Naibu Waziri wa Nishati, Judith Kapinga (kushoto), ambaye alikuwa mgeni rasmi akikata utepe kuashiria uwashaji wa umeme katika vijiji viwili vya Mwasauya na Mdilu vilivyopo Wilaya ya Singida katika hafla iliyofanyika June 5, 2024. Kutoka kulia aliyeshika Maiki .ni Afisa Uhusiano na Huduma kwa Wateja TANESCO Mkoa wa Singida, Rehema Mwaipopo, Diwani wa Kata ya Mwasauya, Salum Juma na Mbunge wa Jimbo la Singida Kaskazini Ramadhan Ighondo.
...........................
Na Dotto Mwaibale, Singidani Blog.
NAIBU Waziri wa Nishati, Judith Kapinga amesema
kutokana na uchapakazi mzuri wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan vijiji vyote vya Mkoa
wa Singida tayari vimefikishiwa umeme huku vijiji 84 vya Singida Kaskazini vikinufaika
kasoro vinne ambayo navyo vitapata kabla ya June 15, 2024 kwani wakandarasi
wapo kazini.
Kapinga ambaye alikuwa mgeni rasmi alitoa kauli
hiyo June 5, 2024 wakati wa hafla ya uwashaji wa umeme katika vijiji viwili vya
Mwasauya na Mdilu vilivyopo Wilaya ya Singida kupitia Mradi wa Wakala wa
Nishati Vijiji (REA) Awamu ya Tatu, mzunguko wa pili kwa kushirikiana na
Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO)
“Kazi hii kubwa aliyoifanya Rais wetu Dkt. Samia
Suluhu Hassan napenda kusema mnyonge mnyongeni lakini haki yake wacha apewe,”
alisema Kapinga huku akishangiliwa.
Kapinga alisema maendeleo ni hatua na kuwa
ilikuwa ni lazima umeme uvikishwe kwanza kwenye vijiji ndipo upelekwe
katika vitongoji vyote na hiyo ndiyo
dhamira ya Serikali.
Alisema katika mwaka huu wa fedha wa 2024/ 2025
Serikali imetenga fedha kwa ajili ya kufikisha umeme katika vijiji 4000 kazi ambayo
itafanywa kwa awamu.
Aidha, Kapinga alisema miradi ya umeme ya namna
hiyo inatekelezwa katika kila kijiji hapa nchini ambapo kwa Mkoa wa Singida
zaidi ya Sh. Bilioni 80 zimetumika kwa kazi hiyo ambapo alitumia nafasi hiyo
kuwaomba wanananchi kuendelea kuunga mkono jitihada anazozifanya Rais Samia na Chama
Cha Mapinduzi (CCM).
Mbunge wa Jimbo la Singida Kaskazini, Ramadhan
Ighondo akizunghumza kwenye hafla hiyo
alimuomba Naibu Waziri wa Nishati Judith Kapinga kuviongezea umeme vijiji uwe
na nguvu ili wananchi wake waweze kufungua viwanda ambavyo vitainua uchumi wao
baada ya kuanzisha viwanda vya kuzalisha bidhaa za aina mbalimbali.
Kwa upande wake Meneja wa TANESCO Kanda ya Kati,
Mhandisi DanstanNdamugoba alisema shirika hilo linaendelea kutoa huduma kwa
wananchi na kuwa Mkoa wa Singida una jumla ya vijiji 441 na mpaka sasa vijiji
437 vimewashwa umeme na vilivyobaki ni vijiji vinne tu na ifikapo June 15, 2024
vijiji vyote vitakuwa vinawaka umeme.
Naye Meneja wa Usimamizi wa Miradi Wakala wa
Nishati Vijijini (REA) ambaye alimwakilisha Mkurugenzi Mkuu REA, Mhandisi
Romanus Lwena alisema Wilaya ya Singida ina jumla ya vijiji 84 ambavyo
vimefikishiwa umeme kasoro vinne na kuwa vitongoji vipo 439 kati ya hivyo
vitongoji 275 tayari vimefikishwa umeme na ambavyobado ni 164.
“Nitoe wito kwa wananchi wa vijiji hivyo
kuwaeleza kwamba Serikali imetoa fedha nyingi kwa ajili ya kutekeleza miradi
hiyo akitolea kwa Wilaya ya Singida peke yake imetoa Sh.Bilioni 10 na kwa mkoa
wote wa Singida ni zaidi ya Sh. Bilioni 86 hivyo kwa yale maeneo ambayo tayari umeme
wamepata tunawaomba wananchi wajitokeze kuutumia kwa kuwekeza miradi mbalimbali
ya kiuchumi ili lengo la Serikali litimie,” alisema Mhandisi Lwena.
Baadhi ya wananchi wa vijiji hivyo wakizungumza kwa nyakati tofauti walimshuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwakamilishia mradi huo kupitia REA na Tanesco na kuwa sasa wanakwenda kubadilika kiuchumi kutokana na matumizi sahihi ya nishati hiyo.
Furaha ikitamalaki Kijiji cha Mdilu wakati wa hafla ya uwashaji wa umeme kijini hapo.
Meneja wa Usimamizi wa Miradi Wakala wa Nishati Vijijini (REA) ambaye alimwakilisha Mkurugenzi Mkuu REA, Mhandisi Romanus Lwena akizungumzia mradi huo.








No comments:
Post a Comment