Mtoto Swaum Shabani Machela (14) akiwa amepakatwa na Mama yake Sauda Selemani nyumbani kwao Pugu kwa Mustafa, Ilala Jijini Dar es Salaam.
.............................
MTOTO Swaum
Shabani Machela (14) Mkazi wa Mtaa wa Kibong’wa Pugu kwa Mustafa Ilala
Jijini Dar es Salaam hajawahi kufurahia
maisha kutokana na maradhi ya usonji aliyonayo.
Swaum ambaye
wakati wote huwa anatabasamu huku akitamani kusimama na kutembea aweze kwenda
shuleni kama ilivyo kwa watoto wengine lakini imekuwa ni kinyume muda wote amekuwa
akilala kutokana na mwili wake kuwa dhoofu kwa maradhi hayo yaliyosababishwa na
ukosefu wa chakula bora.
Mama wa
mtoto huyo Sauda Selemani (39) anasema Swaum alizaliwa Septemba 2, 2013
nyumbani kwao katika Hospitali ya Magoma iliyopo Korogwe Mkoa wa Tanga.
Anasema
alizaliwa akiwa na afya njema na kurejea nyumbani kwake Manzese Jijini Dar es
Salaam alikokuwa akiishi na mume wake.
Sauda
anasema mwanaye alipofikisha miaka minne hali yake ilianza kubadilika kila
ilipofika usiku mwili wake ulikuwa ukipata joto kali na ndipo alipo mpeleka
Hosptali ya Mwananyamala.
Anasema daktari
aliyekuwa akimtibu alimuambia kuwa mwanaye alikuwa akisumbuliwa na nimonia
ambapo alilazwa kwenye chumba cha joto kwa miezi minne lakini hali yake
iliendelea kuteteleka.
Sauda anasema
walilazimika kwenda Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) ambapo waligundua
kuwa mwanaye alikuwa na utapiamlo ambao umemsababishia baadhi ya viungo vyake kudhoofu.
“Muhimbili nilikaa naye kwa wiki kadhaa akipatiwa chakula maalumu ambapo afya yake ilikuwa nzuri kidogo ingawa mwili wake ulikuwa hauna nguvu ndipo nilipompeleka Hospitali ya CCRBT Msasani kwa ajili ya kufanyiwa mazoezi ya viungo.
Daktari alimuambia
kutokana na lishe duni mtoto wake alikuwa amepatwa na usonji hivyo anatakiwa
kumkazania awe anapata chakula cha kutosha na kufanya mazoezi hali yake
itaimarika.
Sauda
anasema anapita katika wakati mgumu mume wake naye ni mgonjwa wakati wote
amekuwa na shinikizo la damu (presha) ambayo imekuwa ikimfanya awe anaanguka na
kupoteza fahamu, hana kazi ya uhakika ya kumuingizia kipato.
Anasema yeye
mwenyewe anachangamoto ya goti la mguu wa kulia kuvimba na kumsababishia
kushindwa kutembea na maisha yao kwa ujumla hayaeleweki hata kula yao ni ya
shida.
Mama huyo
mwenye watoto watano anasema kama angeweza kupata mtaji angefanya chochote ili
aweze kupata fedha za kuendesha maisha yao na kumtibu mwanaye lakini amekwama kwa vile hawana kitu
chochote cha kumuingizia kipato.
Aidha, Sauda
amesema daktari amemuambia mwanaye akipata lishe bora, dawa za kutumia na
kufanya mazoezi atapona, changamoto ni namna ya kupata fedha hizo.
“Swaum kutokana na hali yake mara nyingi amekuwa akizidiwa, juzi hali yake ilibadilika ghafla nikampeleka Muhimbili gharama ya dawa zake alizoandikiwa ilikuwa ni zaidi ya shilingi 75,000 nimeshindwa kuzinunua zaidi ya panado alizopewa,” alisema Sauda.
Alisema
changamoto nyingine aliyonayo ni namna ya kufika Hospitali ya Muhimbili
akizidiwa mwanaye hasa nyakati za usiku kwani wanalazimika kutoka saa 9 usiku
nyumbani kwao Pugu kwa Mustafa.
Mwenyekiti
wa Serikali ya Mtaa anaoishi Sauda Selemani, Shina namba 2, Emanuel Zakaria amethibitisha
mama huyo kuwa na changamoto ya kimaisha.
“Serikali ya Mtaa anapoishi Sauda Selemani na familia yake tunaifahamu changamoto aliyonayo ni kweli anahitaji kusaidiwa,” alisema Zakaria kwa niaba ya Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Kwa Mustafa, Fikiri Selemani (Timbwa).
Ndugu Watanzania mmemsikia Sauda madhira anayopitia na familia yake anaomba msaada ili
aweze kupata fedha au mtaji utakaomuwezesha afanye chochote ili apate fedha
zitakazomsaidia kumtibu mwanaye na kuendesha maisha yao ya kila siku kwani
kutoa ni moyo na wala siyo utajiri.
Kwa yeyote
atakayeguswa kuishika mkono familia hiyo kwa chochote utakachojaaliwa na
Mwenyezi Mungu hata kama utaona ni mdogo ziwe fedha, ushauri, chakula,
Sabuni, chumvi, sukari na mahitaji mengine ya kibinadamu kwake utakuwa ni msaada mkubwa.
Unaweza
kuwasiliana na mama huyo anayepita katika kipindi kigumu moja kwa moja kupitia namba ya simu
0623757336 au 0625414791 jina litakalotokea ni Sauda Selemani Magwelo, Mungu atakubariki kwa utoaji wako.
Mtoto Swaum Shabani, akionesha tabasamu la matumaini, anakuomba msaada wako wewe unayemuangalia, uwe baba, mama, dada, kaka, mtoto mwenzake, kiongozi wa dini, mwanasiasa, mfanyabiashara, mwanafunzi na jamii kwa ujumla. Usimuache mtoto huyu bila ya kufanya chochote juu yake hata Sh. 2000 kwake itampa faraja na matumaini. Wasiliana na mama yake kwa namba ya simu hapo juu utabarikiwa mara 1000 kwa utoaji wako.
Mama mzazi wa Swaum, Sauda Selemani, akiwa na Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa anaoishi Shina namba 2, Pugu kwa Mustafa Jijini Dar es Salaam, Emanuel Zakaria.........................
Taarifa hii imeandaliwa na Dotto Mwaibale namba ya simu 0754362990








No comments:
Post a Comment