Huduma ya kuwaombea wagonjwa na watu wenye changamoto mbalimbali ikifanyika kwenye mkutano wa injili ulioendeshwa na Wachungaji Wanafunzi kutoka Chuo Kikuu cha Teofilo Kisanji (TEKU) cha Kanisa la Moravian Tanzania kilichopo Mkoa wa Mbeya waliopo Mjini Singida kwa ajili ya ziara maalumu ya kufanya uinjilisti mkutano uliofanyika Mei 16, 2024 katika viwanja vya kanisa hilo Parishi ya Sabasaba Mandewa mjini Singida.
.............................
Na Dotto Mwaibale, Singidani Blog.
WACHUNGAJI
Wanafunzi kutoka Chuo Kikuu cha Teofilo Kisanji (TEKU) cha Kanisa la
Moravian Tanzania kilichopo Mkoa wa Mbeya waliopo Mjini Singida kwa ajili ya
ziara maalumu ya kufanya uinjilisti na shughuli nyingine mbalimbali wameonesha matendo ya huruma na kuwaombea
wagonjwa.
Mchungaji Daniel Siyame ambaye ni Makamu
Mwenyekiti wa Umoja wa Wanafunzi wa
Theolojia TEKU (UWATHETE) amesema ziara hiyo imekuwa ya neema kubwa kwao na
wamejifunza mengi kutoka kwa wana Singida.
"Ziara hii tulioianza Mei 13, 2024 imekuwa
na mafanikio makubwa kwetu licha ya kuwepo na changamoto ndogondogo za kawaida
kwani tumepokelewa vizuri na kupatiwa ushirikiano mkubwa na wenyeji wetu,"
alisema Mchungaji Siyame.
Alisema ziara hiyo imekuwa ya baraka nyingi
kutoka kwa Kanisa la Moravian Mkoa wa Singida kupitia Usharika wa Singida Mjini
na Parishi ya Sabasaba.
Siyame alisema msukumo mkubwa wa ziara hiyo
ulitokana na wachungaji hao wanafunzi wa TEKU kupitia umoja wao huo pamoja na
Kanisa la Moravian Usharika wa Singida mjini na parishi zake.
Mchungaji Siyame alisema umoja wao huo umekuwa na
utaratibu wa kufanya ziara ya namna hiyo ya kufanya uinjilisti kila mwaka na
kueleza kuwa mwaka juzi walifanya Mkoa wa Mtwara, mwaka jana Mkoa wa Songwe na
mwaka huu Mkoa wa Singida.
Alisema katika ziara hizo wamekuwa wakifanya
uinjilisiti wa nyumba kwa nyumba kutoa mafunzo ya ujasiriamali, uchumi, makuzi
ya watoto, semina zenye maudhui mbalimbali na kufanya matendo ya huruma ya
kuwatembelea wagonjwa mahospitalini , yatima, wajane, wagane na kuwaombea ikiwa
ni pamoja na kuwapa chochote kama
sabuni, maji na vitu vingine vinavyofanana na hivyo.
Alisema mbali ya kufanya matendo hayo ya huruma
pia huwa wanafanya mkutano wa injili kwa ajili ya washiriki kupata neno la
Mungu ambapo pia watu wenye changamoto mbalimbali uombewa na katika ziara hiyo
mkoani hapa mkutano huo wa injili umekuwa ukifanyika Kanisa la Moravian Parishi
ya Sabasaba iliyopo nyuma ya Hospitali ya Rufaa ya Mandewa.
Akihubiri katika mkutano wa injili uliofanyika
viwanja vya Kanisa la Moravian Parishi ya Sabasaba, Mchungaji Paul Thomas
kutoka Chuo cha TEKU ambaye pia ni Mkuu wa Jimbo la Morogoro la Kanisa la Kiinjili la Kilutheri
Tanzania (KKKT) akizungumzia mitazamo ya watu alisema mtazamo
wa mtu yeyote unaweza kuwa na athari katika maisha yake au kuyainua maisha yake
akifafanua maneno hayo kutoka katika Biblia kitabu Methari 23: 7A.
Alisema mtu ajionavyo nafsini mwake ndivyo alivyo
na akijidharau ndivyo atakavyodharaurika
katika jamii na kueleza kuwa kitu chochote utakachokiruhusu katika nafsi
yako ndio mwenendo wa maisha yako na mtazamo wako.
"Mimi siwezi kufanya biashara na wale wasomi
zaidi yangu, mimi siwezi kujenga nyumba kubwa kibanda chetu hiki hiki na watoto
wetu kinatutosha , mimi nimechoka na haya maisha ya tabu bora ya kufa tu,
wanaokula nyama ni watu wenye uwezo sisi ni dagaa na sukuma wiki tu
(kabeji) mimi sitaweza kufaulu mtihani
wangu nawaachia wenye akili," alisema Mchungaji Thomas akitaja baadhi ya
maneneo hayo ambayo ni mitazamo ya watu wengi yenye kuwakatisha tamaa na
kuwataka kubadilika na kuwa na mitazamo
ya ushindi wakati wote kwani kwa Mungu kila jambo linawezekana.
Mchungaji Thomas alisema inawezekana kuwa
changamoto zote tulizonazo leo hii zimetokana na mitazamo yetu ambayo
tulimkosea Mungu katika maeneo fulani akimtolea mfano mtoto aliyemfuata baba
yake na kumuambia ampe sehemu ya mali yake na baada ya kupewa alikwenda nchi ya
mbali na kutumia mali hiyo kwa anasa.
Alisema baada ya mtoto kuishiwa na kuishi maisha
ya tabu akila chakula cha nguruwe ndipo alipokumbuka kuwa nyumbani kwa baba
yake kuna kila kitu na anawatumishi wengi wanaokula na kusaza hivyo ni heri
arudi kwa baba yake kuomba msamaha na akawe mtumishi kuliko maisha ya tabu
aliyokuwa akiishi ugenini kwa kukosa fedha.
Thomas akinukuu mistari kadhaa kutoka katika
biblia alisema mtoto huyo aliporudi baba yake alimuonea huruma na kumpokea
vizuri na kufanyiwa sherehe kubwa jambo lililomuudhi kaka yake na kusema
alichokifanya dhidi yake hakumtendea
haki kwani amekuwa naye siku zote lakini hakuwahi kumfanyie sherehe kama hiyo
aliyomfanyia mdogo wake ambaye alikwisha mpatia sehemu ya mali yake na akaenda
kuitapanya kwa kuponda raha.
Mchungaji Thomas alisema inawezekana mitazamo yetu leo hii imetufanya
tutangetange huku na kule na kuwa inatupasa tujue kuwa baba yetu mwenye huruma
ni mmoja tu naye si mwingine ni Yesu Kristo na Mungu wetu anayeyajua mahitaji
yetu yote hivyo ni vizuri tukamrudia kama alivyofanya mwanampotevu ambaye
alilia kwa uchungu na kusema ni heri ni rudi kwa baba yangu ambako kuna
watumishi wengi wanakula chakula kingi na kusaza.
Kwa upande wake Mchungaji Oscar Fallanga ambaye
ni kiongozi wa kanisa hilo Mkoa wa Singida akizungumzia kuhusu ziara ya
wachungaji hao alisema kesho kutwa
Jumapili ya Mei 19 , 2024 watashiriki ibada kubwa itakayoongozwa na Askofu wa kanisa
hilo Jimbo la Magharibi Tanzania, MchungajiEzekiel Yona ibada ambayo itakuwa na
changizo la kupata fedha kwa ajili ya ujenzi wa ofisi ya Mission ya Jimbo la
Singida ambalo linatarajiwa kuanzishwa hivi karibuni.
Mchungaji Falanga alitumia nafasi hiyo kuwaalika
wana Singida na wadau mbalimbali kwenda kushiriki ibada hiyo ambayo ni kubwa na
muhimu kwa kanisa hilo.





























No comments:
Post a Comment