MBUNGE GWAU ATOA TAARIFA YA UTEKELEZAJI WA SHUGHULI ZA MAENDELEO JIMBONI - SINGIDANIBLOG

Habari za Hivi Punde

Post Top Ad

Thursday, 28 December 2023

MBUNGE GWAU ATOA TAARIFA YA UTEKELEZAJI WA SHUGHULI ZA MAENDELEO JIMBONI

Mbunge wa Viti Maalum wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Singida, Martha Gwau akitoa taarifa ya utekelezaji wa shughuli mbalimbali za chama na maendeleo alizozifanya katika kipindi cha mwaka 2022/ 2023 katika kikao maalumu cha Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) kilichofanyika Disemba 23, 2023.

..................................................

Na Dotto Mwaibale, Singida

MBUNGE wa Viti Maalum (CCM) Mkoa wa Singida, Martha Gwau ametoa taarifa ya utekelezaji wa shughuli mbalimbali za chama na maendeleo alizozifanya katika kipindi cha mwaka 2022/ 2023.

Akitoa taarifa hiyo katika kikao maalumu cha Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) Mkoa wa Singida kilichoketi Disemba, 23, 2023 alianza kwa kutoa pongezi kwa Wanawake wa Mkoa wa Singida kwa kujitoa kwa wingi na mapokezi mazuri  walioyafanya kwa viongozi mbalimbali wa kitaifa waliofika kwa  ziara za kikazi mkoani hapa kwa nyakati tofauti na kuufanya mkoa wa Singida kung'ara ukilinganisha na mikoa mingine.

Alitaja ziara za viongozi hao kuwa ni ile aliyoifanya Rais Samia Suluhu Hassan, aliyekuwa Katibu Mkuu wa CCM Taifa, Daniel Chongolo na Mwenyekiti wa UWT Taifa, Mary Chatanda.

Gwau akielezea baadhi ya mambo aliyochangia ni michango ya vikao vya chama kuanzia ngazi ya wilaya na mkoa kwa kutoa fedha kwa ajili ya kununulia chakula. maji na mahitaji mengine ikiwemo mchango wa uchaguzi wa chama kuanzia ngazi za matawi, kata, wilaya na mkoa.

Alitaja kazi zingine alizozifanya ni kufanya ziara tofautitofauti na viongozi mbalimbali wa kitaifa waliofika mkoani hapa kama Daniel Chongolo, Mary Chatanda na Rais Samia Suluhu Haasan na kukagua utekelezaji wa Ilani ya CCM.

Gwau alitaja mambo mengine aliyofanya ni uchangiaji wa shughuli za maendeleo kama ujenzi wa miundombinu.ujenzi wa nyumba za makatibu wa chama katika wilaya tano kwa awamu ya kwanza na kuwa Wilaya ya Manyoni hakuweza kuchangia kutokana na eneo la ujenzi kuwa na mgogoro ambapo alisema atatoa mchango mwingine kwa awamu ya pili wakati wa ukamilishaji wa ujenzi wa nyumba hizo.

Aidha, Gwau alisema kazi nyingine aliyoifanya ni kushiriki kuwaingiza wanachama wapya wa UWT kwa kutoa kadi 2500 kwa awamu ya kwanza kwa mwaka 2023 na kuwa kwa mwaka 2024 atafanya hivyo tena lengo likiwa ni kuwa na wanachama wengi watakaokisaidia chama.

Alitaja kazi nyingine aliyoifanya ni kufanya ziara ya kupita kila kata japo si kwa asilimia 100 lengo likiwa ni kuonana na viongozi wa jumuiya ya wanawake ambao wanazijua changamoto zilizopo kwenye maeneo yao kwa kuzingatia kuwa wao ndiyo wamepewa dhamana ya uongozi na kuwa alipokea asilimia 95 za changamoto.

Alizitaja baadhi ya changamoto alizozipokea kuwa ni kutokuwa na vifaa vya kufanyia kazi, matawi yao kuwa mbali na kata, kutokuwa na sare ambapo pia walibainisha changamoto za miundombinu ya barabara, maji na umeme.

"Nikiwa mbunge nilifanya ziara hiyo kwa lengo la kujua maeneo na miundombinu na kupata fursa ya kukutana na madiwani wa maeneo husika ambao walinieleza changamoto zilizopo na ziara hii niliifanya kwa miezi minne kwa mkoa wote," alisema Gwau.

Alisema jambo lingine alililolifuatilia ni mikopo ya asilimia nne kwa wanawake, asilimia nne kwa vijana na asilimia mbili kwa walemavu ambayo ilisimamishwa na Serikali na kuwa amekuwa akifuatilia kujua lini itarejeshwa na kutakuwa na vigezo gani kwa ajili ya kuipata.

Gwau alisema changamoto zingine alizozipokea katika ziara zake hizo ni kutokuwa na uwanja wa ndege wa uhakika mkoani hapa, kushuka kwa bei ya zao la alizeti, miundombinu ya barabara, umeme, maji na zile zilizohusu sekta ya elimu.

Mwenyekiti wa UWT Mkoa wa Singida, Martha Mayaga akizungumza kwenye mkutano huo wakati akitoa salamu za chama aliishukuru Serikali chini ya Rais Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha nyingi za kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo na akaomba jitihada hizo zinazofanywa na Rais zinapaswa kuungwa mkono na kila mpenda maendeleo.

Mayaga aliwataka wanawake hao kuwa na umoja na kushirikiana katika kila jambo na kukifanya chama hicho kiendelee kushika kutawala nchi.



Katibu Mpya wa UWT Mkoa wa Singida, Mwasiti Ituja akiwa kwenye kikao hicho.

 Wajumbe wakishiriki kwenye kikao hicho.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad