Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Dr. Ali Mohammed Shein iliyopo Wilaya ya Ikungi mkoani Singida, Jackson Maruma akizungumza katika mahafali ya 16 ya kidato cha nne yaliyofanyika Oktoba 2, 2025.
.................................
Dotto Mwaibale na Philemon Solomoni, Singida
KITUO cha kuibua vipaji vya mpira wa miguu kinachojulikana kwa
jina la Misughaa Sport Centre kilichoanzishwa Shule ya Sekondari ya Dr. Ali
Mohammed Shein iliyopo Wilaya ya Ikungi mkoani Singida kimeanza kuonesha tija.
Mkuu wa shule hiyo Jackson Maruma akizungumza wakati akitoa
taarifa ya shule hiyo kwenye mahafali ya 16 ya kidato cha nne yaliyofanyika
Oktoba 2, 2025 alisema kituo hicho kimeanza kuonesha tija.
Alisema kituo hicho kimepata usajili namba S13011 Misughaa Sports Centre chenye malengo
ya kuinua na kutengeneza vipaji vitakavyo tumika mashuleni na Taifa kwa ujumla.
“Ajenda yetu kubwa ni kuhakikisha wanafunzi wetu hapa shuleni
hawajihusishi tu kwa masuala ya taaluma madarasani bali ni pamoja na mambo ya vipaji mbalimbali ambavyo Mungu
amewapatia,” alisema Maruma.
Alisema dunia ya sasa mtu anaweza kufanikiwa katika nyanja
mbalimbali ikiwemo ya vipaji vya aina tofautitofauti kama muziki, kuigiza,
michezo na vingine vyote vyenye maslahi mapana kwa Taifa letu.
Mwalimu wa michezo wa shule
hiyo Protasi Hema alisema shule hiyo ilionesha kuwa na watoto wenye vipaji
ambapo alipeleka wazo hilo kwa mkuu wa shule hiyo Maruma ambaye alitoa baraka
zote za kuanzishwa kwa kituo hicho.
Hema alisema kituo hicho kilianza mwaka 2018 ambapo usajili wake
waliupata mwaka 2022.
“Kituo hiki kinachukua wanafunzi kutoka maeneo mbalimbali lakini
wengi wanatoka hapa Sekondari ya Dr. Ali Mohammed Shein,” alisema Hema.
Alisema wamekuwa wakiwapa majaribio ya aina mbalimbali ya kuibua
vipaji vya wanafunzi hao ambapo baadhi yao waliwapeleka timu ya Azam ijini Dar
es Salaam na Mbeya ambao wameonesha kufanya vizuri.
Mwalimu Hema alisema kituo hicho kinaendeshwa na shule lakini msaada
mkubwa unatoka kwa wazazi ambapo
alitumia nafasi hiyo kuwaomba wadau mbalimbali kusaidia kituo hicho ambacho ni
muhimu katika kukuza vipaji vya watoto.
Aidha, Hema alisema wanapo safiri kwenda mikoa mingine wamekuwa
wakisaidiwa na wadau mbalimbali na kueleza kuwa tangu kianzishwe kituo hicho
wamesafiri mara nne.
“Kwetu ni mafanikio makubwa na yenye tija na ni hatua nzuri
tunaomba wadau mbalimbali watushike mkono kwani mahitaji ya kituo chetu ni
makubwa mno changamoto tuliyonayo ni fedha za kukiendesha,” alisema.
Kiongozi wa wanafunzi hao, Haruna Said akizungumza kwa niaba ya
wenzake aliushukuru uongozi wa shule hiyo kwa kuanzisha kituo hicho ambacho
kinawaandaa vizuri kimechezo.
“Tuna mshukuru sana mkuu wa shule yetu Mwalimu Maruma kwa
kuanzisha kituo hiki tumeweza kusafiri kwenda Mbeya na Dar es Salaam kujipima
na timu kubwa kwetu ni fursa kubwa,” alisema.
Said aliwaomba wazazi na wadau mbalimbali kuendelea kuwaunga mkono
kwa hali na mali ili waweze kufika mbali kimichezo na kuwa wachezaji wa kitaifa
na kimataifa.







No comments:
Post a Comment