...........................
Na Dotto Mwaibale
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Hanang’ mkoani Manyara, Teresia Irafay, amewaalika wapangaji wote wa vibanda vya Stendi ya Zamani kuhudhuria kikao maalumu kitakachofanyika Februari 21, 2026.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kitengo cha Habari cha halmashauri hiyo, kikao hicho kinalenga kujadili changamoto za maeneo ya biashara pamoja na kuweka utaratibu bora utakaosaidia kuondoa malalamiko yanayohusu upangaji.
Taarifa hiyo imeeleza kuwa agenda kuu za kikao ni pamoja na kutoa maelezo ya historia ya upangaji wa vibanda hivyo, kujadili changamoto zilizopo, kupokea maoni na mapendekezo ya wadau, pamoja na kufafanua mfumo wa ulipaji wa madeni.
Imebainishwa kuwa katika kikao hicho watakuwepo viongozi na wataalamu kutoka idara husika kwa lengo la kusikiliza hoja na changamoto za wapangaji, huku majadiliano ya wazi yakitarajiwa kufanyika ili kupata suluhisho la pamoja.
Kikao hicho kitafanyika katika viwanja vya Stendi ya Zamani kuanzia saa 3:00 asubuhi, na wadau wote wanahimizwa kuhudhuria kwa wingi.








No comments:
Post a Comment