Afisa Mchambuzi Masuala ya fedha wa benki hiyo, Charles Kanuda, akizungumza kwenye Maadhimisho ya Wiki ya Fedha Kitaifa yanayoendelea viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara Jijini Tanga.
.......................................
Na Mashaka Kibaya,Tanga.
BENKI Kuu ya Tanzania (BOT) imewataka watu wanaojihusisha na
biashara ya kubadilisha fedha za kigeni kuacha mara moja vitendo hivyo.
Rai hiyo imetolewa na Afisa Mkuu Mwandamizi wa benki hiyo,
Mwile Kauzeni, wakati akizungumzia na Waandishi wa habari kwenye Maadhimisho ya
Wiki ya Fedha Kitaifa yanayoendelea viwanja vya Shule ya Sekondari ya Usagara
Jijini Tanga.
“ Tunawataka watu hao wanaojihusisha biashara hiyo kufuata sheria
ambayo itawawezesha kupata leseni inayoruhusu uendeshaji wa shughuli zao,”
alisema Kauzeni.
Mwile aliyasema hayo alipokuwa akijibu baadhi ya maswali ya
wanahabari waliotaka kujua hatua zinachukuliwa na benki hiyo katika kudhibiti watu
hao.
Alisema ili mtu afanye biashara hiyo anapaswa kufuata
taratibu za kisheria vinginevyo atakuwa ametenda kosa la jinai hivyo wenye nia
kuendesha shughuli hiyo watembelee matawi ya benki hiyo kwa maelezo zaidi.
Charles Kanuda ambaye ni Afisa Mchambuzi Masuala ya fedha wa
benki hiyo alisema Serikali imekuja na mfuko wa udhamini wa mikopo ambapo kwa
mtanzania anayehitaji huku akiwa hana dhamana toshelevu atapata dhamana mpaka
asilimia 75.
Kanuda alisema watu wengi wamekuwa wakijaribu kwenda kukopa
huku wakiombwa dhamana yenye thamani kubwa zaidi ya mikopo wanayohitaji hivyo
kushindwa kupata mikopo.
Amesema hali hiyo imewasababisha watanzania wengi kushindwa
kuchukua mikopo au kuchukua kiasi kidogo jambo ambalo limeathiri ufanisi wa biashara
zao wanazoziendesha.
Kauli Mbiu ya maadhimisho hayo ni “Elimu ya fedha , msingi
wa maendeleo ya kijamii na kiuchumi"
Kwa upande wake Mwalimu Mwajuma Kileo wa Shule ya Msingi
Mkwakwani jijini hapa alisema ameridhishwa na elimu aliyoipata baada ya
kutembelea banda la benki hiyo.
“ Kwa kutembelea banda hilo pamoja na wanafunzi wetu
wamejifunza namna ya kutambua fedha bandia mambo ambayo tulikuwa hawayajui
ingawa tulikuwa tukiwafundisha kupitia somo la uraia,” alisema Kileo.
Adrus Mahmoud (12) mwanafunzi wa darasa la sita wa Shule
hiyo alisema amefarijika kupatiwa elimu ya ziada juu ya kutambua alama za
kificho zilizomo kwenye noti hivyo kumsaidia kuzibaini.
Afisa Mkuu Mwandamizi wa benki hiyo, Mwile Kauzeni, wakati akizungumzia na Waandishi wa habari
Mwanafunzi Adrus Mahmoud (12), akizungumza.Mwalimu Mwajuma Kileo wa Shule ya Msingi Mkwakwani akizungumza.







No comments:
Post a Comment