Wataalam wa
Afya katika vituo vya kutolea huduma (Hospitali, Vituo vya Afya, Zahanati n.k)
wamehimizwa kuzingatia matumizi sahihi ya vifaa tiba na vitendanishi ili
kupunguza malalamiko, madhara na matukio hasi. Ushauri huo umetolewa na Ndg.
David Robert Matle - Kaimu Meneja Ufuatiliaji wa Ubora, Ufanisi na Usalama wa
vifaa tiba na vitendanishi kutoka TMDA makao makuu Dodoma wakati akitoa mafunzo
kwa watoa huduma hao yaliyofanyika katika vituo 9 mbalimbali katika Wilaya ya
Ikungi Mkoani Singida kuanzia Aprili 08 hadi 10, 2026 kwa nyakati tofauti.
Bw. Matle,
amesema ya kuwa matumizi yasiyo sahihi yanaweza kusababisha madhara makubwa
yakiwemo malalamiko na matukio yatokanayo na matokeo yasiyo sahihi ya uchunguzi
na hata kuhatarisha maisha ya wanufaika (Mgonjwa).
"Vifaa tiba kama vile sindano, mashine mbalimbali za kupimia pamoja na vitendanishi vinavyotumika vinapaswa kutumika kulingana na miongozo iliyowekwa na watengenezaji" alisisitiza. Dkt. Nassoro Ally Matuzya
- Afisa Ufuatiliaji wa Ubora, Usalama na Ufuatiliaji kutoka TMDA Makao Makuu pia amesema matumizi sahihi ya vifaa tiba na vitendanishi si tu kwamba yanaongeza ubora wa huduma, bali pia yanaimarisha imani kwa jamii kwa watendaji katika sekta ya Afya nchini katika utekelezaji wa sera ya Afya kwa jamii.


















No comments:
Post a Comment