Kamanda wa Polisi Mkoa wa Singida Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Stella Mutahibirwa (kulia) Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani mkoani hapa Mrakibu wa Polisi (SP) Nestory Didi (kushoto) na Mkaguzi wa Polisi, Miguta Kubilu na mmoja wa dereva wa mabasi makubwa wakiangalia kipimo cha kupima kubaini kama dereva amekunywa kilevi wakati wa operesheni ya ukaguzi wa magari na utoaji wa elimu kwa abiria iliyofanyika Disemba 19, 2023 Stendi Kuu ya Mabasi ya Misuna.
.......................................................
Na Dotto Mwaibale, Singida
JESHI la Polisi Mkoa wa Singida kupitia Kikosi cha Usalama Barabarani kwa
kushirikiana na Mamlaka ya Udhibiti Usafiri wa Nchi Kavu (LATRA) linaendelea na
operesheni maalum ya kukagua mabasi na madereva kama wamekunywa pombe ili
kudhibiti ajali ambazo zimekuwa zikijitokeza kipindi cha kuelekea sikukuu za
mwisho wa mwaka.
Pia, LATRA na jeshi hilo wanaendelea kutoa elimu kwa madereva,makondakta wa
mabasi na kwa abiria ili wanapoona dereva anaendesha mwendo kasi ambao
unahatarisha usalama wao waweze kutoa taarifa .
Akizungumza wakati akiongoza operesheni hiyo iliyofanyika Kituo Kikuu cha
Mabasi Misuna, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Singida, Kamishna
Msaidizi wa Polisi (ACP), Stella Mutahibirwa
alisema operesheni hiyo wanayoifanya inalenga kuhakikisha magari yote
yanayoingia Mkoa wa Singida yanaingia na kutoka yakiwa salama.
Alisema katika operesheni hiyo wamebaini kuwa mabasi mengi hayana mikanda
ya usalama na iliyopo ni mibovu na akaongeza kuwa changamoto nyingine ni wazazi
wanaposafiri na watoto wao zaidi ya wawili kutowakatia tiketi za siti zao jambo
ambalo sio nzuri kiusalama .
Alisema madereva wanapoingia katika kituo hicho cha mabasi huwapima kama
wamekunywa pombe kwa kutumia kifaa maalumu na kutoa elimu kwa abiria kuwa
wanaposafiri na kuona dereva anakwenda mwendo wa kasi watoe taarifa kwa jeshi
la polisi kupitia namba za wakuu wa jeshi hilo zilizopo kwenye mabasi hayo.
” Sisi Jeshi la Polisi jukumu letu ni kulinda maisha ya raia na mali zao
hivyo tumeamua kufanya operesheni hii ya kutoa elimu kwa abiria ili waweze
kujua haki zao na kutoa taarifa pale wanapoona madereva wakiendesha mwendo
kasi," alisema Mutahibirwa.
Alisema wamezungumza na abiria na madereva kuhusu wajibu wao wanapokuwa
wanaendesha magari na kuwataka kuzingatia sheria na kanuni zilizowekwa za
usalama barabarani na kuhakikisha wanawafikisha abiria wao salama wanakokwenda na
kuwa kauli mbiu yao ya mwaka huu inasema ‘ukimya wako ni umauti wako paza sauti.
Aidha, Mutahibirwa alisema abiria
nao wanajukumu la kuwasaidia jeshi la polisi kukemea maovu yanayofanyika pindi wanapokuwa kwenye
safari yakiwemo ya mwendo kasi na dereva anayeyapita magari mengine kwa wakati
mmoja na eneo ambalo sio sahihi.
Aliwataka abiria wakati wote wanaposafiri kujenga tabia ya kufunga mikanda
ambayo imewekwa mahususi kuwasaidia pale gari husika litakapopata changamoto ya
dereva wake kusisima kwa ghafla au kupata ajali.
"Jambo la kwanza unapopanda ndani ya gari ni kuhakikisha unafunga mkanda
kwenye siti yako na kama haina mkanda ni vema ukatoa taarifa kwa
kondakta," alisema Mutahibirwa.
Mutahibirwa aliwaambia abiria hao wawe wasaidizi wa jeshi la polisi kwa
kutoa taarifa kuhusu uendeshaji usiofaa wa dereva husika na kuwa maisha yao
yanathamani sana kwao na kwa taifa hivyo aliwaomba wapaze sauti wanapoona mambo
hayo ambayo yanaweza kuhatarisha maisha yao.
Afisa Mfawidhi wa Mamlaka ya Udhibiti Usafiri
Ardhini (LATRA), Mkoa wa Singida, Layla Dafa akizungumza kwenye operesheni hiyo
alisema wamekuwa wakiyakagua mabasi hayo ili kubaini makosa mbalimbali ambayo
yanafanywa na madereva na makondakta moja ya makossa hayo ni kutowakatia abiria
tiketi za kielektoniki ambapo wamewasisitizia sana abiria kutumia tiketi hizo
ili wasizidishiwe nauli wanaposafiri.
Aidha, alisema wamewaelekeza
makondakta na madereva wanapoweka mizigo ya abiria chini ya buti wawe wanaweka
alama za kuonesha majina ya wenye mizigo hiyo wanaosafiri nao ili kuepusha
kuchukuliwa na abiria wengine na kuwa mizigo inakuwa chini ya dhamana yao hivyo
wanapaswa kuitunza.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa
Umoja wa Mawaka wa Mabasi Stendi Kuu ya Misuna, Msafiri Ndui alisema wakati
wote unapofika msimu wa abiria wengi baadhi ya mawakala wasiowaaminifu wamekuwa
wakipandisha bei ya nauli lakini wao wamekuwa wakidhibiti hali hiyo kutokana na
utaratibu waliojiwekea.
“Tunautaratibu wetu tuliojiwekea hairuhusiwi kupandisha nauli na ni lazima abiria aandikiwe bei elekezi na akitokea wakala kukiuka kuna adhabu zetu ambazo tumeziweka,” alisema Ndui.







No comments:
Post a Comment