Bibi Zaina Waziri Kipanga (88) Mkazi wa Kijiji cha Kwakombo Kata ya Kwakombo wilayani Korogwe mkoani Tanga, akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) alipokuwa akimuomba Rais Samia Suluhu Hassan aingilie kati mgogoro wa ardhi dhidi yake na Serikali ya Kijiji cha Kwamsisi.
...............................................
Na Dotto Mwaibale, Korogwe
BIBI kizee Zaina Waziri Kipanga (88) Mkazi wa Kijiji cha Kwakombo Kata ya
Kwakombo wilayani Korogwe mkoani Tanga amemuomba Rais Samia Suluhu Hassan aingilie
kati apate haki yake kufuatia Serikali ya Kijiji cha Kwamsisi kufyeka mazao ya
mahindi katika shamba lake kutokana na mgogoro wa ardhi dhidi yake na Serikali
ya kijiji hicho.
Kikongwe huyo amedai kwamba licha ya viongozi wa Wilaya ya Korogwe kuufahamu
mgogoro huo wameshindwa kumsaidia hali inayoonesha kuwa kuna njama za makusudi
za kutaka kumdhurumu shamba shamba lake.
Akizungumza na vyombo vya habari hivi karibuni Bibi Kipanga alisema
amelazimika kumuomba Rais amsaidie kwa kuwa hajui hatima ya maisha yake kwani hana chakula wala
shamba baada ya Serikali ya Kijiji cha Kwamsisi kumnyang'anya shamba lake la
ekari 12 alilokuwa akilitumia na mume wake Waziri Kipanga ambaye sasa ni
marehemu wakidai ni mali ya kijiji hicho.
Alisema kutokana na mgogoro huo mahindi aliyolima msimu huu wa kilimo yamefyekwa
na Serikali ya kijiji hicho na kutakiwa wasiingie kwenye shamba hilo ambalo
wamekuwa wakilima tangu wakati wa oparesheni vijiji iliyofanyika miaka ya 70.
Aliongeza kuwa viongozi hao wamekusudia kuwanyang'anya shamba lake hilo kwa
hila kwani katika shamba hilo kuna mazao yao ya kudumu kama miembe, minazi,
miti aina ya mitiki na makaburi ya familia hiyo.
Bibi Kipanga alisema kuwa kabla ya marehemu mume wake hajafariki wakiwa
nyumbani kwao na mke mwenzake walifika watu na kuwaambia kuwa wamepita kwenye
eneo la shamba hilo ambapo wamekuta kuna magari na watu wanajenga nyumba kwenye
shamba lao.
Alisema baada ya kuambiwa hivyo walikwenda katika eneo hilo na kukukuta ni
kweli kuna ujenzi ukiendelea na walipohoji waliambiwa kuwa kuna mradi wa
ufugaji wa ng' ombe wa maziwa unatarajiwa kuanzishwa kwenye hilo lakini
hawakuambiwa ni nani aliyetoa eneo kupisha mradi huo.
Alisema mradi huo haukuwahi kufanya kazi tangu wakati huo mpaka ikafikia
hatua ya majengo hayo yaliyojengwa kubomoka lakini wao na mume wao walikuwa
wakiendelea kulima katika shamba hilo hadi hivi sasa ambapo Serikali ya kijiji
hicho ilipoibuka na kudai ni la kwao na kufikia hatua ya kufyeka mazao yao huku
wakikata minazi na mazao mengine ya kudumu jambo ambalo linawashangaza.
Aliongeza kuwa suala hilo lilifikishwa hadi kwenye vyombo mbalimbali vya
sheria lakini Serikali ya kijiji hicho imeshindwa kuthibitisha uhalali wa kudai
shamba hilo ni lao.
Alisema ekari hizo 12 zipo ndani ya ekari nyingine 38 ambazo mradi huo
ulikuwa ufanyike lakini ekari hizo ziliuzwa na watu waliokuwa wakilima lakini
cha kushangaza waliouza wapo na wala hawajachukuwa hatua yoyote jambo ambalo
linaonesha kuna hila inafanyika dhidi yao.
Watoto wa bibi huyo, Said Waziri Kipanga, Mariam Waziri Kipanga, Mkiwa Waziri
Kipanga na Abdallah Waziri Kipanga ambao sasa ni watu wazima wanasema tangu
opareshini ya vijiji wakiwa watoto wazazi wao walikuwa wakiishi katika eneo
hilo na wanashngaa kuona Serikali ya kijiji hicho ikiwafukuza katika shamba lao
hilo.
"Tangu tukiwa watoto wazazi wetu walikuwa wakilima katika shamba letu
hilo namaliza shule naolewa na watoto wangu wanakuwa wanajua hilo shamba ni la
babu yao Mzee Kipanga inatushangaza kuona tukiambiwa tuondoke tuende wapi
tunakuomba Rais Samia Mama yetu wa huruma utusaidie tupate haki yetu,"
alisema Mariam Kipanga.
Said Kipanga ambaye ndie aliyechaguliwa kusimamamia mirathi baada ya baba
yao kufariki amesema amepata misukosuko mingi ikiwemo ya kuwekwa mahabusu mara
kwa mara kwa ajili ya kufuatilia jambo hilo.
Anasema licha ya kuweka tangazo la mirathi kwa muda wa miezi mitatu kuhusu mali za baba yao likiwemo shamba hilo
hakuna mtu yeyote ambaye alijitokeza kupinga lakini wanashangaa Serikali ya
kijiji hicho kuanza kujitokeza hivi sasa wakidai shamba hilo ni mali ya Serikali.
Mkazi wa kiji hicho Hemedi Mwigole ambaye alikuwa na shamba lake kwenye
eneo hilo linalodaiwa kuwa ni la mradi anasema familia hiyo haitendewi haki
kwani mashamba hayo yalikuwa ni ya wazazi wao tangu wakati wa opareshini vijiji
na kuwa baba yake ndiye aliyemkaribisha mzee Kipanga katika eneo hilo.
"Hapa kuna ujanja ujanja tu unafanyika mimi shamba langu nililiuza
sasa kama liklikuwa ni la Serikali mbona sijawahi kuulizwa na mtu yeyote na
Seriklali ya kijiji chetu ilikuwepo" alihoji Mwigole huku akitaka
wafuatiliaji wa jambo hilo waingie kiundani kupata historia ya mashamba hayo.
Mwenyekiti Mstaafu wa Kijiji hicho, Hamadi Mwinyimsanga tangu aliyeshika
madaraka tangu mwaka 1983 hadi mwaka 2006 anasema kwa kipindi chote hicho cha
nyuma hakukuwepo na chokochoko hizo za kudai shamba la familia ya Kipanga ni
mali ya kijiji na wala hakuwahi kuona vielelezo vyovyote vinavyoonesha uhalali
huo.
"Sisi wakati wa uongozi wetu kwa kuzingatia shamba hilo lilikuwa
likitumiwa na familia hiyo tangu wakati wa oparesheni vijiji na baada ya kuona
hakuna mradi unaoendelea katika eneo hilo licha ya kujengwa miundombinu kama
josho na mabanda tuliridhia familia hiyo kuendelea kulima shamba hilo ambalo
lilikuwa na ekari zaidi ya 15 hivi," alisema Mwinyimsanga.
Alisema mradi huo haukufanikiwa kutokana na kutokidhi kwa vigezo na hata
kwenye ramani ya kijiji hicho hakuna sehemu inayoonesha kuwepo kwa mradi na
baada ya hapo kila mtu aliyekuwa na shamba lake kwenye eneo hilo aliendelea
kulima huku wengine wakiyauza.
Mwinyimsanga anasema tangu mwaka 1972 hadi alipokuwa akistaafu nafasi yake
ya Mwenyekiti mwaka 2006 hakukuwepo na changamoto yoyote kuhusu shamba hilo na
hata viongozi wengine waliofuatia waliendelea kuiachia familia hiyo kuendelea
kulitumia shamba hilo la marehemu baba yao.
Alisema mamlaka mbalimbali zimejaribu kulifuatilia jambo hilo lakini bado haioneshi kama haki
inatendeka kwa familia hiyo ambapo baadhi ya viongozi wa kijiji hicho
wakituhumiwa kuhusishwa na njama za kunyang'anya shamba hilo kwa ajili ya
kujijenga kisiasa wakitaka kutumia eneo
hilo kwa ajili ya kuanzisha mnada.
Mwenyekiti wa Kijiji hicho, Salehe Msisi akizungumzia suala hilo alisema
wakati anaingia madarakani alikabidhiwa eneo hilo na viongozi waliomtangulia
likiwa na miundombinu ya josho na baadhi ya mabanda na alielezwa kuwa ni mali
ya Serikali hata hivyo hakuweza kueleza kama kijiji hicho kina hati ya umiliki
wa eneo hilo.
Msisi alipotakiwa kuzungumzia ufyekaji ya mazao yaliyo pandwa na familia
hiyo alisema wamekuwa wakilifanyia usafi eneo hilo lakini hajawahi kupata
taarifa yoyote ya mazao kufyekwa.
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Korogwe, Tito Mganwa akizungumzia
kuhusu mgogoro huo alikiri kuufahamu na
kueleza kuwa eneo hilo ni mali ya halmashauri hiyo na awali lilikuwa
likimilikiwa na Serikali ya kijiji cha Kwamsisi na lilikuwa na miundombinu ya
mifugo kama josho na nyumba ya mtumishi.
Alisema katika eneo hilo kuna ekari kama 50 ambazo halmashauri hiyo
imetenga kwa ajili ya kuanzisha mnada kwa ajili ya kuendeleza uchumi wa
wananchi wa kijiji hicho cha Kwamsisi na kuwa wamekwisha tenga fedha na mwaka
huu wa fedha wa 2023/ 2024 wanatarajia kujenga miundombinu kwa ajili ya kuanza
rasmi mnada huo.
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Korogwe, Tito Mganwa akizungumzia kuhusu mgogoro huo.







No comments:
Post a Comment