POLY MACHINERY YAJA NA MAPINDUZI YA TEKNOLOJIA KWA VIJANA, WANAWAKE - SINGIDANIBLOG

Habari za Hivi Punde

Post Top Ad

Thursday, 27 November 2025

POLY MACHINERY YAJA NA MAPINDUZI YA TEKNOLOJIA KWA VIJANA, WANAWAKE

Mmoja wa mwananchi akipata maelezo alipotembelea mabanda katika maonesho ya  mashine mbalimbali za kilimo, ufugaji na ujenzi zinazozalishwa na kusambazwa nchini na Kampuni ya Poly Machinery yaliyo andaliwa na kampuni ya Poly Machinery yanayoendelea Viwanja vya Nyerere Square Jijini Dodoma.

.....................................

Na Godwin Myovela, Dodoma 

Katika jitihada za kutimiza maono ya Dira ya Taifa 2550, kampuni ya Poly Machinery imedhihirisha kuwa teknolojia ya kisasa inaweza kuwa chachu ya maendeleo kwa wananchi, hususan vijana na wanawake.

Ofisi za kampuni hiyo zilizopo Dodoma zimekuwa kitovu cha ubunifu na mafunzo yanayolenga kuongeza tija katika sekta za kilimo, ufugaji, na ujenzi.

Baraka Mitimingi, Afisa Masoko wa Poly Machinery, amesema kila kukicha wanajitahidi kusaidia jamii kwa kubuni na kuzalisha teknolojia zilizo rahisi kwa matumizi na mtambuka kwa matokeo chanya, ustawi wa uchumi wa mtu mmoja na taifa kwa ujumla. 

Akizungumza jana ndani ya viwanja vya Nyerere Square kwenye maonesho ya Wakandarasi na Wasambazaji wa vifaa vya Ujenzi nchini, chini ya uratibu wa Mat Builders and Contractors Global Expo 2025 yanayoendelea, alihimiza watanzania kutembelea banda lao na kuona mashine na teknolojia mbalimbali zinazovutia.

Alisema kwa sasa wamebobea na kujikita kwenye uzalishaji na usambazaji wa mashine za kupiga na kusafisha karanga, mashine za kupukuchua na kusaga mahindi, pamoja na mashine za kukamua maziwa, alizeti na nafaka nyingine.

Aidha, kampuni imewasilisha mashine za ufugaji za kisasa, ikiwemo kunyonyoa kuku kwa mashine, kukata majani ya mifugo, na teknolojia za ufugaji nyuki na ulinaji asali kwa tija, hatua ambayo inarahisisha kazi ngumu kwa wanawake na kuongeza uzalishaji kwa wajasiriamali wadogo.

Maonesho haya pia yameonesha mashine za kuchanganya mchanga na saruji, kuchanganya zege, na mashine za ufungaji wa tofali, ambazo ni nyenzo muhimu kwa sekta ya ujenzi, na hivyo kutoa fursa ya kuongeza ajira na maendeleo ya jamii.

Kwa mujibu wa Mitimingi, teknolojia hizi si tu zinarahisisha kazi, bali pia zinatoa fursa kwa vijana kuingia katika uzalishaji wa thamani kubwa na kuanza biashara ndogo ndogo zenye faida endelevu.

Kwa wanawake, teknolojia hizi zinatoa nafasi ya kuingia katika sekta za kilimo na ufugaji kwa kutumia mashine zinazopunguza kazi ngumu na kuongeza tija, hatua muhimu katika uwezeshaji wa kijamii na kiuchumi.

Wataalamu wa Poly Machinery wamehimiza serikali na taasisi za umma kuhakikisha teknolojia hizi zinatumika kikamilifu, huku wakiunga mkono uwepo wa mafunzo ya kiufundi na urahisi wa kupata mashine kwa wingi.

Kampuni hiyo ina imani kwamba ushirikiano kati ya sekta binafsi na serikali ni muhimu katika kufanikisha maono ya taifa, huku ikiwataka vijana na wanawake kushirikiana na wajasiriamali wengine kutumia fursa hizi kuongeza tija na kipato.

Maonesho hayo pia yamekuwa jukwaa la kushirikiana, kujifunza, na kuona kwa vitendo jinsi teknolojia ya Poly Machinery inavyoweza kubadilisha maisha ya wananchi na kuimarisha uchumi wa taifa.

Hata hivyo, baadhi ya wadau waliotembelea banda hilo wametahadharisha kwamba teknolojia kama hizi zinapotekelezwa kikamilifu, zinachangia kwa kiasi kikubwa kufanikisha Dira ya Taifa 2550, kuongeza ushindani wa sekta za kilimo na ujenzi, na kutoa fursa ya biashara kwa vijana, wanawake na jamii nzima 

Washiriki wa maonesho hayo hayo wakitoa maelezo kwa Makamu Mwenyekiti wa Taasisi ya Mwalimu Nyererem Peter Mavunde ambaye alikuwa mgeni rasmi aliyetembea mabanda hayo

Makamu Mwenyekiti wa Taasisi ya Mwalimu Nyererem Peter Mavunde akioneshwa bidhaa zinazozalishwa na kampuni hiyo.
Maelezo yakitolewa na washiriki wa maonesho hayo.
 

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad