SHEIKH MKOA WA SINGIDA AWATAKA WAISLAMU KUTOTUMIKA NA WANASIASA WANAO TAKA UONGOZI - SINGIDANIBLOG

Habari za Hivi Punde

Post Top Ad

Saturday, 8 June 2024

SHEIKH MKOA WA SINGIDA AWATAKA WAISLAMU KUTOTUMIKA NA WANASIASA WANAO TAKA UONGOZI

--VIDEO--

Sheikh Mkoa wa Singida, Issa Nasoro akikagua mradi wa mashine ya kusaga na kukoboa unaoendeshwa na Waislamu wa Kata ya Makuro iliyopo Wilaya ya Singida wakati wa ziara yake ya kikazi aliyoifanya jana.

.............................

Na Dotto Mwaibale, Singidani Blog

SHEIKH wa Mkoa wa Singida, Issa Nasoro amewataka Waislamu mkoani humo kutotumika na baadhi ya watu wanaotaka kugombea nafasi mbalimbali za uongozi na kuwa hiyo sio kazi yao.

Kiongozi huyo wa dini mkoani hapa Sheikh Nasoro ambaye alikuwa mgeni rasmi aliyasema hayo jana wakati akizungumza na Waislamu wa Kata ya Makuro baada ya kutembelea na kukagua miradi iliyotekelezwa na waislamu wa kata hiyo.

Baadhi ya miradi aliyoitembelea ni mradi wa mashine za kusaga na kukoboa mahindi ambazo zipo katika vitongoji vya Mkenge, Matumbo, Magugu na maeneo mengine huku idadi yake zikiwa sita ambapo kila mashine imegharimu zaidi ya Sh.Milioni 6.

Miradi mingine iliyotembelewa na Sheikh Nasoro wakati wa ziara hiyo ni madarasa yaliyojengwa kwa ajili ya kufundishia watoto elimu ya dini ambayo yapo katika kila kitongoji na shamba la mahindi la ekari 50 pamoja na gari aina ya Noah.

"Sasa msitumike kwa ajili ya manufaa ya watu wanaogombea hatukatai kila mwananchi anayo haki ya kugombea nafasi yoyote anayoitaka tunachoomba ni Mwenyezi Mungu atuletee viongozi waadilifu na hiyo ndiyo kazi yetu lakini sio ya kutengeneza mazingira ya kupiga debe kwa wagombea wa ubunge na udiwani," alisema Sheikh Nasoro.

Alisema wajibu wao ni kumsemea Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa mambo mengi ya maendeleo aliyoyafanya kwenye sekta za afya, barabara, elimu, maji na nyingine zote na kwa upande wake hakuna mtu atakayemshika mdomo asiweze kusema na kueleza kuwa malipo ya mtenda wema ni kumlipa wema.

Alisema miradi yote hiyo Rais Samia ameisimamia na kuikamilisha  katika kipindi kigumu kwani hakuandaliwa baada ya Rais wa Awamu ya Tano Hayati John Pombe Magufuli kufariki akiwa madarakani na kufanikiwa kuvivaa viatu vyake kwa kutekeleza miradi hiyo kwa zaidi ya asilimia 80.

Sheikh Nasoro alitumia nafasi hiyo kuwapongeza Waislamu wa kata hiyo kwa kuwa vinara wa kutekeleza maagizo ya ofisi yake ya kila waislamu kwenye kata zao kuanzisha miradi ya maendeleo ambapo aliwatia moyo kuwa hata maono yao ya kupata trekta kwa ajili ya kilimo yatafanikiwa kwa kuwa tayari wameonesha njia ya mafanikio.

"Mama Samia anatoa fedha za mikopo na ninyi kupitia umoja wenu huo hamjazuiliwa tuwasiliane tuone namna mtakavyo zipate fedha hizo ili mkopeshwe," alisema Sheikh Nasoro.

Aidha, Sheikh Nasoro aliwataka waislamu wa kata hiyo baada ya kupata mafanikio hayo sasa waanzishe kilimo cha zao la biashara la alizeti na wafungue kiwanda cha uchakataji na kuongeza thamani ya zao hilo kwa kuuza mafuta  yatakayo andikwa Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA) Kiwanda cha Mafuta Makuro.

Kwa upande wake Diwani wa Vitu Maalumu wa kata hiyo Hadija Msuri alisema kazi kubwa wanayoifanya ni kupokea maelekezo kutoka kwa Rais Samia na Mufti wa Tanzania kupitia viongozi wao na kuyapeleka kwa wananchi na kushirikiana nao na ndio chanzo cha mafanikio yao mbalimbali kwenye kata hiyo.

Mlezi wa Waislamu wa kata hiyo,  Iddi Isango alimuomba Sheikh Nasoro kuwasaidia kupata umeme kwa ajili ya kuendesha mashine hizo ambazo zipo katika vitongoji mbalimbali  huku zikiwa  na miundombinu yote lakini hazifanyi kazi kutokana na TANESCO Mkoa wa  Singida  kushindwa kuwaunganishia umeme.

Mtaalamu na Mwanasheria wa Ofisi ya Sheikh Nasoro Abdul Ramadhani alisema Waislamu wa kata hiyo wanajitambua na wanafanya kazi zao kwa kufuata sheria na taratibu za nchi ndio maana wanapata mafanikio makubwa.

Sheikh wa Mkoa wa Singida, Issa Nasoro akipokelewa alipokuwa akianza ziara yake ya kikazi katika Kata ya Makuro.


Sheikh wa Mkoa wa Singida, Issa Nasoro na viongozi mbalimbali wa kiislamu wakitoka kukagua moja ya madarasa yaliyojengwa katika kata hiyo Kitongoji cha Mkenge.

Sheikh wa Mkoa wa Singida, Issa Nasoro na ujumbe wake akikagua mradi wa mashine ya kusaga uliopo Kitongoji cha Mkenge.
Muonekano wa moja ya darasa lililojengwa kitongoji na Matumbo.
Ukaguzi wa ujenzi wa darasa kitongoji cha Matumbo ukifanyika.
Sheikh wa Mkoa wa Singida, Issa Nasoro akipata maelezo ya mradi wa shamba la mahindi uliopo Kata ya Makuro.

Waislamu wa Kata ya Makuro wakitembelea shamba hilo wakati wa ziara hiyo.
Picha ya pamoja ikipigwa wakati Sheikh Nasoro alipotembelea mradi wa mashine ya kusaga na kukoboa nafaka Kata ya Makuro.

Wanawake wa Kiislamu wakiwa katika ziara hiyo ya Sheikh wao Issa Nasoro.

 Wanawake wa Kiislamu wakimsiliza Sheikh Nasoro (Hayupo pichani) alipokuwa akizungumza nao alipokuwa akitoa majumuisho ya ziara yake.

Sheikh Issa Nasoro akisisitiza jambo wakati akizungumza na Waislamu wa Kata ya Makuro wakati akihitimisha ziara yake.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad