Na Dotto
Mwaibale, Dodoma
MWALIMU Helena
Mahamba wa Shule ya Msingi Unyakhae katika Manispaa ya Singida ambaye alikuwa
akisumbuliwa na ugonjwa wa kisukari kwa miaka 17 amefariki dunia katika
Hospitali ya Benjamin Mkapa alipokuwa akipatiwa matibabu.
Mahamba
ambaye alikuwa amelazwa ghorofa ya pili chumba namba mbili katika hosptali hiyo
amefariki Machi 28, 2026 saa 9 usiku.
Helena Mahamba
baada ya kushindwa kumudu gharama za matibabu alilazimika kubaki nyumbani
akijiuguza huku hali yake ikiendelea kudhoofu kila siku.
Taarifa zake zilipotolewa kwenye mitandao ya
kijamii akiomba msaada wa matibabu na kwa jitihada za Naibu Waziri wa Afya Dkt.
Florence Samizi alipoisoma taarifa hiyo aliagiza mgojwa huyo apelekwe Hospitali
ya Rufaa ya Mkoa wa Singida kuanza matibabu upya mara moja.
Pamoja na
kuanza matibabu hali yake iliendelea kuwa mbaya na Machi 14, alipata rufaa ya
kuhamishiwa Hospitali ya Benjamin Mkapa jijini Dodoma kwa ajili ya kuendelea
kupata matibabu.
Mwalimu
Mahamba wakati akipigania uhai wake akiwa nyumbani kwake eneo la Unyakhae alidai
kuwa tangu alipokuwa anaumwa katika kipindi cha miaka 17 Chama cha Walimu
Tanzania (CWT) Manispaa ya Singida kama
mwana chama wao kilimpatia Sh. 100,000 tu huku mwajiri wake naye akishindwa
kumsaidia.
Baadhi ya
viongozi wa chama hicho wakielezea suala hilo walisema katika katiba yao hakuna
kipengele ambacho kinaeleza mwanachama wao anapokuwa na changamoto yoyote
ikiwemo kuumwa apatiwe msaada na kama atapatiwa ni msaada tu wa vitu vidogo
vidogo kama matunda ambavyo atapatiwa kama hisani.
Kauli hiyo
iliwaibua baadhi ya walimu na kuomba katika
katiba yao kuwepo kipengele cha kuwasaidia walimu wanapo kuwa na changamoto
mbalimbali ikiwemo ya kuumwa kutokana na michango yao wanayoichangia kila
mwezi.
Mmoja wa Walimu
hao Robert Mtinga alisema katika Manispaa ya Singida wapo zaidi ya 800 na kila mwezi kila mmoja hukatwa siyo chini ya Sh. 33,000 na wale ambao
wapo daraja la juu hukatwa zaidi ya kiwango hicho na kueleza kuwa ni fedha
nyingi zinazokusanywa.
Aliongeza
kueleza kuwa yakipigwa mahesabu ni fedha nyingi ambazo zinapatikana katika manispaa hiyo ambapo wanaomba ziwe zinatumika kuwasaidia wanapokuwa na changamoto badala ya
kusubiri kusaidiwa jeneza na kusafirishwa kwenda makwao wakifariki.
Kwa upande
wake Mwalimu Helman Magoti alisema ni vema kuipitia katiba yao vizuri ili
kuielewa kama hakuna kipengele cha kutambuliwa wanapokuwa na changamoto ya
maradhi ili wapiganie kiwekwe kwa maslahi mapana ya walimu.
Mama wa
marehemu Helena, Regina Mahamba ambaye alikuwa akimuuguza amesema licha ya jitihada
kubwa zilizofanywa na wauguzi pamoja na madaktari wa hospitali hiyo katika
kumtibu binti yake hali ilibadilika na Machi 28, 2026 alifariki.
Mama Mahamba
amesema taratibu za mazishi zinafanyika nyumbani kwao Mkuhungu Chama jijini
Dodoma.
Buriani Mwalimu
Helena Mahamba mwendo umeumaliza kwa mateso makubwa, kapumzike kwa amani huku ukiwaachia walimu
wenzako changamoto ya kupigania haki na maslahi yao kwa mwajiri na CWT.
Bwana Alitoa
na Bwana Ametwaa jina lake Lihimidiwe Milele Daima.
Taarifa hii imeandikwa na Dotto Mwaibale simu namba 0754362990.







No comments:
Post a Comment