BILIONEA MULOKOZI MFANYABIASHARA MZALENDO TEGEMEO LA WANA MANYARA - SINGIDANIBLOG

Habari za Hivi Punde

Post Top Ad

Friday, 27 September 2024

BILIONEA MULOKOZI MFANYABIASHARA MZALENDO TEGEMEO LA WANA MANYARA

Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Mati Super Brands  Ltd, David Mulokozi.

............................ 

Imeandaliwa na Dotto Mwaibale, (0754-362990)

Uzalendo ni hali ya mtu kuipenda, kuithamini na kujitoa kwa ajili ya nchi yake na Mzalendo wa kweli anaweka maslahi ya nchi mbele na yake binafsi yanakuwa nyuma. 

Mzalendo ni mtu yeyote mzawa wa nchi husika na mwenye kuipenda na kujitoa mhanga na saa nyingine ikibidi kufa kwa ajili ya nchi yake.

 Uzalendo unabeba dhana pana ikianzia asili, utamaduni, lugha, siasa, historia na kuwa dhana kuu ya uzalendo ni utaifa.

Kuna baadhi ya watu licha ya kuwa ni wazalendo ambao wapo tayari kupoteza maisha yao kwa ajili ya kutetea nchi yao uzalendo wao umekwenda mbali zaidi kwa  kujitoa kusaidia jamii bila ya kujali kipato chao cha fedha walichonacho.

Hapa nchini tunao viongozi wengi ambao ni wazalendo na waliokuwa wazalendo kama Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na wenzake wote waliombele za haki na wale ambao bado wapo hai.

Leo napenda kumuongelea David Mulokozi ambaye ni Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Mati Super Brands  Ltd yenye makao makuu yake Babati mkoani Manyara ambayo inazalisha na kusambaza vinywaji, pombe kali aina ya Strong Dry Gin, Sed Pineapple Flavour Gin, Strong Coffee na Tanzanite Premium Vodka..

Mfanyabiashara huyu Bilionea ni mtu ambaye anajitoa kusaidia jamii na makundi mengine kutokana na uzalendo wake alionao na si vinginevyo kwani kuna baadhi ya watu wataweza kuibuka na kusema amekuwa akifanya hivyo kwa sababu ya utajiri wa fedha alionao.

Tumewaona wafanyabiashara wengi aina ya Mulokozi ambao Mungu amewajaalia  kuwa na fedha lakini hawana uzalendo wowote kwa Taifa wala kusaidia jamii niseme tu kuwa kutoa ni moyo wa kizalendo alionao mtu husika na wala sio utajiri.

David Mulokozi ni Mfanyabiashara asiye na makuu ambaye anashirikiana na Serikali vizuri na makundi mengine ya watu na katika kuunga mkono jitihada za Serikali chini ya Rais Samia Suluhu Hassan kuhusu ajira kupitia kampuni yake hiyo ametoa ajira zaidi ya 300.

Binafsi napenda kusema kazi hii kubwa anayoifanya Mulokozi isibezwe bali aendelee kuungwa mkono kwani katika maisha ya kila mtanzania mwenye ajira kwenye familia yake hawapungui watu watano wanaomtegemea hivyo kupitia kampuni hiyo kuna watu wengi ambao wananufaika nayo zaidi ya hao waliopo kwenye ajira.

Kutokana na uzalendo huo mkubwa alionao Mulokozi kwa Taifa na jamii anatambulika na Serikali kwa kulipa kodi stahiki na ndio maana wakati wote viongozi wa Serikali na Chama Cha Mapinduzi wamekuwa wakiitembelea kampuni hiyo kuona uwekezaji uliopo ambao una mchango mkubwa wa kuinua uchumi wa nchi na Mkoa wa Manyara kwa ujumla.

Mulokozi kupitia kampuni yake hiyo ya Mati Super Brands  Ltd amekuwa akijitoa kwa dhati ya moyo wake katika hali ya raha na shida kusaidia jamii na makundi mengine hapa nieleze machache kati ya mengi ambayo yamefanywa na kampuni hiyo chini ya Mkurugenzi huyo Bilionea Mulokozi.

Moja ya jambo kubwa lililowahi kufanywa na kampuni hiyo kupitia mkurugenzi huyo ni pale alipotoa msaada wa vyakula na vitakasa mikono kwa ajili ya kujikinga na virusi vya corona. 

Vifaa vilivyo tolewa ni mchele, mafuta ya kula, sabuni na vitakasa mikono ambavyo vilotolewa kwenye vituo vya watoto yatima na wazee na vitakasa mikono kwa taasisi za serikali ambavyo vilipokelewa na aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Alexander Mnyeti. 

Mbali ya kutoa msaada huo pia kuna misaada minginemingi  amekuwa akiitoa kwa jamii na kwa makundi mengine ya watu wenye uhitaji. 

Mkurugenzi Mulokozi ni mtu mwenye huruma na maono ya mbali kwenye shughuli zake, mbali ya kujitoa kwake huko pia amekuwa mpenzi wa michezo na burudani ambapo amekuwa akishiriki katika mabonaza mbalimbali kwa kuzingatia kuwa michezo ni afya. 

Katika kupenda michezo Mulokozi alizindua Tawi la mashabiki wa timu ya Soka ya Fountain Gate FC Tawi la Babati mkoani humo likiwa na lengo la kuhamasisha vijana kupenda michezo na kuiunga mkono timu hiyo iliyohamia Mjini Babati katika Uwanja wa Tanzanite Kwaraa kutoka mkoani Mwanza.

Mulokozi alipongeza ubunifu wa vijana hao wa kuanzisha tawi hilo ambapo aliahidi kupitia kampuni yake hiyo kuwasaidia.

Mulokozi katika tukio lingine la kuonesha upendo ni lile alilolifanya la kutoa zawadi ya Bajaji mpya kwa Dereva wa bajaji Abel Rajabu ambaye alibandika picha ya Bilionea huyo kwenye bajaji yake baada ya kuvutiwa na kazi anazozifanya za kuwekeza kwenye viwanda na kusaidia jamii inayomzunguka kutokana na faida anayoipata.

Kutokana na kufanya vizuri kampuni hiyo imekuwa ikipongezwa na wadau ambao wamekuwa wakitambua mchango wake ambapo Taasisi ya Kijeshi ya Command and Staff college ilitoa tuzo kwa kampuni hiyo kutokana mchango mkubwa ilioutoa kwa taasisi hiyo.

Taasisi hiyo ilitunukiwa tuzo hiyo kutokana na mchango wake mkubwa  ilioutoa wakati wa mafunzo ya maofisa wa jeshi kutoka nchi mbalimbali waliyoyapata kwenye ziara maalumu ya kimafunzo kupitia kampuni hiyo ya Mati Super Brands Ltd. 

Akipokea tuzo hiyo Mulokozi alisema imewapa heshima kubwa na nguvu ya kuendelea kufanya kazi kwa bidii hasa zile zizazohusisha jamii.

Mafanikio hayo makubwa yanayopatikana ndani ya  kampuni hiyo hayapatikani hivi hivi bali yanatokana na uongozi mzuri wa Bilionea Mulokozi na timu yake ya watendaji kazi ambao wamekuwa wakiwezesha nyenzo mbalimbali za kazi ikiwa ni pamoja na kupatiwa zawadi na motisha kwa wafanyakazi bora.

Binafsi napenda kukuambia Mulokozi kazi unayoifanya inaonekana na jamii nzima ya watanzania hivyo endelea kuifanya kama unavyowiwa huku ukielewa kuwa hakuna kazi isiyo na changamoto Mungu aendelee kukupa afya njema na uendelee kuwatumikia wana Manyara na Taifa kwa ujumla tukijua kuwa wafanyakazi wote uliowapa ajira katika kampuni yako wanatoka mikoa mbalimbali hapa nchini. Kazi Iendelee.

Mmoja wa Viongozi wa Taasisi ya Kijeshi ya Command and staff College alipokuwa akimkabidhi tuzo Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Mati Super Brands LTD, David Mulokozi kutokana mchango mkubwa aliounyesha kwa  taasisi hiyo.

Mkurugenzi wa Kampuni ya Mati Super Brand, ya Mjini Babati mkoani Manyara, David Mulokozi (kushoto) alipokuwa akikabidhi vifaa mbalimbali kwa Serikali wakati wa ugonjwa wa COVID 19.

Mkurugenzi wa Kampuni ya Mati Super Brands Limited, David Mulokozi akipokea Certificate of Recognition kutoka Jeshi la Police Tanzania Mkoa wa Manyara. Kulia anayekabidhi cheti hicho ni aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Manyara,  Alexander Mnyeti.Aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mhe. Makongoro Nyerere (kulia) akipata maelezo kutoka kwa mkurugenzi wa kampuni hiyo, David Mulokozi wakati alipotembelea kiwanda hicho.

Viongozi mbalimbali wa Taasisi ya Kijeshi ya Command and Staff College wakiwa katika picha ya pamoja na uongozi wa Kampuni ya Mati Super Brands LTD baada ya taasisi hiyo kuitunuku tuzo ya heshima kampuni hiyo.

Mkurugenzi wa kampuni hiyo, David Mulokozi akimkabidhi zawadi ya Bajaji Abel Rajabu ambaye alibandika picha ya Bilionea huyo kwenye bajaji yake baada ya kuvutiwa na kazi anazozifanya za kuwekeza kwenye viwanda na kusaidia jamii inayomzunguka kutokana na faida anayoipata.
Mkurugenzi wa Kampuni ya Mati Super Brand, Bilionea David Mulukozi akiongoza moja ya mabonanza mkoani humo.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad