa fani mbalimbali.

Afisa uhusiano huyo ametanabaisha kuwa tayari dirisha la udahili limefunguliwa  akiwataka wakazi wa mkoanwa Tanga na watanzania kwa ujumla kufanya maombi kupitia tovuti ya www.iaa.ac.tz kwa kuwasiliana na uongozi wa chuo kwa simu ili kupatiwa usaidizi kufanya maombi.

Mohamedi Ramadhani Kosta ni mwanafunzi wa IAA, anasema kwamba,kupitia utaratibu huo wa kiotamizi amefanikiwa kuanzisha kampuni yake ya kuchakata mazao ya chakula ambapo alianza kwa kutengeneza unga wa lishe lakini kwa sasa anauza uji wa take away huku akijivunia kuajiri vijana wenzake.

Maadhimisho ya Kitaifa ya elimu, ujuzi na ubunifu 2024 yanafanyika katika viwanja vya Popatlal Jijini Tanga na kauli mbiu yake ni "elimu, ujuzi na ubunifu kwa uchumi shindani".


No comments:

Post a Comment

Post Top Ad