MAKONDA ALIVYOPANGA KUBADILISHA TASNIA YA HABARI MTANDAONI NCHINI - SINGIDANIBLOG

Habari za Hivi Punde

Post Top Ad

Wednesday, January 14, 2026

MAKONDA ALIVYOPANGA KUBADILISHA TASNIA YA HABARI MTANDAONI NCHINI

Waziri wa  Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda akikabidhiana hati na aliyekuwa waziri wa wizara hiyo  Profesa Palamagamba Kabudi katika hafla ya makabidhiano ofisi iliyofanyika Januari 13, 2025 Jijini Dodoma.

.......................... 

Na Dotto Mwaibale

WAZIRI wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda ameonesha dhamira ya dhati ya kubadilisha Tasnia ya Habari Mtandaoni nchini kwa kutoa ahadi ya kuiomba Serikali kutenga Sh. bilioni moja hadi bilioni mbili kwa ajili ya kuwakopesha ili waweze kununua vifaa vya kufanyia kazi.

Makonda ameonesha dhamira hiyo Januari 13, 2026, wakati akizungumza na watumishi wa wizara hiyo Mtumba jijini Dodoma katika hafla ya makabidhiano ya ofisi kati yake na aliyekuwa Waziri wa Wizara hiyo, Profesa Palamagamba Kabudi.

“Mhe. Katibu Mkuu vijana wengi wa taifa letu wamejiajiri kwenye habari hasa online TV na wanaotumia mitandao ya kijamii tutaiomba mamlaka na Mhe. Rais anapenda sana vijana wa Social Media.

Nitaenda kumlilia atupatie fedha kiasi cha sh. bilioni moja hadi bilioni  mbili tuwakopeshe waandishi wa habari za mitandaoni waweze kununua vifaa vya kisasa vya kufanyia kazi,” alisema Makonda.

Alisema wakipata fedha hizo watawapatia waandishi hao ili wawe na vifaa vyao wenyewe na wanaporekodi wasitumie simu badala yake watumie kamera za kisasa,  na kompyuta nzuri na kuweza kutengeneza maudhui ambayo dunia itaiona Tanzania katika ubora  wake.

Ahadi hiyo ya Makonda inakwenda sanjari na maono ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Desemba 18, 2025 Katibu Mkuu wa wizara hiyo na Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari wa mitandaoni na bloga katika kikao kazi kilicho andaliwa na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) alitoa salamu za Rais kuwa ameomba waandishi hao walelewe.

Msigwa alisema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Samia imeendelea kuonesha dhamira ya dhati ya kulea na kuwawezesha waandishi wa habari wa mitandaoni na mabloga,

 Alisema Tanzania Bloggers Network (TBN) na Jukwaa la Mitandao Tanzania (JUMIKITA) kuwa ni wadau wakubwa wa serikali katika tasnia ya habari, akisisitiza kuwa mchango wao ni muhimu katika kusambaza taarifa na kujenga mawasiliano kati ya serikali na wananchi.

 

“Serikali imewaamini waandishi wa mitandaoni, sasa nanyi muendelee kuonesha imani kwa serikali. Ushirikiano wetu umeendelea kuimarika na changamoto zinazojitokeza tunazitatua kwa pamoja,” alisema Msigwa.

 

Aidha, Msigwa alieleza kuwa wizara hiyo ipo katika mchakato wa kuanzisha mfuko maalum kwa ajili ya kuwawezesha waandishi wa habari, hususan wa mitandaoni.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad