......................................
Kwa miaka mingi, biashara ya dhahabu nchini Tanzania ilikuwa ikifanyika kwa mfumo usio rasmi, hali iliyosababisha utoroshaji wa madini, unyonyaji wa wachimbaji wadogo na upotevu mkubwa wa mapato ya serikali. Hata hivyo, uanzishwaji wa masoko rasmi ya madini umeibadilisha kabisa taswira ya sekta hiyo, hususan katika mikoa ya kimadini kama Geita.
Kupitia masoko ya madini yanayosimamiwa na serikali, dhahabu imegeuka kutoka rasilimali iliyokuwa ikivuja kimya kimya na kuwa injini halisi ya uchumi, inayowanufaisha wachimbaji, wafanyabiashara na taifa kwa ujumla.
Sheria ya Madini Yatoa Msingi wa Mageuzi
Uanzishwaji wa masoko ya madini nchini unasimamiwa na Sheria ya Madini, Sura ya 123 ya Sheria za Tanzania ya mwaka 2010, kama ilivyorekebishwa mwaka 2017. Sheria hii iliweka misingi ya urasimishaji wa biashara ya madini kwa kusisitiza uwazi, uthaminishaji wa kitaalamu, bei elekezi na ukusanyaji wa mapato ya serikali.
Kupitia marekebisho hayo, serikali ilipata mamlaka ya kuanzisha masoko ya madini na vituo vya ununuzi karibu na maeneo ya uchimbaji mdogo ili kuwalinda wachimbaji dhidi ya unyonyaji na biashara haramu.
Geita Yajitokeza Kama Kitovu cha Dhahabu
Kwa mujibu wa Mujiolojia wa Mkoa wa Kimadini Geita, John Maganga, mkoa huo unasimamia masoko mawili ya madini pamoja na vituo tisa vya ununuzi wa dhahabu. Vituo hivyo vimeanzishwa karibu na maeneo yenye shughuli kubwa za uchimbaji mdogo ili kupunguza gharama na hatari kwa wachimbaji.
Kisheria, wachimbaji na wafanyabiashara kutoka mikoa mingine na hata nje ya nchi wanaruhusiwa kuuza dhahabu yao katika Soko Kuu la Madini Geita na Katoro kwa kulipa tozo stahiki.
Dhahabu Yazungumza kwa Takwimu
Katika kipindi cha miaka mitano kuanzia mwaka wa fedha 2021/2022 hadi 2025/2026 (hadi Desemba 31, 2025), masoko ya madini ya Mkoa wa Geita yameshuhudia mauzo ya dhahabu yenye:
Uzito wa kilo 14,762.67
Thamani ya shilingi trilioni 2.49
Takwimu hizi zinaonesha wazi mchango mkubwa wa masoko ya madini katika kuimarisha uchumi wa taifa na kuzuia utoroshaji wa madini.
Mapato ya Serikali Yaongezeka
Kwa mujibu wa Peter Jamhuri Nyawegana, Fundi Sanifu wa Tume ya Madini Mkoa wa Geita, serikali imefanikiwa kukusanya zaidi ya shilingi bilioni 168 kupitia mrabaha, ada za ukaguzi na tozo nyingine katika kipindi hicho cha miaka mitano.
Mapato haya yalikuwa yakipotea kabla ya kuanzishwa kwa masoko ya madini kutokana na biashara isiyo rasmi.
Wachimbaji Wadogo Wanufaika
Mwenyekiti wa Soko la Madini Geita, George Paulo Maloba, anasema masoko ya madini yamewawezesha wachimbaji wadogo kupata soko la uhakika, bei shindani na malipo ya haraka bila hatari ya wizi. Anaeleza kuwa soko hilo lina wafanyabiashara wakubwa wa dhahabu 95, hali inayoonesha ukuaji wa uchumi wa eneo hilo.
Wanunuzi wa dhahabu akiwemo Magambo N. Magambo, Mkurugenzi wa Gambo Mine Limited, wanakiri kuwa mfumo wa bei elekezi umeondoa unyonyaji na kuleta haki kwa wauzaji na wanunuzi.
Changamoto Zabaki, Maboresho Yatajwa
Pamoja na mafanikio hayo, changamoto bado zipo, hususan katika Mfumo wa Mineral Market Information Management System (MMIMS) unaohitaji kuboreshwa ili kuimarisha mtandao na ufanisi wa miamala.
Aidha, wachimbaji wadogo wakiongozwa na Hassan Sadick wameiomba serikali kushirikiana na mabenki ili kuwapatia mitaji na vifaa vya uchimbaji, hatua itakayoongeza uzalishaji na mapato ya taifa.
Hitimisho
Masoko ya madini yameleta mapinduzi makubwa katika biashara ya dhahabu nchini. Kwa kusimamia kikamilifu Sheria ya Madini, kuboresha mifumo ya TEHAMA na kuwawezesha wachimbaji wadogo kifedha, sekta ya madini itaendelea kuwa mhimili muhimu wa maendeleo ya uchumi wa Tanzania.
Makala hii imeandaliwa na Victor Bariety 0757856284












No comments:
Post a Comment