WACHUNGAJI KUTOKA CHUO KIKUU CHA TEKU JIJINI MBEYA WAFANYA MATENDO YA HURUMA SINGIDA - SINGIDANIBLOG

Habari za Hivi Punde

Post Top Ad

Friday, May 17, 2024

WACHUNGAJI KUTOKA CHUO KIKUU CHA TEKU JIJINI MBEYA WAFANYA MATENDO YA HURUMA SINGIDA

Huduma ya kuwaombea wagonjwa na watu wenye changamoto mbalimbali ikifanyika kwenye mkutano wa injili ulioendeshwa na Wachungaji Wanafunzi kutoka Chuo Kikuu cha Teofilo Kisanji (TEKU) cha Kanisa la Moravian Tanzania kilichopo Mkoa wa Mbeya waliopo Mjini Singida kwa ajili ya ziara maalumu ya kufanya uinjilisti mkutano uliofanyika Mei 16, 2024 katika viwanja vya kanisa hilo Parishi ya Sabasaba Mandewa mjini Singida.  

.............................

Na Dotto Mwaibale, Singidani Blog.

WACHUNGAJI  Wanafunzi kutoka Chuo Kikuu cha Teofilo Kisanji (TEKU) cha Kanisa la Moravian Tanzania kilichopo Mkoa wa Mbeya waliopo Mjini Singida kwa ajili ya ziara maalumu ya kufanya uinjilisti na shughuli nyingine mbalimbali  wameonesha matendo ya huruma na kuwaombea wagonjwa.

Mchungaji Daniel Siyame ambaye ni Makamu Mwenyekiti  wa Umoja wa Wanafunzi wa Theolojia TEKU (UWATHETE) amesema ziara hiyo imekuwa ya neema kubwa kwao na wamejifunza mengi kutoka kwa wana Singida.

"Ziara hii tulioianza Mei 13, 2024 imekuwa na mafanikio makubwa kwetu licha ya kuwepo na changamoto ndogondogo za kawaida kwani tumepokelewa vizuri na kupatiwa ushirikiano mkubwa na wenyeji wetu," alisema Mchungaji Siyame.

Alisema ziara hiyo imekuwa ya baraka nyingi kutoka kwa Kanisa la Moravian Mkoa wa Singida kupitia Usharika wa Singida Mjini na Parishi ya Sabasaba.

Siyame alisema msukumo mkubwa wa ziara hiyo ulitokana na wachungaji hao wanafunzi wa TEKU kupitia umoja wao huo pamoja na Kanisa la Moravian Usharika wa Singida mjini na parishi zake.

Mchungaji Siyame alisema umoja wao huo umekuwa na utaratibu wa kufanya ziara ya namna hiyo ya kufanya uinjilisti kila mwaka na kueleza kuwa mwaka juzi walifanya Mkoa wa Mtwara, mwaka jana Mkoa wa Songwe na mwaka huu Mkoa wa Singida.

Alisema katika ziara hizo wamekuwa wakifanya uinjilisiti wa nyumba kwa nyumba kutoa mafunzo ya ujasiriamali, uchumi, makuzi ya watoto, semina zenye maudhui mbalimbali na kufanya matendo ya huruma ya kuwatembelea wagonjwa mahospitalini , yatima, wajane, wagane na kuwaombea ikiwa ni pamoja  na kuwapa chochote kama sabuni, maji na vitu vingine vinavyofanana na hivyo.

Alisema mbali ya kufanya matendo hayo ya huruma pia huwa wanafanya mkutano wa injili kwa ajili ya washiriki kupata neno la Mungu ambapo pia watu wenye changamoto mbalimbali uombewa na katika ziara hiyo mkoani hapa mkutano huo wa injili umekuwa ukifanyika Kanisa la Moravian Parishi ya Sabasaba iliyopo nyuma ya Hospitali ya Rufaa ya Mandewa.

Akihubiri katika mkutano wa injili uliofanyika viwanja vya Kanisa la Moravian Parishi ya Sabasaba, Mchungaji Paul Thomas kutoka Chuo cha TEKU ambaye pia ni Mkuu wa Jimbo la Morogoro la Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) akizungumzia mitazamo ya watu alisema mtazamo wa mtu yeyote unaweza kuwa na athari katika maisha yake au kuyainua maisha yake akifafanua maneno hayo kutoka katika Biblia kitabu Methari 23: 7A.

Alisema mtu ajionavyo nafsini mwake ndivyo alivyo na akijidharau ndivyo atakavyodharaurika  katika jamii na kueleza kuwa kitu chochote utakachokiruhusu katika nafsi yako ndio mwenendo wa maisha yako na mtazamo wako.

"Mimi siwezi kufanya biashara na wale wasomi zaidi yangu, mimi siwezi kujenga nyumba kubwa kibanda chetu hiki hiki na watoto wetu kinatutosha , mimi nimechoka na haya maisha ya tabu bora ya kufa tu, wanaokula nyama ni watu wenye uwezo sisi ni dagaa na sukuma wiki tu (kabeji)  mimi sitaweza kufaulu mtihani wangu nawaachia wenye akili," alisema Mchungaji Thomas akitaja baadhi ya maneneo hayo ambayo ni mitazamo ya watu wengi yenye kuwakatisha tamaa na kuwataka kubadilika na kuwa na  mitazamo ya ushindi wakati wote kwani kwa Mungu kila jambo linawezekana.

Mchungaji Thomas alisema inawezekana kuwa changamoto zote tulizonazo leo hii zimetokana na mitazamo yetu ambayo tulimkosea Mungu katika maeneo fulani akimtolea mfano mtoto aliyemfuata baba yake na kumuambia ampe sehemu ya mali yake na baada ya kupewa alikwenda nchi ya mbali na kutumia mali hiyo kwa anasa.

Alisema baada ya mtoto kuishiwa na kuishi maisha ya tabu akila chakula cha nguruwe ndipo alipokumbuka kuwa nyumbani kwa baba yake kuna kila kitu na anawatumishi wengi wanaokula na kusaza hivyo ni heri arudi kwa baba yake kuomba msamaha na akawe mtumishi kuliko maisha ya tabu aliyokuwa akiishi ugenini kwa kukosa fedha.

Thomas akinukuu mistari kadhaa kutoka katika biblia alisema mtoto huyo aliporudi baba yake alimuonea huruma na kumpokea vizuri na kufanyiwa sherehe kubwa jambo lililomuudhi kaka yake na kusema alichokifanya  dhidi yake hakumtendea haki kwani amekuwa naye siku zote lakini hakuwahi kumfanyie sherehe kama hiyo aliyomfanyia mdogo wake ambaye alikwisha mpatia sehemu ya mali yake na akaenda kuitapanya kwa kuponda raha.

Mchungaji Thomas alisema  inawezekana mitazamo yetu leo hii imetufanya tutangetange huku na kule na kuwa inatupasa tujue kuwa baba yetu mwenye huruma ni mmoja tu naye si mwingine ni Yesu Kristo na Mungu wetu anayeyajua mahitaji yetu yote hivyo ni vizuri tukamrudia kama alivyofanya mwanampotevu ambaye alilia kwa uchungu na kusema ni heri ni rudi kwa baba yangu ambako kuna watumishi wengi wanakula chakula kingi na kusaza.

Kwa upande wake Mchungaji Oscar Fallanga ambaye ni kiongozi wa kanisa hilo Mkoa wa Singida akizungumzia kuhusu ziara ya wachungaji hao  alisema kesho kutwa Jumapili ya Mei 19 , 2024 watashiriki ibada kubwa itakayoongozwa na Askofu wa kanisa hilo Jimbo la Magharibi Tanzania, MchungajiEzekiel Yona ibada ambayo itakuwa na changizo la kupata fedha kwa ajili ya ujenzi wa ofisi ya Mission ya Jimbo la Singida ambalo linatarajiwa kuanzishwa hivi karibuni.

Mchungaji Falanga alitumia nafasi hiyo kuwaalika wana Singida na wadau mbalimbali kwenda kushiriki ibada hiyo ambayo ni kubwa na muhimu kwa kanisa hilo.

 Mchungaji Paul Thomas kutoka Chuo cha TEKU ambaye pia ni Mkuu wa Jimbo la Morogoro wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) akihubiri kwenye mkutano huo.
Mthiologia Baraka Kyambala akiongoza maombi kwenye mkutano huo.
Mchungaji Daniel Siyame ambaye ni Makamu Mwenyekiti  wa Umoja wa Wanafunzi wa Theolojia TEKU (UWATHETE) akizungumzia ziara hiyo kwa ujumla.
Wachungaji kutoka TEKU wakiwa meza kuu wakati wa mkutano huo Kutoka kulia ni Mchungaji Fenard Mtepa wa Ushirika wa TEKU, Mchungaji Paulo Thomas, Mthiologia Baraka Kyambala na Mtheologia Israel Kabigili aliyekuwa Mshereheshaji (MC) katika mkutano wa injili.
Mchungaji John Ndomba (wa kwanza kushoto) Mchungaji Mariam Ikenda (wa pili kutoka kushoto) na Mchungaji Pascal George (wa tatu kutoka kushoto) wakiwa katika picha ya pamoja na wakazi wa Singida ambao waliwapa huduma ya kuwafanyia maombi.
Mchungaji Pascal George (wa kwanza kushoto) Mchungaji John Ndomba (wa pili kutoka kushoto na Mchungaji Mariam Ikenda ( katikati) wakifanya maombi wakati wa ziara ya uinjilisti ya  nyumba kwa nyumba walioifanya Mei 16, 2024 mjini Singida..
Wachungaji John Ndomba, Mariam Ikenda na Pascal Georg wakimuombea mama mkazi wa Singida ambaye anachangamoto ya ulemavu wa mguu..
Mchungaji Imani Ndabila akimhubiria neno la Mungu Mkazi wa Singida eneo la Mwenye Theresia Martin wakati akifanya uinjilisti wa nyumba kwa nyumba.
Mkazi wa Singida Theresia Martin akifurahia huduma ya nyumba kwa nyumba baada ya kutembelewa na wachungaji hao kutoka Chuo cha TEKU.
Mchungaji Elizabeth Mbao akifanya huduma ya uinjilisi ya nyumba kwa nyumba.
Mchungaji Mbao (kushoto( na Mchungaji Imani Ndabila wakimuombea mtoto Jaden Isack na wazazi wake wakati wa huduma hiyo ya uinjilisti wa nyumba kwa nyumba.
Muonekano wa Kanisa la Moravian Parishi ya Sabasaba Mandewa unapofanyika mkutano wa injili  na wafunzi hao kutoka Chuo Kikuu cha TEKU.
Furaha ikitamalaki katika mkutano wa injili.
Nifuraha tupu katika mkutano huo.
Mchungaji Yona Mbogo (mwenye shati jeupe mbele aliyeshika maiki) akiongoza hamasa kwenye mkutano huo.
Malaika hawa watoto wa Mungu nao hawakuwa nyuma baada ya kufika na mama yao kwenye mkutano huo ambapo nao walijichotea baraka tele.
Kwaya ya Uinjilisti ya Wanafunzi wa Chuo cha TEKU ikitoa burudani wakati wa mkutano wa injili.
Maombi yakifanyika kwenye mkutano huo.
Mchungaji Mwaipopo kutoka Jimbo la Mbeya akionesha  ishara ya ushindi kwenye mkutano huo.
Maombi yakiendelea.


Taswira ya mkutano huo.
 

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad