SUWASA SINGIDA YAWATUNUKU VYETI WALIOTOA ARDHI YAO KUPISHA UJENZI WA MABWAWA YA KUTIBU MAJI TAKA MANGA - SINGIDANIBLOG

Habari za Hivi Punde

Post Top Ad

Thursday, 6 June 2024

SUWASA SINGIDA YAWATUNUKU VYETI WALIOTOA ARDHI YAO KUPISHA UJENZI WA MABWAWA YA KUTIBU MAJI TAKA MANGA

Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Singida (SUWASA) Hosea Magimbi akizungumzia Mradi wa Ujenzi wa Mabwawa ya kutibu Maji Taka Manga unaotekelezwa Kata ya Manga katika Manispaa ya Singida.

......................... 

Na Dotto Mwaibale, Singidani Blog

MAMLAKA ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Singida (SUWASA) imetoa vyeti vya kuwatambua wananchi wa Kata ya Manga iliyopo Manispaa ya Singida ambao walitoa maeneo yao ya ardhi kwa ajili ya kupisha utekelezaji wa Mradi wa Ujenzi wa Mabwawa  ya kutibu majitaka Manga unaotekelezwa katika Manispaa hiyo.

Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi wa SUWASA katika hafla ya kukabidhi vyeti hivyo kwa wananchi hao pamoja na kuelezea maendeleo ya mradi huo unaotekelezwa kwenye eneo hilo Mkoa wa Singida, Hosea Magimbi alisema mradi huo ni wa muhimu sana.

Alisema mradi huo umegharimu zaidi ya Sh. Bilioni 1.7 fedha ambazo zimetolewa na Serikali chini ya Rais Samia Suluhu Hassan ikiwa ni utekelezaji wa ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) eneo la Kata ya Manga kupitia mkandarasi ambaye atakuwa chini ya usimamizi wa SUWASA.

Magimbi alisema mradi huo ni wa karne kwa maana kwamba mji wa Singida haujawahi kupata mradi wa aina hiyo hivyo mradi huo ni wa kwanza na wananchi waliowengi wanahitaji kunufaika nao.

“Mradi huu utawanufaisha wananchi wengi kwa kuwaondolea adha ya maji taka kutoka kwenye majumba yao na kuyapeleka katika mabwawa hao yatakayojengwa eneo hilo na kutibu maji taka,” alisema Magimbi.

Magimbi alitumia nafasi hiyo kuwashukuru wananchi wa eneo hilo kwa kuwapa ardhi kupisha mradi huo na katika kuthamini mchango wao huo wamewatunuku vyeti maalumu ili iwe kumbukumbu kwao na SUWASA.

Aidha, Magimbi aliwaomba wananchi wa eneo hilo waendelee kutoa ushirikiano wakati wote wa utekelezaji wa mradi huo hadi hapo utakapo kamilika.

Diwani wa Kata ya Manga, Ramadhan Yusuph alisema mradi huo ni wa muhimu kwa wananchi wa eneo hilo kwani watayatumia maji hayo ambayo yatasafishwa kitaalamu kwa ajili ya kuanzisha kilimo cha mboga mboga hivyo uchumi wa wana Manga utakuwa kupitia uuzaji wa bidhaa zitakazotokana na kilimo hicho.

Mkazi wa Kata hiyo Juma Chima alisema walikuwa na changamoto kubwa ya maji hasa wakati wa kiangazi hivyo anawashuru SUWASA kwa kuwapekea mradi huo ambao una kwenda kuwa mkombozi kwao

Abubakari Misughaa mazi wa kijiji hicho alianza kuishukuru Serikali kupitia SUWASA kwa kuwapelekea mradi huo na kueleza kuwa SUWASA wamefika wakati muafaka ndani ya kijiji hicho kuwapelekea mradi huo ambao utakuwa na manufaa makubwa kwa wananachi ambao watakuwa wakiishi kandokando ya mabwawa hayo.

Alisema baadhi ya faida watakayoipata wananchi hao ni kuanzisha kilimo cha umwagiliaji na mbogamboga kilimo ambacho kitabadilisha maisha yao kwa kuinuka kiuchumi na kueleza kuwa SUWASA kwao imekuwa na faida kubwa kwani wamewapelekea maji ya kutumia wananchi na kusambazwa katika taasisi zote za Serikali.

Diwani wa Kata ya Manga, Ramadhan Yusuph , akizungumzia faida ya mradi huo.
Mkazi wa Kata hiyo Juma Chima
Mkazi wa Kata hiyo Juma Chima akizungumzia mradi huo.
Mzee Abubakari Misughaa akichangia jambo kwenye hafla hiyo.
Diwani wa Kata ya Manga, Ramadhani Yusuph akiwakabidhi vyeti wananchi waliotoa ardhi yao kupisha mradi huo.
Vyeti vikikabidhiwa.
Mmoja wa wananchi waliotoa ardhi kupisha mradi huo akipokea cheti chake cha utambuzi.
Wananchi wa Kata ya Manga wakiwa kwenye hafla hiyo.
Hafla hiyo ikiendelea.



 Hafla hiyo ikiendelea.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad